Mungu Anataka Nitumie Vipi Pesa Zangu?

Mungu anajali jinsi tunavyotumia pesa zetu.

Anajali sana kiasi kwamba aliweka kanuni za kifedha katika Neno lake ili kutuonyesha jinsi ya kutumia pesa zetu kwa namna inayomheshimu na kuleta faida kubwa kutokana na pesa tunazopewa.

Hebu tuangalie ushauri wa kifedha ambao Biblia inatoa kwa kuchunguza:

Anza kwa kuelewa jinsi pesa zilivyotumika katika Biblia.

Aya za Biblia kuhusu matumizi sahihi ya pesa:

  • Mheshimu Mungu: Kumbukumbu la Torati 8:18; Mithali 3:9.
  • Toa zaka: Malaki 3:10; Walawi 27:32.
  • Toa sadaka: 2 Wakorintho 9:7; Matendo 20:35.
  • Tuna wanaohitaji: Mathayo 6:3-4; Matendo 4:34-35.
  • Tunza familia yako: Mithali 13:22; 1 Timotheo 5:8.
  • Lipa madeni yako: Warumi 13:7-8; Zaburi 37:21
  • Weka akiba na uwekeze: Luka 14:28-30; Mithali 6: 6-8; Mathayo 25:14-27.

Je, pesa zilitumika kwa namna tofauti wakati wa Biblia?

a Black man wearing glasses and sitting at a table, with his hand on his chin studying an open Bible, in deep thought

Photo by Oladimeji Ajegbile

Pesa katika nyakati za Biblia ilitumiwa kwa njia ile ile kama ilivyo leo.

Watu walitumia pesa kununua walichohitaji na kusaidia familia zao (Mwanzo 42:1-3; Maombolezo 5:4). Pia ilikuwa hutumiwa kulipa wafanyakazi, kodi, kununua starehe na raha, na kuwasaidia wenye mahitaji.1

Watu wakati huo walilazimika kufanya maamuzi ya kifedha pia. Walilazimika kufikiria wangetumia pesa wapi, jinsi wangeweza kuweka akiba na kuwekeza, na jinsi ambavyo wangeweza kutoa mahitaji ya familia zao na kuepuka kupata madeni.

Hata hivyo, kuna tofauti kadhaa kati ya muktadha wa kifedha wa Biblia na leo.

Watu katika nyakati za Biblia:

  • Mara nyingi hawakutumia sarafu: Bidhaa na huduma mara nyingi ziliuzwa na kubadilishana badala ya kununuliwa (Yakobo 4:13-15).
  • Waliishi katika jamii ya kilimo: Kwa sababu watu wengi wakati huo walikuwa wakulima na wachungaji, mazao na mifugo vilikuwa mali muhimu na mara nyingi vilikuwa vinatumika kama njia ya malipo (Walawi 27:30-32; Mwanzo 13:2).
  • Walilenga zaidi katika kuishi kuliko starehe:2 Kabla ya enzi ya viwanda, kazi ilikuwa inachukua muda mwingi na ilihitaji nguvu nyingi. Ukosefu wa uzalishaji kwa wingi ulifanya bidhaa ziwe ghali zaidi. Watu pia walikuwa wakifanya kazi kwa bidii hivyo walikuwa na muda na pesa kidogo kwa starehe na burudani.
  • Walikuwa na motisha zaidi ya kuepuka deni: Ingawa watu wangeweza kukusanya deni, haikuwa inahimizwa kama vile mifumo ya alama za mikopo ya leo. Kulikuwa na adhabu kali zaidi kwa deni wakati huo, na wadeni walikuwa wanapelekwa gerezani au kuwa watumwa hadi walipolipa deni wanalodaiwa (Mathayo 18:23-25; Mithali 22:7).3

Ingawa hizi ni tofauti muhimu kati ya wakati wao na wetu, pesa ilikuwa—na bado ni—sehemu muhimu ya jamii.

Na kujipatia ni hatua ya kwanza tu. Mara tu tunapopata tunapaswa kuamua tutaitumiaje.

Basi tunawezaje kutumia pesa zetu vizuri?

Tunapaswa kuwekaje akiba na kuwekeza? Tunawezaje kutoa mahitaji ya familia zetu na wale wenye uhitaji? Na tunawezaje kushughulikia deni?

Tuone ushauri gani Biblia inatoa kuhusu maswali haya.

Biblia inatushaurije kuhusu kufanya maamuzi ya kifedha?

