Ukweli wa sasa, kulingana na Waadventista wa Sabato, ni imani kwamba ukweli fulani wa Biblia ni muhimu kwa watu wa Mungu katika nyakati maalum katika historia. Mungu anamtuma Roho Mtakatifu kufunua ukweli unaosaidia kuelewa vizuri jinsi ya kutafsiri na kutumia Neno lake katika wakati wa sasa.
Na ingawa hii sio dhana ya Waadventista pekee, ina nafasi kubwa katika Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Tunaweza hata kusema ni muhimu kwa DNA yetu. Lakini zaidi kuhusu hilo baadaye.
Unaposoma, unaweza kutarajia kujifunza majibu ya maswali haya:
- Ukweli wa sasa ni nini, na dhana hiyo inatoka wapi?
- Kuna mifano gani kuhusu dhana hii katika Biblia?
- Kwa nini ni muhimu kwa Kanisa la Waadventista Wa Sabato?
Hebu tuanze na swali muhimu la ukurasa huu.
Ukweli wa sasa ni nini, na dhana hii inatoka wapi?

Photo by Ben White on Unsplash
Ukweli wa sasa ni ukweli ambao Mungu huufunua wakati maalum kwa lengo maalum.
Dhana hii kimsingi inakiri kwamba hali hubadilika, na kwa sababu ya mabadiliko haya, baadhi ya ujumbe wa kweli kutoka kwa Neno la Mungu unaweza kuwa na maana zaidi au faida zaidi kwa wakati uliopo.
Randy Roberts, mchungaji na mtaalam wa theolojia wa Kiadventista, anasema hivi:
“Dunia inabadilika na wakati unabadilika, Mungu atamtuma Roho Mtakatifu kwetu kutusaidia kuelewa jinsi tunavyoishi kulingana na kanuni za Biblia. Kwa njia hiyo, Maandiko ni ya milele na huja kwa wakati.”1
Haupitwi na wakati kwa sababu Biblia imejaa kweli zinazotuhusu bila kujali wakati, mahali, na utamaduni. Lakini pia unakuja kwa wakati kwa kuwa unaweza kuongea moja kwa moja na hali za wakati, mahali, na utamaduni fulani.
Hii haimaanishi kwamba kweli za Biblia zilizoleta athari katika muktadha fulani hazitumiki kwetu leo. Badala yake, zinaweza kutumika kwetu kwa namna tofauti.
Ni muhimu kuelewa kwamba Neno la Mungu halibadiliki.
Ukweli wa sasa hausemi kwamba unafanya hivyo. Kwa kweli, Biblia inatuambia kwamba ukweli wa Mungu hudumu” vizazi na vizazi” (Zaburi 100:5, SUV). Biblia ina kanuni zisizobadilika ambazo zinawahusu watu wote.
Wazo la ukweli wa sasa, basi, ni kwamba Mungu anaweza kutupa ufahamu mpya ili kutusaidia kuelewa Neno lake vizuri zaidi na kulitumia katika hali zinazoweza kutokea wakati fulani. Lakini hizi “kweli mpya” daima zinaendana na kweli nyingine katika Biblia.
Kwa njia hii, ukweli wa sasa hutufundisha jinsi ya kuishi ukweli wa Biblia katika hapa na sasa.
Ellen G. White, mwanzilishi wa Kanisa la Waadventista Wa Sabato na mwandishi maarufu, anagusia jambo hili anaposema,
“Ukweli wa sasa, ambao ni jaribio kwa watu wa kizazi hiki, haukuwa jaribio kwa watu wa vizazi vilivyopita.”2
Na mumewe, James White, ambaye pia alikuwa kiongozi katika Kanisa la Waadventista wa Sabato, aliandika:
“Ukweli wa sasa ni ukweli wa sasa, sio ukweli wa baadaye, na… Neno kama taa inayong’aa mahali tuliposimama na si kwa wazi sana kwenye njia inayoelekea mbali.”3
Hatukutunga mafundisho haya. Yanatoka katika Biblia.
