Ingawa madhehebu mengi ya Kiprotestanti huadhimisha “Siku ya Bwana” Jumapili, au siku ya kwanza ya juma, Waadventista wa Sabato huadhimisha Jumamosi—Sabato ya siku ya saba ya kibiblia ambayo Mungu aliianzisha alipostarehe baada ya kuumba dunia kwa siku sita zilizotangulia (Mwanzo 2:2-3).
Waadventista hushika na kuadhimisha Sabato ya siku ya saba kuanzia Ijumaa jioni (jua linapotua) hadi Jumamosi jioni. Hii ni ili kumtambua Mungu kama Muumba wao, kukuza uhusiano wao naye, na kupumzika kutoka kwenye shughuli za maisha ya kila siku. Mara nyingi hukutana kwa ajili ya ibada ya Sabato asubuhi ya Jumamosi.
Ili kuelewa jinsi yote haya yalivyoanza, hebu tutazame jinsi Mungu alivyotenga siku ya saba kama siku maalum ya kuungana naye na kutafakari juu ya uumbaji wake.
- Kwa nini siku ya saba (Jumamosi) ni maalum kwa Mungu
- Kwa nini Jumamosi ni maalum kwa Waadventista
- Kama kushika Sabato ni ushikaji mkali wa sheriau
- Kama siku unayoabudu ina umuhimu kweli
Tutaanza kwa kuangalia katika kitabu cha kwanza cha Biblia.
Kwa nini Jumamosi ni maalum kwa Mungu?

Photo by Alabaster Co on Unsplash
Jumamosi ni maalum kwa Mungu kwa sababu ni siku ya saba ya juma—siku ambayo Aliitakasa na kuitenga katika Bustani ya Edeni kama ukumbusho.
Biblia katika Agano la Kale inatuambia kwamba:
“Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya” (Mwanzo 2:3, SUV).
“Siku ya saba” inamaanisha Jumamosi, kulingana na kalenda za Kiebrania na za Kikristo za jadi. Mungu aliitakasa siku hii, maana yake aliifanya kuwa maalum na kuitenga kama siku takatifu ambapo watu wanatoka kwenye kufanya kazi, kujitahidi, na kuumba hadi kupumzika, kufurahia, kuthamini, na kutafakari—kama vile Alivyofanya katika Sabato ya kwanza kabisa.
Sabato inakusudiwa kuwa ishara kati yetu na Mungu, onyesho la mara kwa mara la shukrani na ibada yetu (Ezekieli 20:20). Waadventista wanaamini kwamba kushika Sabato pia ni kutambua kazi ya uumbaji ya Mungu alipoumba dunia kabla ya kupumzika siku ya saba.
Zaidi ya hayo, ukweli kwamba Mungu alianzisha Sabato ya siku ya saba wakati wa Uumbaji unatufundisha kwamba kusherehekea Sabato siku ya Jumamosi sio kwa ajili ya Israeli ya kale au imani ya Kiyahudi pekee. Ni kwa ajili ya wanadamu wote.
Kuna dhana inayozunguka kwamba Sabato ya siku ya saba iliondolewa kwa kuanzishwa kwa Agano Jipya. Lakini ukweli ni kwamba, amri ya Mungu ya kushika Sabato haikuwa sehemu ya sheria ya Musa au mapokeo ya Kiyahudi bali ni sehemu ya sheria isiyotikisika ya Mungu—Amri Kumi. Na ilikusudiwa kuwa kwa ajili ya furaha na utajiri wetu! Sio kama mzigo ambao Mafarisayo waliigeuza kuwa, kama tunavyosoma katika simulizi za Injili ya Agano Jipya.
Na tukumbuke kwamba Amri Kumi sio orodha ya sheria za kiholela. Zinatusaidia kuishi maisha yenye kuridhisha kwa kutuonyesha maana ya kumpenda Mungu (nne za kwanza) na kuwapenda wengine (sita za mwisho).
