Mifano ya matendo na maneno yanayounda tabia ni muhimu katika aina yoyote ya mfumo wa imani kwa sababu yanatokana na imani hizo. Waadventista wa Sabato wanatazama Biblia, pamoja na Yesu kama mfano kamili, kwa mwongozo wa kutengeneza tabia zetu za kila siku.
Tunaamini pia kwamba tabia njema haimwokoi mtu yeyote—badala yake, ni ushahidi wa maisha ambayo yameokolewa. Tabia inaathiriwa vyema mtu anapozama katika upendo wa Mungu na Roho Mtakatifu anavyofanya kazi moyoni.
Tutachunguza kwa karibu zaidi:
- Uhusiano kati ya mtindo wa maisha ya Kikristo na wokovu
- Kwa nini mtindo wa maisha ya Kikristo ni muhimu kwa Waadventista
- Kanuni za tabia ya Kikristo tunazozithamini
Lakini, kwanza tazama kauli rasmi ya Kanisa la Waadventista Wa Sabato kuhusu tabia ya Kikristo:
“Tunaitwa kuwa watu watakatifu ambao wanafikiri, kuhisi, na kutenda kwa kulingana na kanuni za Kibiblia katika maeneo yote ya maisha binafsi na ya kijamii.
Ili Roho abadilishe tabia yetu ionekane kama ile ya Bwana wetu, tunajihusisha tu na mambo yatakayozalisha usafi, afya, na furaha ya Kristo katika maisha yetu.
Hii inamaanisha kwamba burudani na starehe zetu zitimize viwango vya juu vya ladha na uzuri wa Kikristo.
Huku tukitambua tofauti za kitamaduni, mavazi yetu yawe rahisi, yenye adabu, na safi, yanayowafaa wale ambao uzuri wao wa kweli haupo katika mapambo ya nje bali katika pambo lisiloharibika la roho ya upole na utulivu.
Pia inamaanisha kwamba kwa kuwa miili yetu ni hekalu la Roho Mtakatifu, tunapaswa kuitunza kwa busara. Pamoja na mazoezi ya kutosha na kupumzika, tunapaswa kutumia lishe lenye afya zaidi iwezekanavyo na kujiepusha na vyakula vilivyoorodheshwa kuwa najisi katika Maandiko. Kwa kuwa mvinyo, tumbaku, na matumizi yasiyo na dhamira ya dawa na madawa ya kulevya ni hatari kwa miili yetu, tunapaswa kujiepusha navyo pia.
Badala yake, tunapaswa kushiriki katika chochote kinachotuleta katika nidhamu ya Kristo, ambaye anatamani afya yetu, furaha, na wema.”
Kwa muhtasari huu, tuanze kwa kuelewa uhusiano kati ya mtindo wa maisha na wokovu.
Kuna uhusiano gani kati ya mtindo wa maisha ya Kikristo na wokovu?

Photo by Yannick Pulver on Unsplash
Waadventista wanafahamu kwamba tumaini letu pekee la wokovu kutoka dhambini linatokana na kifo cha Yesu Kristo kwa ajili yetu. Tunadai zawadi hii kwa imani, ikimaanisha kwamba wokovu haupatikani kwa kutii sheria au kutekeleza mtindo wa Kikristo kikamilifu. Badala yake, mtindo wetu wa maisha ni matokeo ya asili ya wokovu huo.
Hatuwezi kuwa wenye haki—au kufanya mambo sahihi—kwa uwezo wetu wenyewe. Kama mtume Paulo alivyoandika,
“kwa sababu hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki mbele zake kwa matendo ya sheria; kwa maana kutambua dhambi huja kwa njia ya sheria. Lakini sasa, haki ya Mungu imedhihirika pasipo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii; ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote waaminio” (Warumi 3:20–22, SUV).
Tabia yetu haituletei “haki ya Mungu.” Tunapokea haki hiyo kupitia Yesu—Yeye huchukua maisha yetu ya dhambi na kutupa haki yake tunapokubali zawadi ya uzima wa milele kwa imani.
Lakini swali la tabia katika maisha ya Kikristo linahusiana sana na kile Kristo alichofanya kwa ajili yetu.
Na “tabia” hapa haihusu tendo moja tu.
Ni kuhusu tabia, vipaumbele, na mienendo. Hii ni kwa sababu Mungu mara chache alitoa kipaumbele kwa matendo makubwa ya watu lakini mara nyingi alitambua wale ambao kwa kimya na kwa uaminifu walikuwa wanatenda mema.