Aya inayotupatia neno “ukweli wa sasa” iko katika 2 Petro:
“Kwa hiyo nitakuwa tayari kuwakumbusha hayo siku zote, ijapokuwa mnayajua na kuthibitishwa katika kweli mliyo nayo” (2 Petro 1:12, SUV).
Katika aya hii, Petro, ambaye alikuwa karibu na mwisho wa maisha yake, aliwatia moyo washiriki wa vuguvugu la kanisa la awali kwa kuwa imara katika ukweli wa wakati huo maalum.
Lakini ingawa neno “ukweli wa sasa” linatoka katika aya hii katika Biblia, kuelewa kwetu kuhusu hilo unatokana zaidi na jinsi linavyofunuliwa katika Maandiko.
Basi, twende kwenye Biblia kutafuta mifano.
Ipi ni baadhi ya mifano ya ukweli wa sasa katika Biblia?
Biblia ina mifano mingi ya kweli ambazo Mungu alizitoa kwa watu maalum kwa wakati na mahali maalum. Tutazungumzia:
- Onyo la Nuhu kuhusu gharika
- Ujumbe wa Yona kwa Ninawi
- Maelezo ya Yesu kuhusu sheria
- Ujumbe wa Paulo kwa Wayahudi na Mataifa
Onyo la Nuhu kuhusu gharika

Photo by JOHN TOWNER on Unsplash
Kisa cha Nuhu na gharika ni mfano mzuri wa jinsi Waadventista wanavyoelewa ukweli wa sasa.
Mungu alimwagiza Nuhu ajenge safina kwa sababu gharika kuu ilikuwa inakuja duniani (Mwanzo 6:13). Nuhu alisikiliza ujumbe wa Mungu kwake, akajenga safina, na yeye, familia yake, na safina iliyokuwa imejaa wanyama waliokolewa (Mwanzo 7:22).
Je, huu ni mfano wa ukweli wa sasa?
Kweli, ujumbe wa Mungu kwetu leo ni tofauti na ule aliompa Nuhu.
Ujumbe wa Mungu kwa Nuhu ulikuwa, “Ninakusudia kuleta gharika; jenga safina.” Lakini ujumbe wa Mungu kwetu leo sio, “Ninakusudia kuleta gharika; jenga safina.”
Onyo la gharika lilikuwa ukweli wa wakati huo kwa Nuhu na familia yake. Lakini sio kwetu.
Sasa, kwa sababu onyo la gharika sio ukweli wa sasa kwetu haimaanishi kwamba sio kweli.
Tunaamini kwamba gharika ilitokea na Nuhu na familia yake waliokolewa. Tunaweza pia kuchukua kanuni kutoka kwenye kisa hiki na kuzitumia katika maisha yetu: ishi maisha yaliyo salimishwa kwa Mungu, fuata maagizo yake, na kuwa na imani katika mpango wake.
Tunapata mfano unaofanana na huu juu ya ukweli wa sasa katika kisa cha Yona.
Ujumbe wa Yona kwa Ninawi
Ujumbe wa unabii wa Yona kwa Ninawi ulikuwa kwamba wangeangamizwa baada ya siku 40 kwa sababu ya uovu wao (Yona 3:4). Watu waliposikia ujumbe huo waliungama dhambi zao. Na Mungu akawaepusha kwa sababu ya mabadiliko ya mioyo yao (Yona 3:5–10).
Ukweli wa sasa uliotabiri uharibifu wa watu wa Ninawi uliwafanya wabadilishe njia zao mbaya.