Amri ya nne kuhusu kuabudu siku ya Jumamosi siyo tofauti na amri nyingine.
Ni sheria inayofafanua jinsi tunavyoweza kuonyesha upendo na ibada yetu kwa Mungu—kwa kuweka kando siku ambayo Yeye aliitangaza kuwa takatifu.

Photo by Brett Jordan
Mungu alikusudia Jumamosi iwe wakati wa sisi kuweka kando kazi zetu za kawaida na kupumzika kutokana na kazi zetu (Kutoka 20:8-10). Inahusisha mabadiliko—kusimama kidogo. Kwa kusitisha kazi zetu, tunapewa nafasi ya kupumzika kutoka kwenye hisia kwamba tunapaswa kuzalisaha au kufanikisha jambo kila dakika. Kusimama huku kunatupa nafasi ya kuwa makini zaidi, kutafakari, na kujichunguza.
Fikiria hivi. Tuseme umeenda kumtembelea mtu unayemjali. Je, ungejisikia kweli umeungana naye ikiwa muda wote ulipokuwa pale, aliendelea tu na kazi zake na kushughulikia orodha zake za mambo ya kufanya? Ikiwa mawazo yake yalibaki kwenye “vitu” vyote vinavyojaza siku zake? Ikiwa hakutenga muda wa kukaa tu na wewe, kukuzingatia, na kuzungumza nawe?
Na sote tumewahi kuwa na wale marafiki ambao daima wanaonekana kuwa na mawazo mengine wakati unapojaribu kuzungumza nao. Labda wanataka kuwa karibu nawe, lakini muda wote wamevurugika na hawapo kikamilifu. Huonekani kuwa wa muhimu, au kwamba uwepo na umakini wako vinathaminiwa.
Zaidi ya hayo, tuwe wa kweli. Sisi binadamu mara nyingi tunapata ugumu kusimama, kupumzika, au kuweka kando orodha na wasiwasi wetu. Wakati mwingine hata tunajisikia na hatia tukifanya hivyo. Kwa hali hiyo, Sabato inaweza kuonekana kama ruhusa ya Mungu ya kujiondoa, kuacha kusumbuka kuhusu majukumu ya kila wiki, na kuchukua muda kutambua na kufurahia baraka Zake.
Angalia kile aya ifuatayo inachosema kuhusu hili:
“Mtafanya kazi siku sita; lakini siku ya saba ni Sabato ya kustarehe kabisa, kusanyiko takatifu; msifanye kazi ya namna yo yote; ni Sabato kwa BWANA katika makao yenu yote” (Mambo ya Walawi 23:3, SUV).
Neno ‘kazi’ au ‘kufanya kazi’ katika muktadha huu linarejelea shughuli zetu za kila siku, biashara tunazofanya ili kujipatia riziki na kusaidia familia zetu. Ni mambo ya lazima tunayopaswa kufanya kila siku ya wiki ambayo hutumia nguvu na mawazo yetu. Haimaanishi kwamba tunajiepusha na jambo lolote linalohitaji nguvu za mwili au akili. Hilo sio lengo kuu.
Njia moja ya kuangalia hili ni kwamba tunaweka pembeni “biashara” siku ya Sabato.
Hili pia limeelezwa katika Isaya 58:13-14, ikielezea mambo ambayo ni faida kuyaweka pembeni siku ya Sabato. Inataja kutokuzifanya “njia zako” au “kuyatafuta yakupendezayo” (SUV).
Hiyo ndiyo sehemu kubwa ya maana ya “pumziko la pekee.” Sio tu kulala au kupumzika. Ni kujitenga na vishawishi na misongo ya dunia. Ni kuungana na pumziko la kina ambalo Mungu alishiriki baada ya kuumba dunia. Hivi ndivyo tunavyogeuka kutoka kutengeneza hadi kufurahia.