Yakobo 2 inatusaidia kuelewa jinsi imani na matendo vinavyokwenda pamoja. Imani ina nafasi muhimu sana katika wokovu, lakini “Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake” (Yakobo 2:17, SUV).
Kama vile “Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa” (Yakobo 2:26, SUV).
Lakini matendo mema sio sababu ya wokovu. Ni mwitikio wa upendo kwa wokovu tulioupata tayari katika Yesu Kristo. Ni ushahidi wa Roho Mtakatifu anayefanya kazi ndani yetu.
Kwa maneno mengine, mtindo wa maisha unaomcha Mungu utafuata imani ya kweli inayoishi.
Tazama kifungu hiki katika kitabu cha Agano Jipya cha Warumi:
“Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu” (Warumi 12:1-2, SUV).
Warumi inachukuliwa kuwa kitabu cha Biblia kinachotoa moja ya mafundisho wazi na yenye kina zaidi kuhusu wokovu kwa imani pekee. Je, kwa nini pia ina wito wenye nguvu wa kumheshimu Mungu kwa jinsi tunavyoishi?
Sababu ni hii:
Injili na mpango mzima wa wokovu unahusu urejesho—na kukomesha uovu, mateso, na kifo. Mwanadamu alianguka dhambini, lakini Yesu anafanya kazi ya kuturejesha sisi na ulimwengu wetu katika hali yake ya awali.
Ingawa mchakato huu mwishowe unamalizika na uumbaji wa mbingu mpya na nchi mpya, Mungu anaanza kazi hiyo ya urejesho ndani yetu sasa.
Kumpokea Kristo hubadilisha maisha yetu:
“Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya” (2 Wakorintho 5:17, SUV).
“Mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba” (Wakolosai 3:10, SUV).
Kwa nini mtindo wa maisha ya Kikristo ni muhimu kwa Waadventista?
Waadventista wanaamini kwamba mtindo wa maisha wa Kikristo unaruhusu kuishi maisha ya furaha zaidi na yenye kuridhisha ambayo Mungu anatamani kwa ajili yetu. Pia unaturuhusu kuishi kulingana na kanuni za Injili na kuwa mashahidi kwa wasioamini. Kushuhudia wema na upendo wa Mungu kwetu katika Yesu.
Kanuni hii inarudi hadi siku za mwanzo za Israeli ya kale.
Kulingana na Biblia, taifa hili lilikuwa limekusudiwa kuwa mfano kwa ulimwengu. Mfano wa jinsi inavyoonekana kumjua na kumtumikia Mungu wa kweli na muumba wa vitu vyote.
Walitakiwa kuishi maisha safi na kudumu kuwa waaminifu kwa Mungu katikati ya mataifa yanayowazunguka yaliyojaa ibada ya sanamu na dini za uwongo. Walikuwa wameitwa kuwa “nuru ya mataifa” (Isaya 49:6, SUV)—na neno Mataifa likimaanisha mataifa yasiyo Wayahudi.
Ndio maana kabla hawajaingia katika nchi ya ahadi, Musa aliwaagiza:
“Angalieni nimewafundisha amri na hukumu, vile vile kama BWANA, Mungu wangu, alivyoniamuru, ili mzitende katika nchi mwingiayo ili kuimiliki. Zishikeni basi, mkazitende, maana hii ndiyo hekima yenu na akili zenu, machoni pa mataifa watakaozisikia amri hizi zote, nao watasema, Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na akili” (Kumbukumbu la Torati 4:5–6, SUV).
Kuna mambo mawili muhimu hapa.
Kwanza, Mungu aliwapa Waisraeli “amri na hukumu.”
Kwa ufupi, hizi zilikuwa maelekezo kuhusu tabia na mtindo wao wa maisha: jinsi ya kula, nini cha kula, jinsi ya kuvaa, jinsi ya kuwatendea wengine—vyote hivyo!
Pili, walipaswa kufuata kwa uangalifu kanuni hizi za mtindo wa maisha na tabia.
Sababu gani?
Kufanya hivyo kutafunua “hekima yao na ufahamu [wao] mbele ya watu watakaosikia amri hizi zote, na kusema, Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na ufahamu.”