Biblia inatushauri kufanya maamuzi ya kifedha kwa uangalifu, tukijitahidi kadri tuwezavyo kutumia vyema pesa ambazo Mungu ametupatia.

Haijatoa maagizo maalum, bali badala yake, inatupa kanuni za kudumu ambazo mtu yeyote anaweza kutumia katika maisha yake.

Mungu aliweka kanuni hizi kwa sababu anajali jinsi tunavyotumia pesa zetu.

Hii sio kwa sababu Mungu ana wasiwasi na fedha zetu, bali zaidi kwa sababu Yeye anajali hali ya mioyo yetu, na jinsi tunavyotumia pesa zetu inaweza kutupa ufahamu ikiwa tunajitahidi au ni wenye ubinafsi.

Pesa ni chombo, na inaweza kutumika kwa mema au maovu. Tunapotumia kwa mema kwa:

  • kushughulikia mahitaji yetu
  • kushughulikia mahitaji ya wengine
  • kusaidia mashirika yanayofaa, biashara, na huduma, n.k.

Kisha tunawajibika vyema kwa pesa ambazo Mungu ametupatia.

Tunapotumia vibaya pesa tulizopewa tunaweza kukosa fursa ya kuleta tofauti katika maisha ya mtu mwingine.

Ndio maana Neno la Mungu hutufundisha kuwa waangalifu katika matumizi ya pesa na kutuonyesha jinsi tunavyopaswa kuweka kipaumbele katika majukumu fulani ya kifedha.

Na ni nani bora zaidi wa kutufundisha jinsi tunavyoweza kusimamia pesa zetu kuliko Mungu?

Kwanza, Yeye ndiye anayetupatia pesa (Zaburi 24:1; Warumi 11:36). Yeye ndiye anayetupa rasilimali, vipaji, na muda tunahitaji kupata pesa na kujipatia riziki.

Kwa kweli, Biblia inatusaidia kuelewa kwamba pesa sio tu inatoka kwa Baba wa Mbinguni. Ni mali Yake. Kila tunachopata kinatoka kwake na ni kwetu kutumia na kutunza.

Hebu tuone mwongozo gani Maandiko yake yanatoa kuhusu:

  • Zaka
  • Sadaka
  • Kutoa kwa ajili yetu na wengine
  • Deni
  • Kuweka akiba na kuwekeza

Tafadhali kumbuka: Mwongozo katika makala haya hakukusudiwa kuchukua nafasi ya ushauri wa kifedha wa kitaalamu. Ingawa taarifa hii inaweza kuwa na manufaa, tunapendekeza kutafuta wataalamu wa fedha kwa maelekezo zaidi.

Zaka

a small wooden box with a cross on the front and an open slit on the top, sitting on a wooden desk

Photo by Leiada Krözjhen on Unsplash

Biblia inatuita kutoa 10% ya mapato yetu kwa Mungu.

Katika Agano la Kale, tafsiri ya Kiebrania ya asili inaita hii “sehemu ya kumi,” ambayo baadaye ilihuishwa kuwa neno la Kiingereza, “zaka.4

Zamani za Biblia, Waisraeli walitoa zaka kwa kutoa 10% ya mazao yao kusaidia makuhani na Walawi, watu ambao Mungu aliwachagua kuwahudumia Waisraeli na kuwaleta karibu naye (Mambo ya Walawi 27:32; Kumbukumbu la Torati 14:28-29).

Zaka hii ilitolewa kutoka kwa matunda ya kwanza ya mazao yao, kanuni iliyowaongoza kutoa zaka yao kwanza kwa Mungu kabla ya kufanya chochote kingine na mapato yao (Mithali 3:9).

Katika Kanisa la Waadventista, tunafuata kanuni ya sehemu ya kumi ya kwanza kwa kuweka kando 10% ya mapato yetu ya jumla kama zaka mara tu tunapopokea mshahara wetu. Kiasi hiki huchangwa kwa Kanisa ili kuwasaidia viongozi wa Kanisa, sawa na watumishi wa Mungu wa siku hizi.

Unaweza kugundua kuna tofauti kati ya jinsi watu wanavyotoa zaka leo na jinsi watu wa Mungu walivyokuwa wakitoa zaka zamani. Lakini hii haimaanishi kwamba zaka ilikuwa kwa Wayahudi pekee. Sio hata kidogo!

Neno la Mungu linatuambia kuwa zaka ilishikiliwa muda mrefu kabla ya watu wa Israeli. Ibrahimu alifanya hivyo (Waebrania 7:4). Vivyo hivyo Yakobo alifanya (Mwanzo 28:20-22).

