Luka Mwinjilisti Alikuwa Nani katika Biblia?
Tunaweza kuwa tunaifahamu Injili ya tatu ya Agano Jipya, inayojulikana kama “Injili ya Luka” au “Injili kulingana na Luka.” Lakini tunaelewa kiasi gani kuhusu mwandishi wake?
Leo, Luka anatambuliwa kama daktari, mwinjilisti, mwandishi, na mhubiri. Hakuwa sehemu ya wanafunzi 12, lakini alionyesha shauku yake ya kufuata Yesu Kristo na kushiriki Injili kupitia uhusiano wake na mtume Paulo na uandishi wake wa vitabu viwili vya Biblia.
Hivyo hebu tuangalie kwa karibu maelezo yanayojulikana kuhusu:
- Historia ya Luka
- Vitabu alivyoandika
- Mada kuu katika maandishi yake
- Kifo chake na urithi aliotuachia
Hebu tuanze kwa kujua alikotoka.
Historia ya Luka
Kuna fumbo fulani linalozunguka maisha ya awali ya Luka.
Baadhi wanaamini kwamba huenda alikuwa Myahudi wa Kihelenistiki, au Myahudi anayeishi katika utamaduni wa Kigiriki, anazungumza lugha hiyo, na huenda akachukua sehemu mbalimbali za maisha ya Kigiriki.1 Lakini wengi wanaamini kwamba alikuwa Mgiriki wa kuzaliwa.2 Hili linapendekezwa na Maandiko katika maeneo kadhaa:
- Mtume Paulo anamtaja Luka kama sehemu ya watu wa Mataifa (Wakolosai 4:10-14).
- Luka anazungumzia lugha ya Wayahudi kana kwamba sio yake mwenyewe (Matendo 1:19).
- Maandishi ya Luka yanafunua kiwango kikubwa cha ustadi katika lugha ya Kigiriki kana kwamba ilikuwa lugha yake ya kwanza.
Ikiwa kweli Luka alikuwa Mgiriki, angekuwa mtu wa Mataifa pekee, au asiyekuwa Myahudi, kuandika kitabu cha Biblia.3
Jambo moja linalojulikana kutoka kwa habari za Biblia ni kwamba Luka alikuwa daktari. Paulo alimwita Luka, “daktari mpenzi” (Wakolosai 4:14). Na pia tunaweza kuona vidokezo vya taaluma ya Luka katika maandishi yake.
Tafsiri ya Kigiriki ya akaunti ya Injili ya Luka hutoa lugha sahihi ya kitabibu kwa magonjwa kama vile dropsy na ugonjwa wa kuvimba.4 Kitabu cha Matendo ya Mitume pia hutumia lugha sahihi ya kitabibu kwa homa na kuhara, miongoni mwa mambo mengine.5
Maandishi yake pia hutoa kiwango kikubwa cha maelezo, kwa mtindo na umakini wa mtu mwenye elimu rasmi (Luka 1:1-4).
Na mbali na sifa zake za kitaaluma na kielimu, Luka alimtumikia Mungu kama mhubiri na mmisionari.6 Aliweka kipaumbele katika maisha yake kuuhubiri ulimwengu kuhusu Yesu Kristo Mwana wa Mungu (Luka 2).
Luka alikuwa na uhusiano gani na Yesu?
Kwa kawaida inaaminiwa kwamba Luka hakumfahamu Yesu yeye binafsi, bali labda alisikia habari zake kupitia wengine waliomfuata.
Inaonekana hivyo kwa sababu Biblia haitoi maelezo yoyote ya Luka na Yesu kukutana.
Luka hata anaanza maelezo yake ya Injili kwa kueleza kwamba yanategemea maelezo ya moja kwa moja ya wengine (Luka 1:2). Hii inaashiria kwamba yote ambayo Luka aliandika katika kitabu cha Luka hayakuwa uzoefu wake bali wa watu aliowahoji.