Haikuwa tu kuhusu kuwa na kanuni. Bali, ilikuwa ni kuishi kanuni hizo ndizo zingekuwa ushuhuda kwa ulimwengu karibu yao wa wema na ukuu wa Mungu wao.
Karne nyingi baadaye, Yesu alieleza wazo hilo kwa namna rahisi zaidi aliposema:
“Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni” (Mathayo 5:16, SUV).
Na Paulo anaeleza wazo hilo hilo:
“Yatendeni mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu” (Wafilipi 2:14–15, SUV).
Lakini huenda ukajiuliza…kwa sababu Waadventista wanafuata kanuni za tabia ya Kikristo, je hii inamaanisha tunajiona bora kuliko wengine?
Hapana kabisa.
Tunaelewa kile Biblia inachosema kuhusu asili ya dhambi ya binadamu—kwamba sisi sote ni wenye dhambi tunahitaji neema ya Mungu (Warumi 3:9).
Na Mungu anapenda watu wote sawa na anataka mema kwa sisi sote. Yesu alikuja ili kila mtu aweze kuwa na “uzima, na… wawe nao tele” (Yohana 10:10, SUV).
Kufuata kanuni za Biblia katika tabia na mtindo wetu wa maisha huturuhusu kupata uzoefu wa maisha yaliyoahidiwa na Yesu.
Kisha, kadri wasio Wakristo wanavyoona faida tunazopokea kutokana na jinsi tunavyoishi, watakuwa na shauku. Watakuwa wakivutwa kujifunza zaidi kuhusu imani yetu na kwa nini. Na hii inatupa fursa ya kushiriki kuhusu Yesu na yote aliyotufanyia.
Lakini hatujaribu kulazimisha matarajio yetu ya kiroho au kitamaduni kwa wale ambao hawaja zoea au bado wanajifunza. Ni jukumu la Roho Mtakatifu kuwaongoza watu kwenye ukweli na kuwashawishi kubadilika.
Basi, sasa tukishaelewa kwa nini mtindo wa maisha ya Kikristo ni muhimu kwa Waadventista, hebu tuangalie kanuni maalum kadhaa.
Kanuni gani za tabia ya Kikristo waadventista wanathamini?
Waadventista wanathamini kanuni za tabia ya Kikristo zinazohusiana na mahusiano, huduma, burudani, muonekano, na afya. Lakini wanatambua kwamba tabia yote inaanzia ndani—katika mawazo na imani.
Matendo huanzia moyoni (Mathayo 15:19), ndio maana Mithali 4:23 inatuhimiza kulinda mioyo yetu kwa bidii. Lazima tuwe makini na kile tunachoruhusu kiingie ndani yetu.
Hatimaye, kanuni zote za tabia ya Kikristo zinatokana na kazi ya ndani ya Roho Mtakatifu.
Wakati Roho Mtakatifu anabadilisha mioyo yetu, tunapata tunda la Roho: “upendo, furaha, amani, uvumilivu, fadhili, wema, uaminifu, upole, kiasi” (Wagalatia 5:22–23, SUV).
Kanuni hizi zinaongoza maamuzi yetu yote, kama tutakavyoona katika sehemu zifuatazo.
Mahusiano
Linapokuja swala la mahusiano, mara nyingi tunafikiria kuhusu “Sheria ya Dhahabu” – kuwatendea wengine kama tunavyotaka watutendee. Lakini Biblia inachukua hatua zaidi ya hii:
“Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine” (Wafilipi 2:3-4, SUV, msisitizo umeongezwa).
Tunaitwa kuwatanguliza wengine, kuwatendea kwa upendo wa kujitoa kama wa Kristo (1 Wakorintho 13:4–8; 16:14).
Katika Waefeso 4:2, Paulo anatuhimiza kuwajibu wengine kwa unyenyekevu na upole.
Na mazungumzo yetu ni muhimu pia. Wakati Roho Mtakatifu anafanya kazi ndani yetu, tutazungumza maneno ya hisia na neema, yakiinua wale wanaotuzunguka (Waefeso 4:29; Wakolosai 4:5–6).
Huduma

Photo by Artūras Kokorevas
Mwenendo wa Kikristo ni wa ukarimu badala ya tamaa. Mungu ndiye mmiliki wa kila kitu, na ametupa uwakili wa vitu vingi—muda wetu, pesa zetu, mali zetu, nguvu zetu.
