Kama Wakristo wengi wa Kiprotestanti, Waadventista wa Sabato wanaamini katika tendo linalojulikana kama Meza ya Bwana au Ushirika Mtakatifu. Wanakunywa divai ya zabibu na kula mkate usiotiwa chachu wakitii maagizo ya moja kwa moja ya Yesu kufanya hivyo kwa ukumbusho Wake (1 Wakorintho 11:24–25).
Chapisho hili litakuongoza kupitia maelezo ya tendo hili na kwa nini ni muhimu sana kwa Waadventista. Utajifunza:
- Historia ya Meza ya Bwana
- Inahusisha nini
- Inawakilisha nini
- Kwa nini Waadventista huoshana miguu kabla ya Meza ya Bwana
- Nini cha kutarajia katika ibada ya Ushirika ya Kiadventista
- Nani anaweza kushiriki katika ibada hizi
Hebu tuanze kwa kuangalia tamko rasmi la Kanisa la Waadventista wa Sabato kuhusu imani hii:
Katika uzoefu huu wa ushirika, Kristo yupo ili kukutana na kuwatia nguvu watu Wake.
Tunaposhiriki, tunatangaza kwa furaha kifo cha Bwana hadi atakapokuja tena.
Maandalizi ya Meza yanajumuisha kujichunguza, kutubu, na kukiri.
Bwana alianzisha huduma ya kuoshana miguu ili kuashiria utakaso upya, kuonyesha utayari wa kuhudumiana kwa unyenyekevu wa Kristo, na kuunganisha mioyo yetu katika upendo.
Ibada ya ushirika iko wazi kwa Wakristo wote waaminio.”
Sasa, tutaangalia mizizi ya tendo hili.
Je, historia ya Meza ya Bwana ni ipi?

Photo by Tim Wildsmith on Unsplash
Waadventista wanatambua agizo la Meza ya Bwana likianzia siku za mwisho za maisha ya Yesu. Meza hii inatajwa katika sehemu mbili za Biblia: Injili na maandiko ya Paulo katika Agano Jipya (1 Wakorintho 11:23–25).
Meza ya Bwana, pia inayoitwa Mlo wa Mwisho wa Jioni, ina asili yake katika Pasaka ya Agano la Kale—sherehe ya Kiyahudi ya ukombozi wa Waisraeli kutoka Misri.
Waisraeli walikuwa watumwa wa Wamisri, lakini Mungu alikuwa akifanya miujiza ili kuwaokoa. Kwa sababu ya ukaidi wa Farao kuwaachilia Waisraeli, Mungu alileta mapigo juu ya Wamisri.
Usiku kabla ya kutoka Misri, Mungu aliwaagiza Waisraeli washiriki katika ibada ambayo baadaye ikajulikana kama Pasaka. Kupitia Musa, aliwaagiza Waisraeli wamchinje mwana-kondoo na kupaka damu yake kwenye miimo ya milango yao.
Sababu ni ipi?
Kwa pigo la kumi juu ya Wamisri, malaika mharibu angepita katika nchi na kuua mzaliwa wa kwanza wa kila nyumba. Lakini malaika huyo alipoona damu kwenye miimo ya mlango, angepita juu ya nyumba hiyo hakuwaua wazaliwa wao wa kwanza. Hata Wamisri walikuwa na nafasi ya kufanya hivyo na kuokolewa na adhabu (Kutoka 12:21–28).
Asubuhi ilipofika, wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli waliokolewa, wakati katika nchi yote, familia za Wamisri ziliomboleza vifo vya watoto wao wa kwanza na mifugo (Kutoka 12:29–30).
Wayahudi bado wanaadhimisha sikukuu hii kama ukumbusho wa kutoka kwao utumwani Misri. Na Wakristo wanaiona kama ishara au mfano wa kifo cha Yesu kwa ajili yetu, akituokoa na mauti ya milele (1 Wakorintho 5:7).