Aina hii ya mapumziko pia inatoa fursa bora ya kukusanyika pamoja na familia, au wale tunaowajali, na kama jamii ya waumini. Kufurahia kila mmoja kama viumbe wenzetu wa Mungu Muumba wetu. Hii ndiyo maana ya kutajwa kwa “kusanyiko takatifu,” au kukusanyika pamoja kwa kusudi la kiungu.
Yote haya yanajumuishwa katika motisha kuu ya Waadventista wa Sabato kuabudu pamoja siku ya Jumamosi na kuitunza kama Sabato: upendo kwa Mungu na upendo kwa kila mmoja.
Kwa nini Jumamosi ni maalum kwa Waadventista?

Photo by George Dolgikh
Jumamosi ni maalum kwa Waadventista wa Sabato kwa sababu iliumbwa na Mungu kwa faida yetu na hutuimarisha mara kwa mara katika uhusiano wetu naye. Inatukumbusha nafasi yake kama Muumba wetu, na tunatumia fursa hiyo ya kila wiki kumtazama Yeye na yale aliyotutendea huku tukipumzika kutokana na misongo ya maisha ya kila siku.
Tunaweza kuona hisia hii katika maneno ya Ellen G. White, mwanzilishi mwenza wa Waadventista Wasabato:
“Kwa sababu Alikuwa amepumzika siku ya Sabato, ‘Mungu akaibariki siku ya saba, akaitakasa,’—akaichagua kwa matumizi matakatifu. Aliitoa… kama siku ya pumziko. Ilikuwa ukumbusho wa kazi ya uumbaji, na hivyo ishara ya nguvu za Mungu na upendo Wake.”1
Waadventista hushika Sabato kuanzia jioni ya Ijumaa hadi jioni ya Jumamosi kwa sababu, kama inavyosema katika simulizi la Biblia kuhusu siku za uumbaji, Mungu huhesabu siku kamili kuwa ni kuanzia jioni hadi jioni (Mwanzo 1:31; Mwanzo 2:2). Hii inamaanisha kwamba Sabato huanza jua linapozama Ijumaa na kuisha jua linapozama Jumamosi.
Waadventista kwa kawaida huhudhuria ibada za kanisani na masomo ya Biblia (shule ya Sabato) kila Jumamosi. Lakini pia tunaamini katika kumwabudu Mungu kila siku ya wiki, kuanzia Jumapili hadi Jumamosi. Mungu anatuita tuishi maisha ya ibada, tukimletea utukufu katika mambo yote tunayofanya.1
Ibada hii ya kila siku inaweza kuchukua namna mbalimbali, kama vile ibada binafsi asubuhi, ibada ya jioni na familia, au hata kuchukua muda mfupi wakati wa siku kwa ajili ya kuungana tena na Mungu kupitia sala.
Taasisi nyingi za Waadventista wa Sabato kama vile shule za sekondari, vyuo vikuu, biashara, ofisi za mikutano, na vituo vya habari hufanya ibada na wafanyakazi wenzao kabla ya siku ya kazi kuanza.
Kuna makusanyiko ya Waadventista wanaokutana pamoja katika vikundi vidogo kwa ajili ya maombi Jumapili, Jumatano, Ijumaa, au kila siku. Baadhi ya washiriki wa kanisa hukutana majumbani mwao kwa ibada au kujifunza Biblia katikati ya wiki.
Kuna njia nyingi zisizo na idadi ambazo kwazo tunaweza kumwabudu Mungu. Maisha yetu wenyewe yanaweza kumletea utukufu tunapoongozwa na Roho Mtakatifu.
Lakini tunaamini ibada ya Sabato inapaswa kuwa ya kipekee. Mungu alituambia tuitakase, na hivyo tunatunza Sabato kwa kujiepusha na kazi na kuelekeza mawazo yetu katika kukuza uhusiano wetu na Yeye.
Kujiepusha na kazi mara kwa mara ni kama kusema hatufanywi watakatifu kwa matendo yetu wenyewe, bali kwa kumtegemea Mungu.