Hata ilionekana katika Agano Jipya, Yesu na Paulo wakiwaita Wakristo kutoa zaka (1 Wakorintho 9:13–14; Mathayo 23:23) (Yesu hata anasema watu wake wanapaswa kuzingatia kukuza tabia kama ya Kristo kwanza, lakini wasisahau kutoa zaka pia).

Lakini kuna nini kikubwa kuhusu zaka, hata hivyo?

Vizuri, yote inarudi kwa wazo kwamba Mungu anamiliki pesa zetu. Tunapotoa sehemu ya kumi, tunarudisha tu 10% ya pesa ambazo Mungu alitupa mwanzoni. Hiyo ni kama vile mtu akikupa dola 100 na kuomba urejeshe dola 10 tu. Isingekuwa vigumu kwako kumrudishia dola 10 mtu ambaye tayari amekupa vingi, sivyo?

Lakini kwa nini hata kuwa na ubadilishanaji huu? Kwa nini Mungu asi tupe dola 90 na kubaki na dola 10 kwa ajili Yake mwenyewe?

Linakuja kwa wazo kwamba kutoa hutubadilisha.

Tunapotoa kwa imani tunakua kiroho. Tunanza kutegemea pesa kidogo na zaidi kwa Mungu. Tunapotoa, tunatambua pesa zetu zinatoka kwa nani na tunaweza kumtegemea nani kweli.

Biblia inasema:

“Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la “ (Malaki 3:10, SUV).

Aya hii inatuhakikishia kwamba kutoa zaka haisababishi tupungukiwe–kama tunavyoweza kudhani. Badala yake, roho yetu ya kutoa inafungua mioyo yetu kupokea baraka tele kutoka kwa Mungu.

Kutoa sehemu zaka pia hutupa nafasi ya kuhusika katika kazi ya Mungu na kuonyesha shauku yetu ya kumweka Mungu wa kwanza katika maisha yetu.

Katika Kanisa la Waadventista Wa Sabato, pesa hizi kwa kawaida hutumika kusaidia wachungaji, wafanyakazi wa utawala wa mkutano, miradi ya uinjilisti, na huduma za washiriki.

Lakini zaka sio njia pekee unayoweza kusaidia kazi ya Mungu.

Unaweza pia kuisaidia kwa kutoa sadaka.

Sadaka

Kama zaka, sadaka ni michango inayotolewa kwa Kanisa. Hata hivyo, tofauti na zaka, hakuna kiasi maalum ambacho watu wanaitwa kutoa. Na hakuna wakati maalum ambapo inapaswa kutolewa.

Katika Biblia, watu walikusanya sadaka kwa ajili ya kumheshimu Mungu, kusaidia wengine, na kusaidia huduma ya Mungu.5

Walitakiwa kutoa kwa hiari kama walivyokuwa wakiitwa na Roho Mtakatifu.

Vivyo hivyo, tunaweza kutoa chochote na wakati wowote tunapojisikia kuhamasishwa kutoa. Tunaweza kutoa sadaka kwa Kanisa na kwa huduma na mashirika yasiyo ya faida yanayosaidia watu wenye mahitaji.

Michango, kama zaka, ni njia nyingine tunayoonyesha Mungu kwamba tunamwamini kututunza na kutumia pesa tunazokuwa nazo—hata kama hatuna pesa nyingi.

Katika Biblia, Yesu Kristo alisifu sadaka ya uaminifu ya mjane:

“Akainua macho yake akawaona matajiri wakitia sadaka zao katika sanduku la hazina. Akamwona mjane mmoja maskini akitia mle senti mbili. Akasema, Hakika nawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; maana, hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo” (Luka 21:1-4, SUV).

Hii sio kusema kwamba Mungu daima anatarajia tutoe pesa zetu zote tunapotoa sadaka. Anatarajia tutumie kiasi fulani kwa ajili yetu sisi wenyewe na familia zetu ambao wanatutegemea.

Kisa cha mjane kiko hapo kutukumbusha kwamba hatupaswi kamwe kuogopa kutoa ikiwa tunahisi tunaitwa—hata kama ni kwa hasara yetu. Ingawa hii haimaanishi kwamba Mungu atatubariki na utajiri kama thawabu kwa kutoa kwetu, tunaahidiwa kwamba Mungu atatutunza (Wafilipi 4:19).

Pia tunafurahia baraka ya kujua kwamba tumesababisha mabadiliko chanya katika maisha ya mtu mwingine… na ndani yetu wenyewe.