Wakati Yesu alisherehekea Pasaka na wanafunzi Wake kwa mara ya mwisho (ndiyo maana tunaiita Mlo wa Mwisho wa Jioni), Aliweka kile tunachokijua kama Meza ya Bwana:
“Hata saa ilipofika aliketi chakulani, yeye na wale mitume pamoja naye. Akawaambia, Nimetamani sana kuila pasaka hii pamoja nanyi kabla ya kuteswa kwangu; kwa maana nawaambia ya kwamba siili tena hata itakapotimizwa katika ufalme wa Mungu” (Luka 22:14–16, SUV).
Hebu tuchunguze kinachotokea wakati wa ibada hii leo.
Meza ya Bwana inahusisha nini?

Image by Usman Yousaf from Pixabay
Wakati wa Meza ya Bwana, waumini hushiriki kula mkate usiotiwa chachu na kunywa divai ya zabibu pamoja.
Biblia inatuambia kwamba “Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu” (Mathayo 26:26, SUV).
Kisha baada ya mkate, “Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi” (Mathayo 26:27–28, SUV).
Kama ilivyo katika sherehe ya Pasaka, mkate ni usiotiwa chachu, maana yake hauna chachu (hamira) (Kutoka 12:18–20; Marko 14:1).
Kuhusu kinywaji kinacho ambatana na mkate, “zao la mzabibu” linamaanisha zabibu.
Wakati makundi mengi ya imani hutumia divai halisi kwa ajili ya ushirika, Waadventista hutambua madhara ya kutumia vinywaji vya kilevi (Mithali 20:1; Warumi 14:21; Waefeso 5:18) na hutumia divai ya zabibu isiyochachwa (isiyo na kilevi).
Kama agizo la mwisho, Yesu aliwaagiza wanafunzi Wake “fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (Luka 22:19, SUV).
Ni kwa utii wa moja kwa moja kwa agizo hili ndipo Waadventista wanashiriki Meza ya Bwana kama ukumbusho wa Yesu na dhabihu Yake kwa ajili yetu.
Lakini Yesu aliposema kwamba mkate ni mwili Wake na kinywaji ni damu Yake, huenda unajiuliza maana yake halisi ni nini…
Je, mkate na divai ni mwili na damu halisi ya Kristo?
Hapana, mkate na kinywaji sio mwili na damu halisi ya Kristo. Ni ishara kwa ajili ya ukumbusho.
Waadventista hawaamini kwamba mkate na divai ni kitu kingine zaidi ya mkate na kinywaji cha zabibu, kama vile hawamini kwamba kuzamishwa majini wakati wa ubatizo kunamtakasa mtu dhambini kwa njia ya kimiujiza.
Badala yake, mkate na divai katika ibada ya Meza ya Bwana ni ishara ya dhabihu ya Kristo.
Hata hivyo, chakula hiki cha jioni ni zaidi ya mlo wa ukumbusho tu.
Ni onyesho la wazi la kujisalimisha kwetu kwa Kristo na shauku yetu ya kuendelea kumtumikia. Tunakiri wokovu na ahadi ya uzima wa milele vinavyokuja kwa sababu ya mwili Wake uliovunjika na damu Yake iliyomwagika.
Tutaangazia zaidi alama hizi hivi punde.
Meza ya Bwana inamaanisha nini?

Photo by DNK.PHOTO on Unsplash
Meza ya Bwana inatukumbusha Pasaka, kifo cha Yesu msalabani kama dhabihu, agano jipya, na kurudi kwa Yesu mara ya pili.
Kama tulivyoona, Meza ya Bwana ilifanyika wakati wa Pasaka ambapo mwana-kondoo alitolewa dhabihu kama unabii wa Mwokozi ajaye.
Kristo alitimiza unabii huo kwa kifo chake na akaanzisha Meza ya Bwana badala yake.
Hivyo, Pasaka ilikuwa ishara ya agano la kale—uhusiano maalum wa Mungu na Israeli wa kale (Kutoka 34:27; 1 Mambo ya Nyakati 16:15; Zaburi 132:12).
Kwa upande mwingine, Meza ya Bwana ni ishara ya agano jipya, ambalo ni uhusiano maalum wa Mungu na watu wake wote (Waebrania 8:13; 12:24).
Pia inatuonyesha tumaini la kuungana tena na Yesu atakaporudi.
Wakati wa Meza ya Bwana, Yesu aliwaambia wanafunzi wake:
“Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu” (Mathayo 26:29, SUV).