Yeye ndiye chakula chetu—“Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu” (Matendo 17:28, SUV). Na pia ni kupitia Kwake ndipo tunapopata pumziko la kweli.
Waanzilishi wa Kanisa la Waadventista wa Sabato walijifunza ukweli kuhusu kutunza Jumamosi kama siku ya kweli ya ibada katika miaka ya 1840 kutoka kwa Wabaptisti wa Sabato. Walitusaidia kuelewa kwamba kuitenga siku hii ya kila wiki kwa ajili ya Mungu ni jambo ambalo bado Anataka tuweze kulifurahia.
Na utafiti wa pamoja na wa kudumu wa Maandiko wa Waadventista wa mwanzo ulithibitisha ukweli huo. Sabato ya siku ya saba ilitunzwa na Yesu Kristo Mwenyewe (Luka 4:16) na na waumini Wake katika Neno la Mungu lote, ikiwa ni pamoja na Kanisa la Kikristo la awali (Marko 15:42-47; Matendo 13:14-17; 16:13; 17:2; 18:4).
Je, kushika Sabato ni ushikaji mkali wa sheria?
Je, kushika mojawapo ya Amri Kumi kunachukuliwa kuwa ushikaji mkali wa sheria? Au chochote kilichoandikwa katika Maandiko kama maagizo kutoka kwa Mungu?
Ni pale tu amri hizo au maagizo hayo yanaposhikwa ili kwa namna fulani “kupata” kibali kwa Mungu, au kufikia kiwango cha juu cha kustahili au utakatifu.
Kutunza Sabato ya siku ya saba ni sehemu ya sheria ya Mungu, Amri Kumi. Tunatunza Sabato iliyoelezwa katika amri ya nne kama vile tunavyoshika zile tisa nyingine.
Kushika amri za Mungu hakupaswi kuwa kuhusu “matendo” au “ushikaji uliopitiliza wa sheria.” Waadventista hawaamini kwamba sheria yoyote ya Mungu inaweza au inapaswa kushikwa kwa lengo la kupata wokovu kwa jitihada za kibinadamu.
Kama tunavyoshika amri nyingine kwa upendo kwa Mungu na kwa kutambua hekima na mwongozo Wake, ndivyo ilivyo pia kwa Sabato. Sio kuhusu kupata kibali bali ni kuhusu kukumbuka Yeye ni nani. Ni kuhusu kujisalimisha kwa Yesu Kristo, Mwokozi wetu, na kupumzika katika neema Yake.
Mungu anataka tushike Sabato kwa sababu tunampenda na tunaamini kwamba sheria Zake zimekusudiwa tu kutuboresha na kutubariki. Mwishowe, Alituumba tukiwa na uhuru wa kuchagua ili tusishike amri Zake kwa lazima, kwa hofu, au ili “tuonekane” watakatifu.
Na bado, wengi wamekosea kuelewa Sabato ni nini hasa. Wengine hata wamepotosha maana yake kama njia ya kudhibiti jamii zao na kujifanya watakatifu kuliko wengine:
Wakati wa Yesu, Mafarisayo waliweka sheria kali kuhusu jinsi Wayahudi wenzao wanavyopaswa kushika Sabato. Hii ilisababisha watu wengi kuona Sabato kama siku ya ibada kali ya kidini badala ya tukio takatifu na la furaha la kumlenga Mungu.
Hata walimshutumu Yesu Mwenyewe kwa kuvunja Sabato (Yohana 5)! Hilo pekee linaonyesha jinsi sheria za Mafarisayo zilivyokuwa kinyume kabisa na kile ambacho Mungu anatuomba.
Yesu alieleza kwamba Mungu hakukusudia Sabato ishikwe kwa ukali wa kisheria kama wa Mafarisayo. Aliwaambia kwamba Sabato haikukusudiwa kuwa mzigo bali baraka, akisema kwamba Sabato iliumbwa kwa ajili ya mwanadamu, sio mwanadamu kwa ajili ya Sabato (Marko 2:27).
