Waadventista Wasabato wanaamini kwamba Yesu ni Mungu kamili kama mmoja wa wanachama wa Utatu pamoja na Mungu Baba na Roho Mtakatifu. Yuko na jukumu kuu ndani yake.
Tunaamini kwamba ingawa Yesu ni Mungu kamili, Alikuja duniani kama mtoto mchanga (Luka 1:30–33), ambaye kisha alikua mtu mzima na kuishi na kufa kama binadamu kama sisi tulivyo (Wafilipi 2:5–8).
Ili kukusaidia kuelewa vipengele hivi viwili muhimu vya Yesu, tutajadili:
- Uungu wa Yesu
- Maana ya Yesu kuwa “Mwana pekee wa Mungu”
- Kwa nini uungu wake ni muhimu
- Ubinadamu wa Yesu
- Kwa nini alikuja duniani
- Kwa nini uanadamu na uungu wake bado ni muhimu leo
Ubinadamu kamili na uungu kamili wa Yesu ni muhimu sana kwa Mwadventista wa Sabato kufahamu Mungu ni nani, jinsi anavyotupenda, na jinsi mpango wa wokovu unavyofanya kazi.
Hapa ni taarifa rasmi kuhusu imani hii kama ilivyopatikana kwenye tovuti ya kanisa:
Mungu Mwana wa Milele alikuwa mwili katika Yesu Kristo.
Kupitia Yeye vitu vyote viliumbwa, tabia ya Mungu inafunuliwa, wokovu wa binadamu unatimizwa, na ulimwengu unahukumiwa.
Milele kweli Mungu, alikuwa pia kweli binadamu, Yesu Kristo. Alikuwa mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu na kuzaliwa na bikira Mariamu. Aliishi na kujaribiwa kama binadamu, lakini akawa kielelezo kamili cha haki na upendo wa Mungu. Kwa miujiza yake alionyesha nguvu za Mungu na akathibitishwa kama Masihi aliyeahidiwa na Mungu.
Aliteseka na kufa kwa hiari msalabani kwa ajili ya dhambi zetu na mbadala wetu, akafufuliwa kutoka kwa wafu, na kupaa mbinguni ili kutumika katika patakatifu pa mbinguni kwa niaba yetu. Atakuja tena kwa utukufu kwa wokovu wa mwisho wa watu wake na urejeshaji wa vitu vyote.
Tuangalie kwa undani zaidi.
Uungu wa Yesu Kristo ni hakika

Photo by Megan Watson on Unsplash
Biblia inafundisha kwamba Yesu ni Mungu (Yohana 1:1), na kwa Waadventista wa Sabato, Biblia na Biblia pekee ndiyo chanzo cha mafundisho na matendo yetu yote (2 Timotheo 3:16).
Tunapata ushahidi wa asili ya kimungu ya Kristo hata katika Agano la Kale.
Katika moja ya unabii wa kimasihi maarufu zaidi (ukimtaja Yesu kama Masihi), nabii Isaya aliandika:
“Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli” (Isaya 7:14, UV030).
Jina Imanueli lina maana ya “Mungu pamoja nasi.” Hapa tunapata tamko la mara ya kwanza la Mungu kuzaliwa katika ubinadamu.
Karne nyingi baadaye, Agano Jipya linarejea moja kwa moja kwenye maandiko ya Agano la Kale:
“Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa Mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi” (Mathayo 1:23, UV030).
Tangu mwanzo katika Agano Jipya, Yesu anaitwa Mungu—hata akiwa mtoto mchanga.
Kweli, neno la kawaida la Kigiriki kwa Mungu katika Agano Jipya ni theos. Hapa ndipo neno theolojia, ambalo maana yake ni utafiti wa Mungu, linapotoka. Na mara nyingi, Yesu anatajwa katika Biblia kama theos.
Kwa mfano, wakati Tomaso—ambaye alijulikana kama “Tomaso Mwenye Shaka”—hatimaye alimtambua Yesu aliyefufuka, alipaza sauti akimwambia, “Bwana wangu na Mungu wangu [theos]” (Yohana 20:28, UV030)! Kumbukumbu moja kwa moja ya Yesu kama Mungu.
Mtume Paulo aliandika:
“…. alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili. Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu [theos], mwenye kuhimidiwa milele. Amina” (Warumi 9:5, UV030).