Kwa hiyo kila mara tunaposhiriki Meza ya Bwana, tunatazamia wakati ambapo tutashiriki pamoja na Yesu Mwenyewe mbinguni.
Na kila kipengele cha ibada hii kina maana ya mfano pia. Hebu tuangalie kwa kifupi.
Mkate usiotiwa chachu
Mkate usio na chachu unaashiria mwili wa Yesu (Mathayo 26:26).
Chachu inawakilisha dhambi (Luka 12:1; 1 Wakorintho 5:8), hivyo mkate usio na chachu unatukumbusha maisha yasiyo na dhambi ambayo Yesu aliishi.
Yesu alijitambulisha na mkate aliposema, “Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe” (Yohana 6:35, SUV).
Divai ya zabibu
Divai ya zabibu inawakilisha damu ya Yesu iliyomwagika kwa ajili ya ukombozi wetu (Mathayo 26:27–28; Waebrania 9:22).
Biblia inatuambia kwamba tunaokolewa tu kupitia Yesu na dhabihu Yake kwa ajili yetu msalabani, ambako alitoa damu na kufa kwa niaba yetu (Mambo ya Walawi 17:11; 1 Yohana 1:7).
Kwa kumwamini Yeye na kukubali zawadi Yake, tunakuwa na uhakika wa wokovu, na hiki ndicho Kristo alichomaanisha wakati wa Karamu ya Mwisho.
Divai pia inaonyesha jinsi Yesu pekee anavyoweza kutosheleza mahitaji yetu ya ndani kabisa.
Akasema,
“Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe” (Yohana 7:37, SUV).
Na kwa yule mwanamke kisimani, Akasema,
“Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele” (Yohana 4:13–14, SUV).
Vipengele vya Meza ya Bwana ni alama za utoshelevu wa kiroho unaopatikana katika Kristo. Kama vile chakula na maji yalivyo muhimu kwa maisha hapa duniani, kumkubali Yesu ni muhimu kwa uzima wa milele (Yohana 17:3).
“Kula mwili Wake” na “kunywa damu Yake”
Wakati wa Karamu ya Mwisho, Yesu alisema kwamba mkate ulikuwa mwili Wake na kinywaji kilikuwa damu Yake.
Hii inafanana na Yohana 6:48–58, ambako alisema kwamba mkate ni mwili Wake anaoutoa kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu. Na ili tupate uzima wa milele, lazima tukae ndani Yake kwa kula mwili Wake na kunywa damu Yake.
Alimaanisha nini katika haya yote?
Hakuwa akizungumza kuhusu kula mwili Wake na kunywa damu Yake kihalisi; alikuwa akitumia mfano kuelezea maana ya kuwa na uhusiano wa karibu Naye kwa imani (Yohana 6:63).
Wakristo wanaishi maisha haya mapya katika Yesu Kristo kwa kujisalimisha maisha yetu kwa Mungu, kumtii, kudai ahadi Zake, kuomba, kujifunza Biblia, na kuishi kulingana na yale tunayojifunza.
Moja ya misingi yetu ya imani inasema:
“Kula mwili wa Kristo na kunywa damu Yake ni lugha ya mfano kwa ajili ya kujikita katika Neno la Mungu, ambamo waumini wanadumisha ushirika na mbinguni na kuwezeshwa kuwa na uzima wa kiroho… Waumini wanakula kutoka kwa Kristo, mkate wa uzima, kwa kushiriki Neno la uzima—Biblia. Pamoja na Neno hilo huja nguvu ya uzima ya Kristo.”1
Hii inaeleza umuhimu wa Meza ya Bwana. Ni maelezo ya kile kinachomaanisha kumpokea Yesu kama Bwana na Mwokozi wetu, yote yakiwa yamejengwa juu ya kifo Chake kwa ajili yetu.
Lakini huenda umesikia kwamba Waadventista pia hujumuisha kile kinachoitwa “kuoshana miguu” katika ibada ya Meza ya Bwana.
Hii ndiyo sababu.
Kwa nini Waadventista huoshana miguu wakati wa Meza ya Bwana?