Katika Kanisa la Waadventista wa Sabato, wale wanaotoa sadaka wanaweza kutuma michango yao kwa huduma yoyote watakayo. Kwa namna hii, sadaka kwa kawaida husaidia katika matumizi ya kanisa la mahali na miradi ya kuwafikia wengine.

Kama zaka, kutoa sadaka hutusaidia kukua kiroho kwa kutufundisha kuwa na imani kwa Mungu na kutuelekeza katika upendo na huduma kwa wengine.

Na kama vile Roho Mtakatifu alivyowahamasisha Kanisa la awali kutoa sadaka, vivyo hivyo tunaweza kuomba, tukiomba Roho Mtakatifu atuongoze katika kutoa kwetu.

Tunaweza kujifunza kuwa watoaji wenye furaha katika kutoa sadaka kwa kufuata amri kuu—upendo kwa Mungu na upendo kwa jirani yetu (Marko 12:28-34; 2 Wakorintho 9:7).

Kujitunza sisi wenyewe na wapendwa wetu

A person counts bills and organizes them on a tabletop. Stacks of receipts, a calculator, and a checkbook are also present.

Photo By: Kaboompics.com from Pexels

Matumizi mengine mazuri sana ya pesa zetu ni kuzitumia kujisaidia sisi wenyewe na wapendwa wetu.

Na hilo labda ndilo jambo la kwanza linalokuja akilini tunapopokea mshahara wetu, sivyo?

Tunaanza kufikiria jinsi tunavyoweza kutumia hiyo kulipa umeme, mahitaji ya nyumbani, na nguo mpya za shule kwa watoto wetu.

Ni jukumu ambalo Biblia inatuita tulitimize baada ya kutoa sehemu ya kumi—na ni moja muhimu sana (1 Timotheo 5:8; Kumbukumbu la Torati 26:2).

Baada ya yote, tunawezaje kuwa sehemu ya kazi ya Mungu ya kupenda na kuwafikia wengine tunaposhindwa hata kujitunza wenyewe au watu wanaotutegemea?

Mtume Paulo alisisitiza umuhimu wa kufanya kazi ili kupata mshahara wa haki na kujitegemea, kama yeye na wengi wa Wakristo wa mwanzo walivyofanya wakati wa huduma yao:

“Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu; wala hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote. Si kwamba hatuna amri, lakini makusudi tufanye nafsi zetu kuwa kielelezo kwenu, mtufuate” (2 Wathesalonike 3:7-9, SUV).

Kwa njia hii, Paulo anatuita tufanye tunachoweza kuendesha maisha yetu.

Wakristo hawaitwi kuchukua kutoka kwa wengine. Wanapaswa kuwa chanzo cha kutoa, kama vile Yesu alivyokuwa (Matendo 20:35).

Bila shaka, kunaweza kuwa na mazingira ambayo yanafanya iwe vigumu au isiwezekane kwa watu kujitegemea. Katika hali kama hizi, kuomba msaada kutoka kwa wengine sio jambo la kuaibisha. Kanisa la Mungu linapaswa kuwa mahali ambapo watu wanaweza kwenda ili kupata msaada.

Kwa watu wengi, kazi yetu huanza kwa kuwajali watu wanaotutegemea nyumbani kwetu, kama vile kuwatunza watoto wetu na kuwajali wazazi wetu wanaozeeka (Methali 13:22).

Lakini pia tunatumia pesa zetu kununua mahitaji muhimu na kulipa madeni yetu (Mathayo 6:31-33).

Deni

Eneo lingine ambapo Biblia inatuita kutumia pesa zetu ni kuzitumia kulipa madeni.

Baada ya kulipa zaka zetu na kutoa mahitaji ya familia zetu, ni wazo zuri kuweka kipaumbele kulipa madeni.

Sote tuna uzoefu wa madeni katika ulimwengu wetu wa kadi za mkopo, mikopo ya wanafunzi, na mikopo ya nyumba, lakini mara nyingi watu wanajikuta wamezidiwa.

Wanakusanya madeni ambayo hawawezi kumudu kulipa. Au wanakwenda bila kulipa madeni yao kwa muda mrefu hivyo inakusanya mlima wa riba.

Ndiyo maana ni muhimu kulipa madeni yetu kabla hayajaanza kuwa mengi.

Lakini, zaidi ya hayo, kulipa madeni yetu ni tendo la uaminifu na uwajibikaji (Warumi 13:7; Zaburi 37:21). Pia ina madhumuni yake ya vitendo—yaani, kutusaidia kutoroka utumwa wa deni.