Paul hata ananukuu Agano la Kale katika Waebrania 1:8, ambayo pia inamrejelea Mwana kama Mungu:
“Lakini kwa habari za Mwana asema, Kiti chako cha enzi, Mungu [theos], ni cha milele na milele” (UV030).
Hii inalinganisha Yesu na Mungu Mwenyewe.
Mtume Petro pia anatoa maoni kuhusu Yesu kama Mungu:
“Simoni Petro, mtumwa na mtume wa Yesu Kristo, kwa wale waliopata imani moja na sisi, yenye thamani, katika hali ya Mungu wetu, na Mwokozi Yesu Kristo” (2 Petro 1:1, UV030).
Yesu ni Mungu na Mwokozi. Kwa kweli, sababu pekee ambayo anaweza kuwa Mwokozi wetu ni kwa sababu yeye ni Mungu.
Je, Yesu aliwahi kujiita Mungu?

Photo by Tim Wildsmith on Unsplash
Katika maeneo mengi katika Agano Jipya, Yesu hutumia neno “Mimi Ndiye” kwa njia ambazo zinakumbusha jina linalotumiwa na Mungu Mwenyewe kujirejelea alipokuwa akizungumza na Musa na Waisraeli.1
Paul Peterson, profesa wa Agano Jipya katika Chuo Kikuu cha Andrews, anasema:
“Madai kadhaa mengine ambayo Yesu alifanya alipotumia neno ‘Mimi Ndimi…’ yanamaanisha kiwango kikubwa sana cha mamlaka ambacho kawaida ni cha Mungu pekee. Yesu ndiye ‘…njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi’ (Yohana 14:6). Yeye ni ‘ufufuo na uzima’ (Yohana 11:25) na ‘mkate wa uzima’ (Yohana 6:48).”2
Moja ya mifano yenye kuvutia zaidi ya matumizi haya ilikuwa wakati Yesu alikuwa katika mjadala na viongozi wa kidini. Yesu alisema:
“Ibrahimu, baba yenu, alishangilia kwa vile atakavyoiona siku yangu; naye akaiona, akafurahi. Basi Wayahudi wakamwambia, Wewe hujapata bado miaka hamsini, nawe umemwona Ibrahimu?” (Yohana 8:56-57,UV030).
Yesu alijibu vipi?
“Yesu akawaambia, Amin, amin, naambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko” (Yohana 8:58, UV030).
Kwa Kiingereza, neno “Mimi ndiye” linaonekana kuwa rahisi sana. Lakini jibu la viongozi wa kidini linasema kila kitu:
“Basi wakaokota mawe ili wamtupie;” (Yohana 8:59, UV030).
Kwa nini wangeweza kutaka kumuua Yesu isipokuwa waliamini alijifanya kuwa Mungu? Alisema tu “MIMI NDIYE,” na walielewa hili kama Yesu akijirejelea Mungu, Mungu wa milele aliyeongea na Musa kutoka kwenye kichaka kilichowaka moto.
Zamani katika Agano la Kale, Mungu alipomwambia Musa kwamba yeye ndiye atakayewaongoza waisraeli kutoka Misri, Alitumia neno “MIMI NDIYE”:
“… Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? Niwaambie nini?” (Kutoka 3:13, UV030).
“Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu” (Kutoka 3:14, UV030).
Kisa kingine ambapo Yesu anajiita Mungu ni katika Ufunuo.
Ufunuo 1:8 unasoma:
“Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, asema Bwana Mungu, aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja, Mwenyezi” (UV030).
Huyu ndiye Bwana, “Mwenyezi,” akijitambulisha kama “Alfa na Omega, Mwanzo na Mwisho.”
Baadaye katika Ufunuo 22:13, Yesu pia anasema:
“Mimi ni Alfa na Omega, Mwanzo na Mwisho, wa kwanza na wa mwisho” (UV030).
Yaani, Yesu anasema, “Mimi ni Mungu.”
Na kama Mungu ndiye Muumba wetu, je, Yesu pia?
Yesu ndiye Muumbaji?
Huku Mungu Baba akirejelewa kwa kawaida (na kwa usahihi) kama Muumba, vivyo hivyo Yesu, Mwana wake (Yohana 1:1–5).