Ellen White ananukuu mfano huu kwa kina anapozungumzia jinsi ukweli wa sasa ulivyo muhimu, kwa watu wa Ninawi na kwetu leo:
“Sasa, fikiria watu fulani wakisema, ‘Tunao ukweli wote ambao mababu zetu walikuwa nao; hatutaki zaidi,’ na Mungu wa mbinguni awape ujumbe kama alivyofanya kwa Ninawi. Ni nini kingetokea? Kitu kile kile ambacho kingetokea kwa Waninawi kama wasingetubu. Hukumu ilikuwa imetangazwa juu yao, lakini toba yao iliwakomboa. Tunapaswa kuwa na shukrani kwamba tunaye Mungu ambaye ataghairi kutokana na mabaya yaliyotishwa, wakati wapotofu wanaporudi kwake kwa kutubu kweli kwa moyo.”4
Ukweli wa sasa unaweza kutuonyesha tulipokosea na kutuchochea kuchukua hatua. Ni fundisho linaloonyesha neema, upendo, na wokovu wa Mungu wetu.
Maelezo ya Yesu kuhusu sheria

Photo by Mick Haupt on Unsplash
Ukweli wa sasa unaweza pia kutupatia ufahamu mpya wa habari za zamani.
Kuna sheria 613 katika Torati—vitabu vitano vya kwanza vya Agano la Kale. Sheria hizi, zilizotolewa kwa wana wa Israeli baada ya kutoka utumwani, zilikuwa na lengo la kuwaongoza katika maeneo mengi ya maisha yao.
Na walihitaji aina hiyo ya ufasaha: walikuwa wachanga katika safari zao za kiroho. Walikuwa watumwa kwa mamia ya miaka, na bila mifano ya moja kwa moja, hawakujua jinsi ya kujiendesha kwa njia itakayomheshimu Mungu na kuwaheshimu wenzao.
Endelea mbele hadi huduma ya Yesu hapa duniani.
Kufikia wakati huu, Waisraeli walikuwa wameweka kipaumbele sheria zao za ibada juu ya uhusiano wao na Mungu. Kwa kuzingatia sheria zote hizi za ibada, walikuwa wamesahau lengo lao, na kwa upande mwingine, walivunja amri ya kwanza kati ya Amri Kumi: “Usiwe na miungu mingine ila mimi” (Kutoka 20:3, SUV). Walikuwa wamefanya tamaduni na ibada zao kuwa sanamu.
Basi Yesu, Mwana wa Mungu, alikuja kufafanua sheria ambazo walikuwa wakizitunza kwa bidii.
Aliwaambia viongozi Kiyahudi:
“Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii” (Mathayo 22:37–40, SUV).
Yesu aliwapa ukweli wa sasa ili kuwasaidia kuelewa roho, au kiini, ya sheria walizokuwa wakizishika. Muhtasari wake wa sheria—upendo kwa Mungu na upendo kwa wengine—ulikuwa na lengo la kuwasaidia Waisraeli kubadilisha mtazamo—kuelewa kwa njia mpya—maana ya kumwabudu na kumtumikia Mungu.
Kwa maneno mengine, Yesu aliwapa namna mpya ya kutumia Neno la Mungu katika sasa hivi. Alikuwa akionyesha kutopitwa na wakati na uhalisia wa sheria ya Mungu.
Ujumbe wa Paulo kwa Wayahudi na Wamataifa
Baada ya kifo na kufufuka kwa Yesu, Injili (kwa maana halisi, “habari njema”) ilienea kwa watu katika maeneo yote ya jirani, Wayahudi na watu wa Mataifa (wasio Wayahudi) pia.
Lakini washiriki Wayahudi wa kanisa la Kikristo la awali walipambana kuelewa injili na mara nyingine tena wakazingatia tamaduni na sherehe zao kuliko injili.
Walianza kulazimisha desturi hizi kwa washiriki wa kanisa wasio Wayahudi pia.
Hata hivyo, Paulo alikuwa na ukweli wa sasa wa kutoa kwa kanisa la awali. Katika barua yake kwa Wagalatia katika Agano Jipya, aliandika:
“Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo” (Wagalatia 3:28, SUV).