Tunaposhika Sabato kama Mungu alivyoamuru, tunajifungulia baraka Zake na kutafuta kuzishiriki na wengine. Sabato ni fursa nzuri ya kushirikiana na waumini wenzetu kanisani na kutafuta njia za kuwahudumia wengine katika jamii yetu.
Tunaweza kufikiria amri za Mungu kwa namna inayofanana na jinsi wazazi kwa kawaida hulenga kuweka sheria kwa watoto wao kwa upendo. Lengo lao ni kuwafanya watoto wao kuwa na afya na furaha kadri inavyowezekana, wakitumaini kuwasaidia kuepuka mitego au vishawishi vya maisha. Sio kwa sababu ya kutaka mamlaka au nguvu. Na, wazazi kwa kawaida wanatumaini kwamba watoto wao watafuata sheria hizo kwa upendo na heshima, sio kwa hofu au kama njia ya kupata “alama za ziada.”
Mungu ni kama mzazi wetu mwenye nguvu zote, mwenye upendo wote, na mkamilifu. Muumba wetu. Sisi sote ni watu wa Mungu. Naye anajua kwamba pumziko la kweli la Sabato linaweza kutunufaisha kwa namna nyingi.
Kupumzika hutusaidia kupata nafuu baada ya siku sita za kazi. Inatupa fursa ya kuhuisha nguvu zetu, kupumzisha akili zetu, na kuweka kando shinikizo na msongo wa mawazo unaotokana na maisha yetu yenye shughuli nyingi.
Bwana anawaita wote waliochoka na kulemewa waje kwake wapate pumziko (Mathayo 11:28).
Katika Waebrania 4:10 tunasoma:
“Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake” (SUV).
Pumziko la Sabato linatukumbusha kwamba ndani ya Yesu tunapata pumziko—tumeokolewa kwa haki Yake na sio kwa matendo yetu. Na kwa kuwa tumeokolewa kwa haki Yake pekee, Yeye huwapa watu Wake neema na nguvu za kushika amri Zake kwa jinsi anavyoagiza.
Je, ina maana yoyote ni siku gani ya juma ni Sabato?

Photo by Blessing Ri on Unsplash
Ndiyo, siku ya Sabato iliwekwa rasmi na Mungu, tangu mwanzo katika kitabu cha Mwanzo, kuwa ni Jumamosi, siku ya saba ya juma.
Kushika Sabato katika siku nyingine tofauti na Jumamosi ni kinyume na kile ambacho Biblia inasema kuhusu jambo hili. Kushika siku ya saba ni kuheshimu utakaso wa Mungu wa Jumamosi wakati wa Uumbaji, na amri Yake ya kuitakasa siku hiyo.
Fikiria kuhusu mume na mke wanaosherehekea kumbukumbu ya ndoa yao kila mwaka. Kila siku ya mwaka, wanaonyeshana upendo wao lakini wanatambua kwamba kumbukumbu ya ndoa yao ni siku maalum. Wanasherehekea siku hiyo kama ishara ya upendo na kujitolea kwao kwa kila mmoja.
Sasa fikiria mmoja wao angeamua kubadilisha tarehe ya kumbukumbu ya ndoa. Badala ya kusherehekea, tuseme, Septemba 17, anataka kubadilisha tarehe ya kumbukumbu kuwa Septemba 18. Licha ya upendeleo au sababu ya mabadiliko hayo, hata hivyo, kumbukumbu yao ya ndoa itabaki kuwa Septemba 17 kwa sababu hiyo ndiyo tarehe waliyooana.
Baada ya Uumbaji, katika siku ya saba, Biblia inatuambia kwamba:
“Na siku ya saba Mungu alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe siku ya saba, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoifanya. Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya” (Mwanzo 2:2-3, SUV).
Tunaweza kuona wazi kabisa hapo. Mungu aliitenga Jumamosi kama Sabato Yake maalum. Aliitakasa, akituomba tuiheshimu na kutumia muda pamoja Naye ili tufurahie baraka zinazokuja na pumziko la Sabato.