Photo by Samuel Lima
Ingawa desturi hii haijaenea sana miongoni mwa Wakristo leo, Waadventista wanaamini kwamba kuoshana miguu (Yohana 13) kunapaswa kuwa sehemu ya ibada ya Meza ya Bwana.
Inapofahamika vizuri, inatupa ujumbe wenye nguvu wa maana ya kuwa wafuasi wa Yesu.
Biblia inatuambia kwamba Yesu aliwaosha miguu wanafunzi Wake kabla tu hawajala. Alifanya hivyo kuonyesha unyenyekevu na huduma:
“Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga” (Yohana 13:5, SUV).
Lakini Petro alishtuka kwamba Yesu, ambaye alimwamini kuwa Bwana wake na Masihi aliyekuwa ameahidiwa, angeweza kujishusha na kuosha miguu yake (Yohana 13:6–9).
Hata hivyo, Yesu alisisitiza. Kisha akahitimisha matendo Yake kwa maneno yafuatayo:
“ …. Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea? Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi” (Yohana 13:12–15, SUV).
Katika maneno haya ya Yesu, Waadventista wanapata agizo lao la kibiblia kushiriki katika tendo la unyenyekevu la kuoshana miguu.
Wakati wa Yesu, watu walitembea kila mahali na walivaa viatu vya wazi, hivyo mwisho wa siku miguu yao ilikuwa michafu sana. Hata hivyo Yesu aliiosha.
Mfano Wake unatufundisha jinsi ya kujinyenyekeza katika kuhudumia wengine. Ikiwa Yesu Kristo, Masihi, aliweza kuosha miguu ya watu wa kawaida, basi hakuna mtu aliye juu kiasi cha kushindwa kuosha miguu ya jirani yake.
Ni tendo hili la kwanza la unyenyekevu kamili ndilo linaloandaa moyo kushiriki katika ibada ya Meza ya Bwana.
Je, umuhimu wa kiroho wa kuosha miguu ni upi?
Kuosha miguu ni onyesho jingine la utayari wa Kristo kujitoa kikamilifu kwa ajili yetu—kama vile Alivyo “…. jifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu” (Wafilipi 2:7, SUV).
Ibada hii pia ni ishara ya kutakaswa moyo kutoka kwenye dhambi na unajisi.
Kwa kawaida, watu wanaoshiriki Meza ya Bwana na ibada ya kuosha miguu tayari wamebatizwa. Ibada hizi za ukumbusho hazikusudiwi kuchukua nafasi ya ubatizo bali ni desturi takatifu kwa waumini.
Lakini kama vile miguu iliyosafishwa inavyoweza kuchafuka tena haraka, Wakristo wanahitaji kusafishwa kila siku kutoka kwa “dhambi ile ituzingayo kwa upesi” (Waebrania 12:1, SUV).
Roho Mtakatifu anapotushawishi kuhusu dhambi zetu, tunamjia Yesu kwa toba, naye hutusafisha na kutusamehe.
Hatimaye, kuosha miguu hutukumbusha kwamba ndani ya Kristo, hakuna tofauti kati ya tajiri na maskini, mwenye nguvu na dhaifu, maarufu na asiyejulikana.
Mbele ya msalaba, sote ni sawa—wenye dhambi wanaohitaji neema ya Mungu.
Utarajie nini katika ibada ya Meza ya Bwana ya Kiadventista
Makanisa mengi ya Waadventista hufanya Meza ya Bwana mwishoni mwa kila robo mwaka—hiyo ni mara nne kwa mwaka. Lakini hii sio amri. Makanisa au makundi tofauti yanaweza kufanya mara nyingi zaidi au chache zaidi, kanisani au katika hafla mbalimbali.
Kwa kawaida hufanyika wakati wa ibada ya kawaida ya asubuhi ya Sabato.
Unapoingia kanisani, unaweza kuona meza mbele, iliyofunikwa kwa kitambaa cheupe. Chini yake kuna vyombo maalum vya Meza ya Bwana vilivyo na mkate na divai ya zabibu.
Ibada itaendelea kama kawaida—kuanzia shule ya Sabato hadi ibada kuu na hubiri. Katika makanisa mengine, mahubiri yanaweza kuwa mafupi kidogo ili kutoa muda zaidi kwa ajili ya Meza ya Bwana.