Injili ya Yesu Kristo haikuwa imekusudiwa kwa kikundi kimoja cha watu tu. Ilikuwa imekusudiwa kwa watu wote.
Sasa tumejifunza baadhi ya mifano ya kibiblia ya ukweli wa sasa, hebu tujifunze kuhusu umuhimu wake katika Uadventista.
Kwa nini ukweli wa sasa ni muhimu kwa Kanisa la Waadventista wa Sabato?

Photo by Emmanuel Phaeton on Unsplash
Ukweli wa sasa ni sehemu muhimu ya Kanisa la Waadventista wa Sabato kwa sababu mafundisho yetu ya msingi mengi—ikiwemo Sabato, wokovu kwa imani, Kazi ya Yesu katika patakatifu pa mbinguni, na ujumbe wa malaika watatu—uligunduliwa wakati Mungu alipotoa ufunuo mpya wakati wa kujifunza Biblia kwa unyenyekevu.
Kwa sababu ya ukweli wa sasa, Uadventista uko ulivyo leo.
Ukweli wa sasa unaendelea kuwa dhana muhimu katika Kanisa la Waadventista wa Sabato karibu miaka 200 baadaye. Umuhimu wake unaweza kufupishwa kwa sababu zifuatazo.
- Unatuzuia tusiunge mkono mafundisho ya wanadamu
- Unatuzuia tusiwe wafuasi wa msimamo mkali wa kidini
- Unatuzuia tusome Maandiko na kufanya mazungumzo kati yetu
- Unatusaidia kuelewa nyakati tunazoishi ndani yake
Unatuzuia tusiunge mkono mafundisho ya wanadamu
Waasisi wa Uadventista walithamini ukweli wa sasa kwa sababu ulizuia kanisa kushikilia aina yoyote ya imani ya kibinadamu badala ya Biblia.
Lakini ili kuelewa hili vizuri zaidi, tunahitaji historia kidogo.
Wakati Kanisa la Waadventista wa Sabato lilipokuwa katika miaka yake ya mwanzo, moja ya mambo yaliyolifanya liwe tofauti na harakati nyingine za kidini za wakati huo ilikuwa upinzani wake mkali dhidi ya mafundisho ya imani au “taarifa rasmi za imani za kidhehebu ambazo kwa dhana zilizoonekana kana kwamba haziwezi kubadilika.”5
James White alisema kwamba “kuunda imani ni kuweka vizuizi, na kuziba njia ya maendeleo yote ya baadaye.”6
Na John Loughborough, mhubiri wa awali wa Waadventista, alisema kwa nguvu:
“Hatua ya kwanza ya uasi ni kuunda kanuni, kutuambia ni nini tutakachopaswa kuamini. Ya pili ni kufanya kanuni hiyo kuwa kipimo cha ushirika. Ya tatu ni kuwajaribu washiriki kwa kanuni hiyo. Ya nne ni kuwatangaza wale ambao hawaamini kanuni hiyo kuwa makafiri. Na, ya tano, kuanza mateso dhidi yao.”7
Kupinga imani kali na isiyoweza kubadilika ilimaanisha kwamba Waadventista wa mwanzo wangeweza kusikiliza kwa makini sauti ya Mungu na kweli ambazo Anaweza kufunua.
Hapa ndipo ukweli wa sasa unapoingia.
Dhana ya ukweli wa sasa iliwapa Waadventista wa mwanzo uhuru wa kugundua mambo mapya kuhusu imani yao. Hakika, walitaka kuwa wazi kupokea ukweli zaidi kutoka kwa Mungu.
Unatulinda dhidi ya msimamo mkali wa kidini.