Biblia inasema:

“Tajiri humtawala maskini, Naye akopaye ni mtumwa wake akopeshaye” (Mithali 22:7, SUV).

Ni wazo zuri kuepuka kupata madeni kwanza ikiwezekana (Mhubiri 5:5). Moja ya njia nzuri ya kufanya hivyo ni kufuatilia hali ya kifedha ili unaponunua kitu kwa mkopo, ujue kwamba utaweza kulipa bili yako bila shida.

Unaweza kugundua kwamba ni muhimu hata kununua kitu kwa pesa taslimu au kwa kadi yako ya malipo badala ya kununua kwa mkopo.

Kwa namna yoyote ile, matumizi yenye uwajibikaji ndio kanuni kuu.

Akiba na kuwekeza

a man sitting at a desk with a piggy bank on it, in a darkened room lit by a desk lamp, recording in his ledger.

Photo by Dziana Hasanbekava from Pexels

Tunafanya nini na pesa iliyobaki baada ya zaka, sadaka, kununua mahitaji muhimu, na kulipa madeni yetu?

Tunaweza kufikiria kutumia pesa kwenye vitu tunavyotaka na kufurahia. Na kwa kweli, hakuna ubaya wowote katika hilo. Mungu haweki mipaka watu wake kwenye mahitaji ya msingi; pia anataka tuweze kufurahia mambo madogo (1 Timotheo 6:17).

Tatizo pekee ni kwamba kununua vitu tunavyotaka kunaweza kuwa kipaumbele kisicho sahihi. Matumizi yanapozidi yanaweza kutushawishi hata kuweka vipaumbele kwa vitu tunavyotaka kuliko mahitaji yetu au mahitaji ya wengine.

Hivyo, hata tunaponunua vitu tunavyofurahia, ni muhimu kuwa na kiasi na umakini.

Ili kutumia pesa zetu kwa busara, hatuwezi tu kufikiria kuhusu sasa hivi. Tunapaswa kufikiria kujiandaa kwa ajili ya siku zijazo. Hapa ndipo inakokuja akiba na kuwekeza.

Akiba ni uamuzi wa kuhifadhi pesa zetu hadi tutakapokusanya ya kutosha kutumia kwa jambo muhimu.

Kwa njia hii, kutunza pesa kunaweza kutusaidia kununua vitu vikubwa bila kukopa, kutusaidia kujitunza vizuri sisi wenyewe na wengine wakati ujao. Pia inaweza kutusaidia kujiandaa kwa dharura.

Biblia inasema hivi:

“Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia? Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi, watu wote waonao wakaanza kumdhihaki, wakisema, Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza” (Luka 14:28-30, SUV).

 

“Ewe mvivu, mwendee chungu, Zitafakari njia zake ukapate hekima. Kwa maana yeye hana akida, Wala msimamizi, wala mkuu, Lakini hujiwekea akiba ya chakula wakati wa jua; Hukusanya chakula chake wakati wa mavuno” (Mithali 6: 6-8, SUV).

Kuwekeza, kwa upande mwingine, ni uchaguzi wa kutumia pesa zetu kwenye kitu ambacho kitakuwa na thamani zaidi kwetu baadaye kuliko pesa tulizokuwa nazo awali.

Hii inaweza kufanywa kwa kuwekeza katika ardhi, akiba yetu ya uzeeni, elimu ya watoto wetu, na kadhalika.

Katika mfano mmoja, Yesu anazungumzia kuwekeza pesa alipokuwa anaelezea bwana anayewapa watumishi watatu kiasi tofauti cha pesa kuzilinda kwa ajili yake (Mathayo 25:14-27). Mtumishi wa kwanza na wa pili wanachukua pesa zao na kuziwekeza, wakimletea bwana faida, huku wa mwisho kulenga tu kuziweka akiba. Bwana anapowauliza watumishi kuhusu pesa, anaridhika na wa kwanza na wa pili lakini ana hasira na wa tatu ambaye hakutumia vyema pesa alizopewa.

Kanuni zote tulizozungumzia hadi sasa zinatumika kwetu kama ilivyokuwa kwa watu wa zamani wa Biblia.

Lakini kutakuwa wakati ambapo Mungu atatutaka tutumie pesa yetu kwa namna tofauti?

Tunapaswa kutumia pesa zetu vipi katika nyakati za mwisho?