Mungu anataka ukarimu wetu wa vitu hivi uanze moyoni. 2 Wakorintho 9:7 inahimiza:
“Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu” (SUV).
Uthibitisho wa kazi ya Mungu katika maisha yetu ni jinsi tunavyowatendea “mmojawapo wa hao walio wadogo” – wale wenye uhitaji (Mathayo 25:44-45). Tutatumia muda wetu, nguvu, na pesa kufungua nyumba zetu kwa watu, kutembelea wale wanaoumia, kukaa na wale wanaosumbuka, na kuwatia moyo wale walio wagonjwa.
Burudani
Kama ilivyo katika maeneo mengine ya maisha yetu, Waadventista hutafuta kuakisi utukufu wa Mungu kupitia burudani tunazoshiriki (1 Wakorintho 10:31).
Ushauri wa Paulo anatuongoza katika kuchagua shughuli, burudani, na zaidi:
“Hatimaye, ndugu zangu, mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo” (Wafilipi 4:8, SUV).
Kifungu hiki kinatuhimiza tuwe makini na tunachoruhusu kuingia akilini mwetu kupitia milango yetu ya fahamu.
Badala ya kukuza tabia za ushindani, kulinganisha, na kudhalilisha wengine ili kujiinua, shauku yetu ni kushiriki katika shughuli za kujengana na kuinuana (Wafilipi 2:3–4).
Muonekano
Waadventista wanatambua kwamba uzuri na thamani ya kweli haitokani na mapambo— iwe ni mavazi na vito vya thamani au magari ya ghali. Badala yake, inatoka kwenye moyo uliojengwa katika Mungu (1 Petro 3:3–4).
Kwa sababu hii, lengo letu ni kuishi maisha yanayoonyesha unyenyekevu na upole wa Kristo badala ya kuonekana kwa namna isiyohitajika (1 Timotheo 2:9).
Urahisi wa mtindo wa maisha na muonekano unatenga Wakristo. Unatuweka katika tofauti kubwa na tamaa, ubinafsi, na ubunifu wa…jamii. Jamii ambapo thamani zinazingatia vitu vya kimwili badala ya watu.1
Hii haimaanishi kwamba tunaachana na muonekano kabisa—sivyo! Badala yake, tunataka muonekano wetu uakisi usafi, kupendeza, na uhalisia wa maisha ya Kikristo.
Afya
Neno la Mungu linatukumbusha kwamba “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe” (1 Wakorintho 6:19, SUV). Hii inamaanisha miili yetu ni zawadi kutoka kwa Mungu kwa uumbaji na ukombozi.
Kama mawakili wema wa kile Mungu alichotupatia, tunajitahidi kutunza afya yetu vizuri kadiri tuwezavyo.
Na wakati huohuo, Waadventista wanafahamu kwamba “Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu” (Warumi 14:17, SUV).
Hivyo sisi pia jaribu kuwa makini isiwe tunafanya sanamu ya chakula tunachokula au tunachokunywa—au kwa kuishi kiafya kwa ujumla. Badala yake, kuishi maisha yenye afya ni namna nyingine ambayo tunaweza kumtukuza Mungu.
Upendo ni msingi wa kanuni zote za mtindo wa maisha na tabia ya Kikristo

Photo by Larm Rmah on Unsplash
Ikiwa tungepunguza kanuni zote za maisha za Kibiblia kuwa moja, ingekuwa upendo.
1 Wakorintho 13 inazungumzia vipawa na mafanikio mbalimbali ya kiroho. Kwa hitimisho, inasema:
“Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo” (1 Wakorintho 13:13, SUV).
Kwa hiyo, kanuni za mtindo wa maisha ya Kikristo ni muhimu, lakini hazina maana ikiwa kwanza kabisa hazitoki katika upendo wa ndani kwa Mungu, ambao kisha unajitokeza katika jinsi tunavyowatendea wengine.
Katika muktadha wa kusaidia watu wenye mahitaji, Yohana aliandika:
“Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?” (1 Yohana 3:17, SUV).
Ndiyo maana Waadventista wanasisitiza mtindo wa maisha unaovuka maisha yetu binafsi na kuleta tofauti kwa wale wanaotuzunguka. Tunatamani kufanya ulimwengu kuwa mahali bora, ndiyo maana tunatafuta njia za kusaidia wahitaji, wanaoumia, na wanaoteseka.