Msimamo mkali wa kidini, au utiifu usiobadilika kwa kanuni za msingi na tamaduni za dini, ni kitu ambacho waanzilishi wa mwanzo wa Waadventista wa Sabato walikiepuka. Ufundishaji wa ukweli wa sasa uliwakumbusha wao—na sisi—kwamba haijalishi imani zetu za msingi ni nyingi au za zamani kiasi gani, lazima tuwe tayari daima kupokea kweli kutoka kwa Mungu.
Mfano mmoja wa hili ulitokea katika kikao cha mwaka 1888 cha Mkutano Mkuu wa Waadventista Wa Sabato.
Kwa ufupi, mkutano huu ulisaidia kubadilisha kanisa kutoka kuzingatia sheria na tamaduni zilizopendwa hadi kuzingatia wokovu kwa imani katika Bwana wetu Yesu Kristo. Tunapomkubali kwa imani, Yeye hutupa nguvu ya kuishi kwa ajili Yake.
Mabadiliko haya katika mtazamo hayakutokea kwa urahisi. Lakini wakati kanisa lilikuwa hatarini kuwa na msimamo, Mungu alifunua ukweli wa wokovu kwa imani kwa wana matengenezo vijana na Ellen White.
Katika mada hii, alisema:
“Hakuna kisingizio kwa yeyote kuchukua msimamo kwamba hakuna ukweli zaidi wa kufunuliwa na kwamba maelezo yetu yote ya Maandiko hayana kosa. Ukweli kwamba mafundisho fulani yamekuwa yakishikiliwa kama ukweli kwa miaka mingi na watu wetu sio ushahidi kwamba mawazo yetu ni makosa. Umri hautafanya kosa kuwa ukweli, na ukweli unaweza kujitetea. Hakuna fundisho la kweli litakalopoteza chochote kwa uchunguzi wa karibu.”8
Tunapokuwa wazi kwa mitazamo mipya ambayo Biblia inaweza kuwa nayo kwetu, tunabaki wenye mzunguko na tunajilinda dhidi ya misimamo mikali ambayo hatimaye inaweza kutufanya tuache Neno la Mungu.
Unatupa nafasi ya kutafakari Maandiko na kufanya mazungumzo na wenzetu
Ukweli wa sasa unahakikisha kwamba hatunyamazi linapokuja swala la ufahamu wetu wa Biblia.
Tunatambua kwamba ni usalama wa uwongo kufikiri tuna 100% ya ukweli ambao Mungu anataka tujue.
Majadiliano, mazungumzo, na jamii ni thamani kuu za Kanisa la Waadventista wa Sabato, na tunapojifunza Maandiko pamoja, tunaweza kugundua ukweli wa Mungu wa sasa kwetu pia.
Tena, tukimnukuu Ellen White kuhusu mada hii:
“Wakati watu wa Mungu wanapokua katika neema, daima watakuwa wanapata kuelewa zaidi Neno lake…. Lakini wakati uzima halisi wa kiroho unapungua, daima kumekuwa na tabia ya kusita kuendelea katika kujifunza ukweli. Watu hujiridhisha na mwanga walioupokea tayari kutoka katika Neno la Mungu, na kukataza uchunguzi zaidi wa Maandiko. Wanakuwa na msimamo mkali, na kujaribu kuepuka majadiliano…. Wengi sasa, kama ilivyokuwa zamani…wataambatana na tamaduni, na kuabudu wasichokijua…. Wakati watu wa Mungu wametulia, na kuridhika na mwanga wao wa sasa, tunaweza kuwa hakika kwamba h autawasaidia.”9
Kanisa la Waadventista linashikilia kuwa ni muhimu kwa afya ya kiroho ya kanisa kushiriki katika kujifunza Biblia pamoja, ili kuendelea kwa kudumu katika ukweli ambao Neno la Mungu linao kwa ajili yetu.
Unatusaidia kuelewa nyakati tunazoishi
Mafundisho mengi muhimu ya Uadventista yamejengwa na dhana ya kweli ya sasa. Imetusaidia kuelewa umuhimu wa vipengele fulani vya Biblia kwa wakati wetu maalum.