(Na vivyo hivyo Roho Mtakatifu, kwa sababu watu wote watatu wa Utatu walihusika.)
Tambua matumizi ya viwakilishi vya wingi katika kisa cha Uumbaji:
“Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; ….” (Mwanzo 1:26, UV030).
Kuna aya chache zaidi katika Maandiko ambazo zinamhusisha Mungu Baba na Mungu Mwana katika jukumu la muumba:
“Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu” (Waebrania 1:1–2, UV030).
“Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika“ (Yohana 1:1–3, UV030).
Maneno yote ya Kigiriki yanayotumika kwa Mungu katika mifano hii yanatoka kwa theos. Hata Yohana anasema wazi kwamba “Neno alikuwa Mungu [theos]” (Yohana 1:14 inaonyesha wazi kwamba Neno ndiye aliyegeuka kuwa mwili na damu ya binadamu.)
Maandiko pia yanasema kwamba “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika” (Yohana 1:3, UV030).
Kwa hivyo, chochote “kilichofanyika”—chochote ambacho hapo awali hakikuwepo lakini kikaja kuwepo—kilifanyika hivyo tu kupitia Yesu. Ili hili liwe kweli, Yesu lazima awe amekuwepo daima.
Lakini kama hivyo ndivyo ilivyo, kwa nini Mungu Baba anamwita Yesu Mwana wake?
Inamaansha nini kuwa Yesu ni “mwana pekee wa Mungu”?

Photo by wisconsinpictures on Unsplash
Kwa sababu Biblia inaeleza wazi Yesu kama Mungu amekuwepo daima, cheo chake kama “Mwana wa Mungu” au “Mwana pekee” inahusiana na jukumu lake la kutimiza ahadi maalum ya wokovu kwa watu wake, kama ilivyokuwa kwa Isaka kuwa “mwana pekee” wa Ibrahimu (Waebrania 11:19).
Andiko la Biblia linalomwita Yesu “Mwana pekee wa Mungu” ni aya maarufu, Yohana 3:16:
“Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele” (UV030).
Neno “Mwana pekee” kwa hakika linasikika kana kwamba Yesu alitokea baada au kutoka kwa Baba, sivyo?
Hapa ndipo ambapo ufahamu kidogo wa lugha ya asili unavyosaidia.
Neno la Kigiriki, monogenes, lililotafsiriwa katika tafsiri za Biblia kama “aliyezaliwa pekee,” halimaanishi kuzaliwa au uzazi.
Badala yake, neno hilo linamaanisha “mmoja wa aina yake” au “pekee.
Ni kuhusu asili ya kitu, sio kuhusu uumbaji wake. Mono kwa Kigiriki inamaanisha “moja,” kama vile Mungu mmoja, na genes inamaanisha “aina.” Pamoja, yanamaanisha “mmoja wa aina yake.”
Kwa mfano mwingine, tuchunguze Waebrania 11:17:
“Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee” (UV030).
Mwana pekee? Lakini Abrahamu alikuwa na mwana mwingine, Ismaeli. Na baadaye alikuwa na wana wengine zaidi (Mwanzo 25:1–4).
Hivyo, vipi Isaka angeweza kuwa mwana wake pekee, kama vile mwana pekee aliyezaa?
Hakuweza, na hakuwa. Msisitizo hapa ulikuwa kwenye hadhi ya pekee ya Isaka. Alikuwa mwana—mwana pekee—ambaye angekuwa mrithi wa ahadi za agano zilizofanywa na Ibrahimu (Mwanzo 17:19).
Wazo la Yesu kama “Mwana pekee aliyezaliwa” linamaanisha jukumu lake pekee kama Mwana wa Mungu katika mpango wa wokovu. Anatimiza ahadi ya agano la Mungu kwetu la kutuma Mkombozi (Mwanzo 3:15). Haina uhusiano wowote na asili yake.
Asili yake, kama ilivyozungumziwa awali, ni kutoka milele, hata kabla ya uumbaji wa ulimwengu. Na kama Baba, Yeye ni wa milele na mungu.
Kwa nini Uungu wa Kristo ni muhimu

Photo by Aaron Burden on Unsplash
Uungu wa Kristo una maana kwamba Mungu Mwenyewe, sio kiumbe wa chini, alikufa msalabani kwa ajili yetu. Na alifanya hivi ili sisi kama wenye dhambi tuwe na ahadi ya uzima wa milele pamoja naye.