Inaweza kuwa jambo kubwa kama kujenga hospitali na vituo vya matibabu na kuendesha makazi ya watoto yatima. Au inaweza kuwa jambo dogo lakini lenye umuhimu sawa na kuwa na uso unao tabasamu na mkono wa msaada katika kuandaa supu au kumfikia jirani aliye peke yake.
Yote inarejea kwenye upendo wetu kwa Mungu.
Bila shaka, upendo ni ushahidi muhimu zaidi wa mtindo wa Kikristo – kuwapenda wengine kwa ajili ya kuwapenda kwa sababu wao ni watu ambao Kristo alikufa kwa ajili yao.
Unajiuliza jinsi upendo huo unavyoweza kuathiri mahusiano yako na wengine?
Chagua Masomo ya Biblia Mtandaoni
Unataka kuendelea kujifunza? Pata habari zaidi kuhusu Yesu, mwanadamu, mpango wa wokovu, na jinsi Mungu anavyokupenda kiasi cha kutosha kujitolea kila kitu, ili tu kukupatia nafasi ya kumchagua.
Wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kujua pa kuanzia, ndio maana tunatoa chaguo za masomo ya Biblia mtandaoni bure, rahisi kutumia, unaweza kufanya wakati wowote, mahali popote, na kwa kasi yako mwenyewe.
Shule hii ya Biblia mtandaoni itakuelekeza kupitia mada kuu za Maandiko, ikivunja dhana ngumu za Biblia katika vipande vidogo, ambavyo vinaweza kukusaidia kupata majibu ya maswali magumu zaidi ya maisha.
- Seventh-Day Adventists Believe (General Conference of Seventh-day Adventists, 2005), pp. 320–321. [↵]
Kurasa zinazohusiana
Majibu Zaidi
Kile Waadventista Wasabato Wanaamini Kuhusu Yesu kama Mwana wa Mungu
Waadventista Wasabato wanaamini kwamba Yesu ni Mungu kamili kama mmoja wa wanachama wa Utatu pamoja na Mungu Baba na Roho Mtakatifu.
Wanavyoamini Waadventista Wa Sabato Kuhusu Huduma ya Yesu Katika Patakatifu pa Mbinguni
Waadventista Wasabato wanaamini, kulingana na kitabu cha Waebrania, kwamba Yesu yuko katika patakatifu pa mbinguni—au hekaluni—sasa hivi.
Waadventista wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Pambano Kuu (Wema na Uovu)?
Pambano Kuu” ni msemo ambao Waadventista wa Sabato kawaida huutumia kuelezea mgogoro wa kiroho wa ulimwengu kati ya nguvu za mema (Mungu) na nguvu za uovu au dhambi (Shetani/iblis).
Waadventista Wa Sabato wanaamini nini kuhusu Ubatizo?
Kama Wakristo wengi wa Kiprotestanti ulimwenguni kote na katika historia, Kanisa la Waadventista wa Sabato linaamini katika ubatizo, sherehe ambapo watu huzamishwa ndani ya maji kudhihirisha hadharani “kufa kwa maisha ya zamani” na “kuanza kwa maisha mapya katika Kristo”.
Waadventista Wasabato wanaamini nini kuhusu Biblia?
Biblia ndiyo msingi wa kila kanuni na mafundisho ya Waadventista wa Sabato.
Waadventista Wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Mamlaka ya Biblia?
Jifunze jinsi kitabu kimoja cha zamani sana (Biblia) kilivyo msingi pekee wa imani zote za Waadventista wa Sabato.
Je, Waadventista Wasabato Wanaamini Wao Pekee Ndiyo Watakao Kwenda Mbinguni?
Hapana, Waadventista hakika hawaamini kwamba wao ndio pekee watakao kwenda mbinguni. Kwa kweli, hatuamini kwamba kupokelewa mbinguni kunategemea kanisa au madhehebu tunayohusiana nayo.
Je, Waadventista Wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Uumbaji Katika Biblia?
Waadventista Wa Sabato wanaamini kwamba Mungu ndiye Muumbaji wa ulimwengu. Wanafikia hitimisho hili kutoka kitabu cha kwanza cha Biblia—Mwanzo.
Namna Waadventista Walivyojifunza Fundisho la Patakatifu na Maana Yake
Wakati Waadventista wanapozungumzia “fundisho la Patakatifu,” wanarejelea dhana kwamba hekalu la mbinguni linafunua mpango wa wokovu