Tunasisitiza ukweli huu wa sasa kwa sababu tunaamini ni muhimu kwa wakati tunaoishi sasa.
Baadhi ya mifano ni unabii wa Danieli na Ufunuo pamoja na ujumbe wa malaika watatu katika Ufunuo 14:6–12. Tunasisitiza ukweli huu wa Biblia kwa sababu tunaamini kwamba unatuandaa kwa ajili ya ujio wa pili wa haraka wa Yesu! Unaelezea siku za sasa na karibu siku zijazo.

Photo by Aron Visuals on Unsplash
Ujumbe kwa wakati kutoka kwa Mungu asiyepitwa na wakati
Muda unavyokwenda na tunakaribia mwisho wa dunia na ujio wa pili wa Kristo, tunaweza kupokea ukweli wa sasa zaidi kutoka kwa Mungu. Anaweza kutufunulia mambo katika Maandiko ambayo hatukuyaona—au hatukulazimika kuyaona—kabla.
Lakini tunaweza kuwa na imani kwamba Mungu atafunua ukweli kwetu wakati wa kufunuliwa kwa kweli hizo.
Kwa kusoma Maandiko na kujadiliana pamoja, tunaweza kusikiliza mwongozo wa Roho Mtakatifu na kuendelea kukua katika safari yetu ya kiroho na Mwokozi wetu.
Ikiwa unataka kujifunza zaidi kuhusu kuwa na safari yako ya kiroho na Yesu, unaweza kubonyeza kitufe hapa chini kwenda kwenye ukurasa wetu wa masomo ya Biblia.
Chagua Masomo ya Biblia Mtandaoni
Unataka kuendelea kujifunza? Pata habari zaidi kuhusu Yesu, mwanadamu, mpango wa wokovu, na jinsi Mungu anavyokupenda kiasi cha kutosha kujitolea kila kitu, ili tu kukupatia nafasi ya kumchagua.
Wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kujua pa kuanzia, ndio maana tunatoa chaguo za masomo ya Biblia mtandaoni bure, rahisi kutumia, unaweza kufanya wakati wowote, mahali popote, na kwa kasi yako mwenyewe.
Shule hii ya Biblia mtandaoni itakuelekeza kupitia mada kuu za Maandiko, ikivunja dhana ngumu za Biblia katika vipande vidogo, ambavyo vinaweza kukusaidia kupata majibu ya maswali magumu zaidi ya maisha.
- Roberts, Randy, “Why I Am an Adventist”, Praxis, Loma Linda Church, August 21, 2021. [↵]
- White, Ellen G., Testimonies for the Church, vol. 2 (Pacific Press, Mountain View, CA, 1868), p. 693. [↵]
- White, James, “A Sketch of the Rise and Progress of the Present Truth”, The Review and Herald, Dec. 31, 1857, p. 61. [↵]
- White, Ellen G., The Review and Herald, June 29, 1886. [↵]
- Knight, George, A Search for Identity: The Development of Seventh-day Adventist Beliefs, p. 21. [↵]
- White, James, The Review and Herald, October 8, 1861. [↵]
- Knight, George, A Search for Identity: The Development of Seventh-day Adventist Beliefs, p. 22. [↵]
- White, Ellen G., The Review and Herald, December 20, 1892. [↵]
- White, Ellen G., Testimonies for the Church, vol. 5 (Pacific Press, Mountain View, CA, 1882), pp. 706–707. [↵]
Kurasa zinazohusiana
Majibu Zaidi
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria” Za Ndoa?
Dini nyingi au tamaduni ulimwenguni zina mila, taratibu, au matarajio ya kipekee katika ndoa au sherehe ya harusi.
Viongozi wa Kanisa: Ni Nini Majukumu ya Mchungaji wa Kiadventista?
Wachungaji – tumesikia juu yao, lakini wanafanya nini hasa? Hebu tuangalie nafasi ya mchungaji wa Kiadventista katika kanisa.