Maana kubwa ya hii inaonyeshwa katika aya kama zifuatavyo:
“Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi” (Warumi 5:8, UV030).
“Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi” (1 Timotheo 1:15, UV030).
Inaonyesha zaidi upendo mkubwa wa Mungu kwa binadamu wote:
“Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?” (Warumi 8:32, UV030).
Ingekuwa ni udhalilisho usio na mwisho Kwake kuwa binadamu tu. Lakini kujitoa Mwenyewe kama dhabihu kwa ajili yetu alipokuwa hajafanya kosa lo lote? Alipofanikiwa pale tuliposhindwa? Ni jambo lisiloweza kufikirika kuhusu Mungu wa ulimwengu kutupenda sisi kiasi hicho.
Waadventista wanauona uzuri wa upendo huu unaotoka katika maisha na dhabihu ya Yesu.
Sasa, hebu tufunue zaidi kuhusu ubinadamu Wake.
Yesu alikuwa binadamu kamili
Waadventista wanaamini kwamba ingawa Yesu Kristo alikuwa Mungu kamili, pia alikuwa mwanadamu kamili.
Lakini hiyo ingewezekanaje?
Hatuelewi.
Kama vile hatuelewi sababu ya sheria ya mvuto (gravity) kufanya kazi kama inavyofanya. Lakini kutokuelewa kwetu kuhusu jinsi mvuto unavyofanya kazi haimaanishi kwamba hauifanyi kazi.
Na kama vile hatuwezi kuelewa kabisa mvuto, kuna mambo mengi ambayo hatuelewi kabisa kuhusu ulimwengu wetu na kuhusu Mungu aliyeumba vyote hivyo. Hivyo ndivyo ilivyo linapokuja swala la asili ya Yesu kama Mungu na mwanadamu.
Pamoja na uungu wa Kristo, Maandiko yanathibitisha ubinadamu wa Yesu.
Vitabu vingi vya Biblia katika Agano la Kale na Jipya la Biblia vinaelezea Bwana Yesu Kristo kama Mwana wa Adamu, ikionyesha ubinadamu wake (Danieli 7:13; Luka 21:27).
Biblia inaonyesha kwamba ingawa Yesu daima alikuwa Mungu, hakuwa daima mwanadamu. Alichukua umbo la kibinadamu na kuzaliwa kati yetu katika mazingira ya unyonge (Luka 2:7).
Aliendelea kukua na kujifunza kama sisi (Luka 2:52); alikuwa na ndugu kama sisi tulivyo na ndugu (Marko 6:3); alilia kama binadamu tunavyolia (Yohana 11:35); alichoka kama sisi tunavyochoka (Yohana 4:6); alijaribiwa kama binadamu wanavyojaribiwa. Tofauti pekee ilikuwa kwamba hakuwa amefanya dhambi kamwe (Waebrania 4:15).
Uanadamu wa Kristo ulijaribiwa kwa nguvu jangwani wakati shetani alipotaka kumjaribu baada ya kuwa na njaa na dhaifu baada ya siku 40 za kufunga (Mathayo 4:1–10).
Jambo muhimu kuzingatia ni kwamba Yesu alijaribiwa kama binadamu. Alikuwa na mwili, mifupa, damu, homoni, hisia, na tamaa. Alikuwa binadamu. Na hata hivyo katika ubinadamu wake, Yesu hakuanguka kwa majaribu.
Aliutumia Neno la Mungu kama ulinzi wake dhidi ya kuanguka na kutenda dhambi.
Kwa mfano, wakati shetani alipotaka kumfanya autilie shaka utambulisho wake kama Mwana wa Mungu, Yesu alijibu, “Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu” (Mathayo 4:4, UV030).
Hakika alishinda majaribu, pia alituonyesha jinsi sisi binadamu tunavyoweza kushinda pia.
Kama binadamu, Yesu hakutumia faida yoyote ya uungu wake kwa sababu sisi binadamu hatuwezi kufanya hivyo. Alitegemea kabisa Mungu Baba na Roho Mtakatifu, kama tunavyopaswa sisi pia.