Baada ya mahubiri, mzee wa kanisa kwa kawaida hutoa maelezo mafupi, anaomba, na kutoa maelekezo. Kisha waumini wanatawanyika kwa ajili ya ibada ya kutawadha miguu.
Huduma ya kutawadha miguu
Wakati wa huduma ya kutawadha miguu, wanaume na wanawake hukutana katika maeneo tofauti ndani ya kanisa kwa ajili ya heshima na ustaarabu. Wakati mwingine, chumba cha ziada hutolewa kwa ajili ya wanandoa na familia kuwa pamoja.
Kuoshana miguu kunaweza kufanyika katika ukumbi wa ushirika, vyumba mbalimbali vya shule ya Sabato, au hata nje, kutegemeana na kanisa na hali ya hewa.
Katika maeneo mbalimbali, mashemasi (kwa wanaume) na mashemasi wanawake (kwa wanawake) wataongoza. Watatoa mabeseni yenye maji na taulo.
Watu kwa kawaida wanapangana wawili wawili ili kuoshana miguu. Wanaweza kuomba pamoja na kisha kubadilishana kuoshana miguu.
Kutegemea na kanisa, kundi linaweza kukaa na kuimba pamoja wakati wakisubiri wengine wamalize na kisha kurudi kwenye ibada kuu.
Ibada ya Meza ya Bwana
Kurudi katika ukumbi mkuu wa kanisa, mchungaji au mzee ataongoza Ibada ya Meza ya Bwana, akisaidiwa na wazee wengine, mashemasi wa kiume, na mashemasi wa kike.
Mchungaji au mzee atasoma andiko kuhusu jinsi Yesu alivyoumega mkate na kuwapa wanafunzi Wake. Kisha baada ya sala, mchungaji atawapa mashemasi sinia zilizo na mkate, ambao watausambaza kwa waumini kutoka benchi hadi benchi.
Baada ya kila mtu kupokea kipande cha mkate, mchungaji atawaomba waumini watumie huku wakiomba.
Mchakato huo huo unarudiwa kwa vikombe vidogo vya divai ya zabibu.
Mwisho wa ibada, makanisa mengine yatakuwa na kipindi kifupi cha ushuhuda na fursa ya kutoa sadaka ya shukrani (inayoitwa mara nyingi “sadaka ya Msamaria Mwema”).

Photo by Pavel Danilyuk
Kisha, kama vile Yesu na wanafunzi walivyoimba wimbo baada ya Karamu ya Mwisho, waumini wataimba pamoja kabla ya sala ya mwisho na kuagana (Mathayo 26:30).
Nani anaweza kushiriki Meza ya Bwana katika Kanisa la Waadventista?
Waadventista wanafanya kile kinachoitwa “Meza ya Bwana iliyo wazi.” Yeyote aliyempokea Kristo anaweza kushiriki Meza ya Bwana.
Hivyo basi, hatuhitaji mtu awe mshiriki wa kanisa ili kushiriki. Lakini tunawahimiza wote wanaokuja wawe na moyo wa unyenyekevu na toba.
Watu hupokea baraka kuu zaidi wanapokuja kwa imani, wakimtegemea Yesu na sifa Zake, Yeye aliyeutoa mwili Wake na kumwaga damu Yake kwa ajili yetu. Kupitia Meza ya Bwana, tunashiriki naye.
Ungependa kujifunza zaidi kuhusu kile Yesu alichofanya kwa ajili ya wanadamu?
Chagua Masomo ya Biblia Mtandaoni
Unataka kuendelea kujifunza? Pata habari zaidi kuhusu Yesu, mwanadamu, mpango wa wokovu, na jinsi Mungu anavyokupenda kiasi cha kutosha kujitolea kila kitu, ili tu kukupatia nafasi ya kumchagua.
Wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kujua pa kuanzia, ndio maana tunatoa chaguo za masomo ya Biblia mtandaoni bure, rahisi kutumia, unaweza kufanya wakati wowote, mahali popote, na kwa kasi yako mwenyewe.
Shule hii ya Biblia mtandaoni itakuelekeza kupitia mada kuu za Maandiko, ikivunja dhana ngumu za Biblia katika vipande vidogo, ambavyo vinaweza kukusaidia kupata majibu ya maswali magumu zaidi ya maisha.