Ingawa tunaweza kujiandaa kwa dharura nyingine kwa kuweka akiba ya pesa, hakuna kiasi cha pesa kitakachotuandaa kwa wakati wa mwisho.

Njia pekee tunayoweza kuitumia kujiandaa ni kujenga uhusiano na Yesu, ili tunapofika mwisho tuweze kumtegemea Yeye kwa kila hitaji letu (Luka 12:10-21,29-31; 1 Timotheo 6:17-19).

Kwa ujumla, Biblia inaonya dhidi ya kulimbikiza pesa. Ingawa tunaweza kuweka akiba, unaweza kufika wakati ambapo tunazingatia sana kutunza na kuhifadhi pesa zetu hivi kwamba inaweza kwenda bure au tunakuwa na hofu kwamba itachukuliwa kutoka kwetu na kuwa na shauku kubwa ya kuikusanya.

Yesu anasimulia mfano mmoja kuhusu mtu tajiri aliyehifadhi pesa zake zote kwa mipango kwamba siku moja ataitumia (Luka 12:13-21). Lakini mtu huyo anakufa kabla ya kuweza kutumia. Kwa maneno mengine, alikuwa amejikita sana katika kile alichoweza kufanya na pesa baadaye hivyo akakosa fursa ya kile ambacho angekuwa amefanya nayo sasa.

Vivyo hivyo, kutakuja wakati mwishoni mwa nyakati ambapo pesa zetu hazitakuwa na maana kwetu. Hazitakuwa na thamani yoyote na hazitaweza kutununulia tunachohitaji (Yakobo 4:13-15).

Huenda hii ndiyo sababu Biblia inataka tuelewe mapema kwamba pesa, ingawa inatusaidia sasa, sio kitu kitakachotuokoa, wala sio kitu kitakachodumu.

“Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako” (Mathayo 6:19-21, SUV).

Ndiyo maana ni muhimu tuombe kwa ajili ya uwezo wa kutambua ni nini cha kufanya na pesa zetu wakati wa mwisho. Wakati tunafanya hivi, Roho Mtakatifu atatuonyesha lini na jinsi ya kuweka akiba na lini na jinsi ya kutumia pesa zetu kwa kitu cha thamani.

Tunaweza kuitwa kuelekeza pesa zetu kusudi la Mungu, kusaidia kueneza Injili wakati bado tunaweza, kabla ya mwisho kufika na pesa zetu kupoteza thamani yake (Luka 12:29-34).

Hatimaye, kuwafikia wengine na ukweli unaookoa maisha wa Yesu ndio matumizi makubwa zaidi ya pesa zetu, na uwekezaji mkubwa zaidi ambao tunaweza kufanya milele.

Kutumia vyema tulichopewa

Kanuni za kifedha za Biblia zinatuonyesha jinsi tunavyoweza kutumia pesa zetu vizuri. Na, kwa uongozi wa Roho Mtakatifu, tunaweza kujifunza jinsi ya kutumia kanuni hizo katika maamuzi ya kila siku.

Unapoanza, inaweza kuwa na manufaa kwako kuunda bajeti ili uwe makini zaidi kuhusu jinsi pesa yako inavyotumika.

Unaweza pia kuomba kwa ajili ya utambuzi wa Roho Mtakatifu katika kufanya maamuzi ya jinsi ya kutumia pesa yako vizuri.

Mwishowe, hiyo ndio maana ya kuwa wakili mwema.

Jifunze zaidi kuhusu uwakili kwa kusoma,

Kurasa zinazohusiana

  1. Deuteronomy 24:14-15; Matthew 20:1-16; Matthew 17: 24-27; John 12:3; Acts 4:34-35. []
  2. Rafferty, John P., “The Rise of the Machines: Pros and Cons of the Industrial Revolution,” Britannica. []
  3. Nichol, F.D. Seventh-day Adventist Bible Commentary And Bible Students’ Source Book , Seventh-day Adventist Church, 1978. p. 204. []
  4. “4643.” Bible Hub. []
  5. Psalm 96:8; Acts 4:34-35; Exodus 35:21-29.[]

Je, Una swali kuhusu Waadventista? Uliza hapa!

Pata majibu kwa maswali yako kuhusu Waadventista Wasabato

Majibu Zaidi

Biblia Inasemaje Kuhusu Mbingu?

Biblia Inasemaje Kuhusu Mbingu?

Maisha baada ya kifo ni jambo linalowasumbua watu wote. Iwe Mkristo au la, binadamu ana shauku ya asili ya kuelewa kinachofuata.