Hapa kuna maandiko zaidi kuhusu ubinadamu wa Yesu:
“Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi” (Waebrania 2:14, UV030).
“Hivyo ilimpasa kufananishwana ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake” (Waebrania 2:17, UV030).
“Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu” (1 Timotheo 2:5, UV030).
Hivyo unaweza kujiuliza, kama Yeye alikuwa Mungu kama Baba, kwa nini alikuja duniani kuwa binadamu? Na kwa nini ni Yeye pekee, na sio mwingine yeyote katika huo Utatu?
Tutachunguza hiyo baadaye.
Kwa nini Yesu alikuja duniani badala ya Mungu Baba?

Photo by Nico Ehmann on Unsplash
Wakristo wanaamini Yesu alikuja duniani kwa sababu mbili:
- Kuishi maisha bila dhambi ili Astahili kujitoa kwa ajili yetu
- Kuwa mfano kwetu
Alitujia kuwa kielelezo kamili cha maana ya kuishi maisha ya imani na utii.
Kama mwanadamu, Alipitia majaribu na vishawishi sawa na sisi sote. Tofauti ni kwamba Hakuanguka kwa vishawishi hivyo. Aliishi kwa kutii kabisa mapenzi ya Mungu Baba na kutupa nguvu ya kufanya vivyo hivyo.
Hapa kuna njia nyingine ya kufikiria juu ya Yesu kama kielelezo chetu:
Karibu jamii zote zina mahusiano yanayohusisha mamlaka— mzazi/mtoto, mfanyakazi/mwajiri, n.k.
Vivyo hivyo, Mungu hutuita tuwe watoto wake na warithi pamoja na Yesu.3 Na Yesu, kama Mwana wa Mungu, alikuja kutufundisha kuwa hivyo—kuwa watoto wanaopenda na kumtii Mungu.
Kwa kuelewa hili, angalia maandiko yafuatayo yanayoonyesha utii wa Yesu kwa Baba.
“Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika?” (Mathayo 26:53, UV030).
“Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe” (Mathayo 26:39, UV030).
“Kwa kuwa mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka” (Yohana 6:38, UV030).
Kwa kunukuu Zaburi 40:7, Paulo anarejelea jinsi Yesu alivyokuja duniani kutimiza unabii wa Agano la Kale kumhusu kuwa Mwokozi wetu na kutii mapenzi ya Baba yake:
“Kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema,
Dhabihu na toleo hakutaka,
Lakini mwili uliniwekea tayari;
Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo;
Ndipo niliposema, Tazama,
nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa)
Niyafanye mapenzi yako, Mungu” (Waebrania 10:5–7, UV030).
Katika jukumu lake kama Mwokozi wetu, mbadala, na kielelezo, Yesu aliishi kwa umoja kamili na Baba, kutuonyesha jinsi ya kufanya vivyo hivyo.
Zaidi kuhusu jinsi uungu na ubinadamu wa Yesu unavyotuathiri kibinafsi.
Kwa nini uungu na ubinadamu wa Yesu Kristo bado ni muhimu leo
Ubinadamu wa Yesu ndio kiungo muhimu kati ya Mungu na sisi. Na uungu wake unatuunganisha na mbinguni.
Pamoja, kati ya uungu na ubinadamu wa Kristo, tuko na hakika ya ukaribu wa Mungu na ufahamu wa tunachopitia. Na hivyo ni kwa sababu Mungu Mwenyewe alipitia shida, majaribu, na mateso katika ubinadamu wa Yesu.
Yesu alikuja katika mwili wa kibinadamu, kama binadamu, ili awe mbadala wetu kamili na mfano wetu kamili.
Yeye alikuwa binadamu pekee aliyeishi bila dhambi. Ndiyo sababu yeye pekee angeweza kuwa mbadala wetu na kufa msalabani ili kutupatia haki yake kamili (Waebrania 4:15).
Hii ni muhimu kwa mpango wa wokovu.
Sisi kama binadamu tumetenda dhambi, na, kama matokeo, tunakabiliwa na adhabu ya kifo. Tunastahili hilo. Kama Biblia inavyosema, “….mshahara wa dhambi ni mauti” (Warumi 6:23, UV030).