- Seventh-day Adventists Believe (General Conference of Seventh-day Adventists, 2005), p. 231. [↵]
Kurasa zinazohusiana
Majibu Zaidi
Kile Waadventista wa Sabato Wanaamini Kuhusu Uwakili (na Maana Yake)
Kile Waadventista wa Sabato Wanaamini Kuhusu Uwakili (na Maana Yake)Upendo kwa Mungu na kwa wanadamu wenzetu ndiyo kanuni kuu ya imani ya Waadventista wa Sabato. Na tunaonyesha upendo huo kwa njia kuu kupitia jinsi tunavyosimamia mambo—ya kimwili na yasiyo ya...
Waadventista Wanaamini Nini Kuhusu Maisha, Kifo, na Ufufuo wa Yesu?
Yesu Kristo, mtu aliyeishi Palestina ya karne ya kwanza, ndiye msingi wa imani ya Waadventista.
Wanavyoamini Waadventista wa Sabato Kuhusu Tabia ya Kikristo
Wanavyoamini Waadventista wa Sabato Kuhusu Tabia ya KikristoMifano ya matendo na maneno yanayounda tabia ni muhimu katika aina yoyote ya mfumo wa imani kwa sababu yanatokana na imani hizo. Waadventista wa Sabato wanatazama Biblia, pamoja na Yesu kama mfano kamili, kwa...
Kile Waadventista Wasabato Wanaamini Kuhusu Yesu kama Mwana wa Mungu
Waadventista Wasabato wanaamini kwamba Yesu ni Mungu kamili kama mmoja wa wanachama wa Utatu pamoja na Mungu Baba na Roho Mtakatifu.
Wanavyoamini Waadventista Wa Sabato Kuhusu Huduma ya Yesu Katika Patakatifu pa Mbinguni
Waadventista Wasabato wanaamini, kulingana na kitabu cha Waebrania, kwamba Yesu yuko katika patakatifu pa mbinguni—au hekaluni—sasa hivi.
Waadventista wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Pambano Kuu (Wema na Uovu)?
Pambano Kuu” ni msemo ambao Waadventista wa Sabato kawaida huutumia kuelezea mgogoro wa kiroho wa ulimwengu kati ya nguvu za mema (Mungu) na nguvu za uovu au dhambi (Shetani/iblis).
Waadventista Wa Sabato wanaamini nini kuhusu Ubatizo?
Kama Wakristo wengi wa Kiprotestanti ulimwenguni kote na katika historia, Kanisa la Waadventista wa Sabato linaamini katika ubatizo, sherehe ambapo watu huzamishwa ndani ya maji kudhihirisha hadharani “kufa kwa maisha ya zamani” na “kuanza kwa maisha mapya katika Kristo”.
Waadventista Wasabato wanaamini nini kuhusu Biblia?
Biblia ndiyo msingi wa kila kanuni na mafundisho ya Waadventista wa Sabato.
Waadventista Wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Mamlaka ya Biblia?
Jifunze jinsi kitabu kimoja cha zamani sana (Biblia) kilivyo msingi pekee wa imani zote za Waadventista wa Sabato.
Je, Waadventista Wasabato Wanaamini Wao Pekee Ndiyo Watakao Kwenda Mbinguni?
Hapana, Waadventista hakika hawaamini kwamba wao ndio pekee watakao kwenda mbinguni. Kwa kweli, hatuamini kwamba kupokelewa mbinguni kunategemea kanisa au madhehebu tunayohusiana nayo.
Je, Waadventista Wa Sabato Wanaamini Nini Kuhusu Uumbaji Katika Biblia?
Waadventista Wa Sabato wanaamini kwamba Mungu ndiye Muumbaji wa ulimwengu. Wanafikia hitimisho hili kutoka kitabu cha kwanza cha Biblia—Mwanzo.
Namna Waadventista Walivyojifunza Fundisho la Patakatifu na Maana Yake
Wakati Waadventista wanapozungumzia “fundisho la Patakatifu,” wanarejelea dhana kwamba hekalu la mbinguni linafunua mpango wa wokovu