Sabato husaidia kuandaa akili zetu kwa ibada
Kwa Waadventista, Sabato ya siku ya saba kweli ni siku ya ibada.
Lakini ni zaidi ya kuhudhuria ibada kanisani tu.
Ni njia ya kuandaa akili zetu kwa ajili ya ibada. Katika dunia yenye shughuli na harakati zisizoisha, siku hii ya pumziko ni kimbilio kutoka kwenye pilkapilka za maisha na hutusaidia kuingia katika hali ya ibada. Kwa njia hii, tunaweza kuelekeza mawazo yetu kwenye mambo ya kweli yanayojalisha maishani—uhusiano wetu na Yesu Kristo na mahusiano tuliyo nayo na wengine.
Je, ungependa kujifunza zaidi kuhusu jinsi siku hii maalum ilivyo?
Chagua Masomo ya Biblia Mtandaoni
Unataka kuendelea kujifunza? Pata habari zaidi kuhusu Yesu, mwanadamu, mpango wa wokovu, na jinsi Mungu anavyokupenda kiasi cha kutosha kujitolea kila kitu, ili tu kukupatia nafasi ya kumchagua.
Wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kujua pa kuanzia, ndio maana tunatoa chaguo za masomo ya Biblia mtandaoni bure, rahisi kutumia, unaweza kufanya wakati wowote, mahali popote, na kwa kasi yako mwenyewe.
Shule hii ya Biblia mtandaoni itakuelekeza kupitia mada kuu za Maandiko, ikivunja dhana ngumu za Biblia katika vipande vidogo, ambavyo vinaweza kukusaidia kupata majibu ya maswali magumu zaidi ya maisha.
Kurasa Zinazohusiana
- White, Ellen G., The Desire of Ages, p. 281. [↵]
Majibu Zaidi
Kila Kitu Unachohitaji Kujua Kuhusu Chakula cha Siku ya Sabato
Kwa Waadventista Wa Sabato, kushiriki chakula cha Siku ya Sabato pamoja na marafiki na familia ni moja ya sehemu muhimu na ya kumbukumbu ya Sabato.
Je! Tunaweza Kuitunza Siku Yoyote ya Wiki Kama Sabato?
Katika sura za kwanza kabisa za Biblia, tunamwona Mungu akianzisha kumbukumbu ya kila wiki na siku ya mapumziko, inayoitwa Sabato (Mwanzo 2:2-3).
Pumziko na Kuunganishwa Tena: Maana Halisi ya Kutunza Sabato
Biblia inatuambia kwamba tunatunza Sabato kwa kuepuka kazi. Mungu alitoa sheria hii kwa sababu alijua itatuimarisha na kutuletea furaha, pamoja na kutupa muda wa kuungana naye na kujipatia nguvu kutokana na maisha yetu yenye shughuli nyingi.
Nani Aliyebadilisha Sabato kwenda Jumapili?
Nani Aliyebadilisha Sabato kwenda Jumapili?Ikiwa Biblia haijawahi kutaja mabadiliko ya Sabato, kwa nini leo wengi wanaenda kanisani Jumapili? Nani alibadilisha siku hiyo? Lakini hilo sio swali sahihi la kuuliza. Sabato haijabadilika. Kilichobadilika ni uamuzi wa...
Kila kitu unachohitaji kujua kuhusu Shule ya Sabato
Kila kitu unachohitaji kujua kuhusu Shule ya SabatoShule ya Sabato ndio sehemu ya kujifunza Biblia ya programu za kanisa katika makanisa mengi ya Waadventista wa Sabato. Ni wakati wa kujifunza Biblia kuhusu mada au somo fulani. Badala ya kumsikiliza mhubiri, watu...
Ninawezaje Kuanza Kutunza Sabato?
Sabato, inayokuja kila siku ya saba ya juma, ni siku maalum inayoheshimu amri ya nne na uumbaji wa Mungu.