Lakini kwa sababu Yesu alishuka na kuishi kama mmoja wetu, Alionja mauti kwa ajili yetu:
“ila twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu, aionje mauti kwa ajili ya kila mtu” (Waebrania 2:9, UV030).
Na Yeye ni kielelezo chetu kwa sababu alituonyesha maana ya kuishi kwa imani. Yohana aliiweka wazi kwamba tunapaswa kufuata mfano wa Yesu alipoandika:
“Yeye asemaye ya kuwa anakaa ndani yake, imempasa kuenenda mwenyewe vile vile kama yeye alivyoenenda” (1 Yohana 2:6, UV030).
Kwa kweli, katika udanganyifu wa mwisho wa siku za mwisho, watu wa Mungu wanatajwa kama wale wanao “…. wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu” (Ufunuo 14:12, UV030).
Watakuwa na imani inayolingana na imani ya Yesu—imani inayowawezesha kushika sheria ya upendo ya Mungu. Kama vile Yesu alivyofanya.
Ili kupata machapisho zaidi kuhusu Yesu,
Chagua Masomo ya Biblia Mtandaoni
Unataka kuendelea kujifunza? Pata habari zaidi kuhusu Yesu, mwanadamu, mpango wa wokovu, na jinsi Mungu anavyokupenda kiasi cha kutosha kujitolea kila kitu, ili tu kukupatia nafasi ya kumchagua.
Wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kujua pa kuanzia, ndio maana tunatoa chaguo za masomo ya Biblia mtandaoni bure, rahisi kutumia, unaweza kufanya wakati wowote, mahali popote, na kwa kasi yako mwenyewe.
Shule hii ya Biblia mtandaoni itakuelekeza kupitia mada kuu za Maandiko, ikivunja dhana ngumu za Biblia katika vipande vidogo, ambavyo vinaweza kukusaidia kupata majibu ya maswali magumu zaidi ya maisha.
Kurasa Zinazohusiana
Majibu Zaidi
Wanavyoamini Waadventista Wa Sabato Kuhusu Huduma ya Yesu Katika Patakatifu pa Mbinguni
Waadventista Wasabato wanaamini, kulingana na kitabu cha Waebrania, kwamba Yesu yuko katika patakatifu pa mbinguni—au hekaluni—sasa hivi.
Waadventista wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Pambano Kuu (Wema na Uovu)?
Pambano Kuu” ni msemo ambao Waadventista wa Sabato kawaida huutumia kuelezea mgogoro wa kiroho wa ulimwengu kati ya nguvu za mema (Mungu) na nguvu za uovu au dhambi (Shetani/iblis).
Waadventista Wa Sabato wanaamini nini kuhusu Ubatizo?
Kama Wakristo wengi wa Kiprotestanti ulimwenguni kote na katika historia, Kanisa la Waadventista wa Sabato linaamini katika ubatizo, sherehe ambapo watu huzamishwa ndani ya maji kudhihirisha hadharani “kufa kwa maisha ya zamani” na “kuanza kwa maisha mapya katika Kristo”.
Waadventista Wasabato wanaamini nini kuhusu Biblia?
Biblia ndiyo msingi wa kila kanuni na mafundisho ya Waadventista wa Sabato.
Waadventista Wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Mamlaka ya Biblia?
Jifunze jinsi kitabu kimoja cha zamani sana (Biblia) kilivyo msingi pekee wa imani zote za Waadventista wa Sabato.
Je, Waadventista Wasabato Wanaamini Wao Pekee Ndiyo Watakao Kwenda Mbinguni?
Hapana, Waadventista hakika hawaamini kwamba wao ndio pekee watakao kwenda mbinguni. Kwa kweli, hatuamini kwamba kupokelewa mbinguni kunategemea kanisa au madhehebu tunayohusiana nayo.
Je, Waadventista Wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Uumbaji Katika Biblia?
Waadventista Wa Sabato wanaamini kwamba Mungu ndiye Muumbaji wa ulimwengu. Wanafikia hitimisho hili kutoka kitabu cha kwanza cha Biblia—Mwanzo.
Namna Waadventista Walivyojifunza Fundisho la Patakatifu na Maana Yake
Wakati Waadventista wanapozungumzia “fundisho la Patakatifu,” wanarejelea dhana kwamba hekalu la mbinguni linafunua mpango wa wokovu