Na kwa mwandishi kama alivyokuwa Luka, bila shaka angekuwa amejumuisha mwingiliano wowote aliokuwa nao moja kwa moja na mtu ambaye kitabu chake kizima kilikuwa kinamhusu.
Kwa kweli, kuna kisa kimoja tu katika maandishi yake ambapo inaonekana alikuwa anarekodi ripoti ya moja kwa moja. Na sio katika Injili yake, bali katika Matendo ya Mitume alipozungumzia kuhusu kazi yake ya huduma pamoja na Paulo (Matendo 28:16; Matendo 16:10-17).
Luka alikuwa na uhusiano gani na wafuasi wengine wa Kristo?
Tunaona katika Filemoni 1:24 kwamba Luka alifanya kazi pamoja na Paulo na Wakristo wengine, ikiwa ni pamoja na Marko, ambaye aliandika maelezo mengine ya kisa cha Injili.
Biblia haiweki wazi ikiwa Luka aliwahi kukutana na Wanafunzi 12 wa Yesu. Lakini, ikizingatiwa kwamba mara nyingi alisafiri na Paulo (ambaye alikutana na baadhi ya wanafunzi), na kwamba maandiko yake yanajumuisha baadhi ya uzoefu wa kibinafsi wa wanafunzi, ni jambo la uwezekano kwamba Luka alizungumza na angalau baadhi yao wakati fulani.
Paulo, hata hivyo, ndiye mtu ambaye ushahidi wa Biblia unaonyesha alikuwa karibu naye zaidi . Paulo alimtaja kati ya wale aliowaita watendakazi wenzake (Wakolosai 4:10-14), na katika sura za mwisho za Matendo, alipokuwa akizungumzia huduma ya Paulo, Luka mara nyingi hutumia kirai “sisi” kana kwamba alikuwa akimhudumia Paulo na wale waliokuwa pamoja naye kwa karibu sana.7
Luka alifanya safari nyingi za uinjilisti pamoja na Paulo, akikabiliana na hali za hatari kama kufungwa gerezani, dhoruba kali, na kuzama kwa meli. Lakini alibaki karibu na Paulo wakihubiri Injili huko Troa, Makedonia, Yerusalemu, na Roma (Matendo 27:1-44).8
Hata alibaki karibu na Paulo wakati wengine walipomwacha, alipokuwa tena kifungoni. Katika barua ya mwisho ya Paulo, inaaminiwa kuwa moja ya barua zake za mwisho,9 alitaja uaminifu wa Luka, akisema:
“Jitahidi kuja kwangu upesi. Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia… Luka pekee yuko pamoja nami…”(2 Timotheo 4:9-11, SUV, msisitizo umeongezwa).
Sio jambo gumu kudokeza uaminifu wa Luka kama mmisionari. Si ajabu alipewa jina la “mpenzi” daktari na Paulo. Lazima alikuwa msaada muhimu kwa Paulo na wale aliokuwa nao safarini.
Maandishi ya Luka
Kuhusu uandishi wa Luka wa Injili yake na Matendo ya Mitume (inayojulikana zaidi kama Kitabu cha Matendo), habari hii haielezwi moja kwa moja katika Maandiko. Lakini vitabu hivi kwa ujumla vinahusishwa naye pamoja kwa sababu:
- Hakuna mashaka kwamba Luka Mwinjilisti aliandika kitabu cha Luka. Hata hati za awali za Injili ya Luka zina “kulingana na Luka” katika jina kitabu.10 Na kuelekezwa kwa Injili ya Luka na Matendo kwa Theofilo kunayafanya kuwa kazi ya vitabu viwili vilivyoandikwa na mtu mmoja.
- Katika sura ya kwanza ya Matendo, mwandishi anataja “hadithi yake ya kwanza” kuhusu “yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, hata siku ile alipochukuliwa juu…” (Matendo 1:1-2,UV030). Huo ni muhtasari wa kisa chote cha Injili.