Biblia Inasema Nini Kuhusu Staha na Adabu?
Biblia inafundisha kwamba adabu, aina ya unyenyekevu na heshima, ni sifa yenye thamani kwa kila mtu—wanaume, wanawake na watoto.
Muhtasari wa Elimu ya Juu ya WaAdventista wa Sabato
Muhtasari wa Vyuo Vikuu Vya Waadventista wa SabatoKanisa la WaAdventista Wasabato lina takribani shule za sekondari 118 ulimwenguni kote.1 Ingawa nyingi zipo ndani ya Amerika Kaskazini, pia utapata vyuo vikuu vya WaAdventista katika nchi mbalimbali duniani—mahali kama...
Waadventista Wasabato Wanatafsiri Vipi Unabii wa Biblia?
Jifunze zaidi kuhusu jinsi Waadventista wanavyotafsiri unabii katika Biblia—hasa katika vitabu kama Danieli na Ufunuo.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria”?
Tunashikilia kanuni tunazoamini zitasaidia kuweka uhusiano wa karibu na Yesu na Neno lake. Jifunze jinsi kanuni hizi zinavyo-ongoza mtindo wa maisha wa Waadventista.
Jinsi Waadventista Wanavyoshughulikia Kifo na Mazishi
Mazishi mengi ya Waadventista wa Sabato yanafanana na yale ya madhehebu mengine ya Kiprotestanti, kama vile Wamethodisti, Wabatisti, au Wapresbiteri, lakini unaweza kupata tofauti chache au taratibu za pekee.
Filamu za Kiadventista: Mahali Imani na Filamu Zinapokutana
Tangu mwanzo, lengo la Kanisa la Waadventista wa Sabato limekuwa kueneza kweli ya Mungu katika Biblia.
Ni nini Mtaalam wa Matibabu wa Kiadventista?
Mmishonari wa matibabu katika Kanisa la Waadventista ni mtu anayejali mahitaji ya matibabu ya watu kama njia ya kuonyesha upendo wa Yesu.
Je, Waadventista Wasabato Wanasherehekea Siku Kuu Zinazohusiana na Pasaka?
Kufufuka kwa Yesu, kunakoadhimishwa katika siku kuu nyingi zinazohusiana na Pasaka, ni muhimu katika imani za Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Chakula cha Pamoja Katika Kanisa la Kiadventista: Mahali Ambapo Chakula na Urafiki Vinakutana
Mara nyingi, kawaida kwenye ratiba inayotofautiana kutoka mara moja kwa wiki hadi mara moja kwa mwezi hadi mara moja kwa robo, kanisa la Waadventista litakuwa na “karamu za ushirika,” mara nyingi zikiitwa chakula cha mchana cha pamoja.
Je, Mahubiri ya Waadventista wa Sabato Yako Namna Gani?
Karibu katika kila Kanisa la Waadventista wa Sabato, mahubiri ndiyo kitovu cha ibada kuu—kama ilivyo kwa madhehebu mengi ya Kikristo ya Kiprotestanti.
Wasimamizi wa Waumini Wana Nafasi Gani Ikilinganshwa na Wachungaji?
Neno “Usimamizi wa kidini” linatokana na neno la Kigiriki laikos, ambalo maana yake ni “wa watu.”
Muundo wa Uongozi wa Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Kanisa la Waadventista wa Sabato lina mfumo wa uwakilishi unaounganisha makanisa yake zaidi ya 90,000 ulimwenguni na kuwapa washiriki wake nafasi katika kufanya maamuzi.
Kitabu cha Nyimbo cha Waadventista Wa Sabato
Kitabu cha nyimbo cha Waadventista wa Sabato ni kitabu cha nyimbo kinachotumiwa ulimwenguni kote na makanisa mengi ya Waadventista wakati wa ibada zao.

