- Mwandishi wa Matendo anazungumzia kuhusu kwenda na Paulo katika safari zake za kimishonari, na Paulo anamthibitisha Luka kama mtu aliyehudumu kwa karibu naye (Wakolosai 4:14; 2 Timotheo 4:11). Wataalamu wa historia na viongozi wa kanisa la awali pia wanamuelezea Luka kama mfanyakazi mwenza katika huduma.11
- Waandishi wengi wa Biblia hawatumii lugha sahihi ya matibabu kwa sababu hawakusomea udaktari. Luka, hata hivyo, alikuwa daktari. Inaelekea kwamba yeye ndiye aliyekuwa na jukumu la kuandika vitabu viwili vilivyokuwa na lugha sahihi ya matibabu.12
Tukiwa na mambo haya akilini, hebu tuangalie vipengele muhimu vya Injili ya Luka.
Injili Kulingana na Luka

Photo by Tim Wildsmith on Unsplash
Baada ya akaunti za Injili za Mathayo na Marko, hadithi ya Luka kuhusu maisha na huduma ya Yesu ndiyo Injili ya mwisho katika Injili zinazoendana , au iliyoelezwa kama muhtasari wa kihistoria.
Luka alianza kwa kuzungumza na mtu aliyeitwa Theofilo. Na kwa kuwa Luka anazungumza Theofilo “mtukufu” msemo wa kawaida wa heshima, baadhi wanaamini hii inaweza maanisha Luka alikuwa anaandika injili hii kwa afisa mwenye cheo kikubwa.13
Na kwa kuzingatia mtindo na kina cha uandishi wa Luka, inaonekana alikuwa anaandika kwa watu kama Theofilo akilini, ili kuwasaidia kuelewa na kukubali Injili vizuri zaidi.
Wengine wanaamini kwamba Theofilo huenda alikuwa mtu aliyesaidia kugharamia uandishi wa vitabu vya Luka ili yeye na wasomaji wengine wa Mataifa waweze kujifunza zaidi kuhusu Yesu.14
Ukweli ni kwamba Luka alikuwa anaandika kwa wasikilizaji wa Mataifa unathibitishwa zaidi na jinsi alivyozingatia zaidi huduma ya Yesu kwa Mataifa kuliko rekodi nyingine yoyote ya Injili.15 Aidha, Luka “anatafsiri maneno ya Kiaramu kwa maneno ya Kigiriki na kueleza desturi za Kiyahudi na jiografia ili kufanya Injili yake iweze kueleweka zaidi kwa wasomaji wake wa asilia ya Ugiriki.16
Mbali na kutoa ufahamu zaidi kwa wasomaji wa Mataifa, Luka alitoa muktadha wa kina zaidi kwa kutaja visa na mifano ambayo haipatikani katika rekodi nyingine za Injili.
Baadhi ya mifano hiyo ni ule wa Msamaria Mwema, Mwana Mpotevu, na Tajiri na Lazaro.17
Mfano wa Msamaria Mwema unasimulia kisa cha Myahudi ambaye alisaidiwa na Msamaria mwenye huruma na ukarimu (Luka 10:25-37). Myahudi mmoja aliporwa na kupigwa njiani. Watu tofauti, ikiwa ni pamoja na kuhani na Mlawi, walimwona amelala chini akiwa ameumizwa lakini hawakusimama kumsaidia. Lakini kisha Msamaria, ambaye watu wake walikuwa na uhasama mkali na Wayahudi, alisimama kumsaidia. Yesu alitumia mfano huu kuonyesha jinsi ufalme wa Mungu haukuishia kwa Wayahudi pekee, bali kwa kila mtu anayefanya mapenzi yake kwa kumpenda jirani yake.
Mfano wa mwana mpotevu unasimulia jinsi mwana alivyopoteza urithi wake kwa upumbavu na baadaye kurudi kwa baba yake, akiwa amechakaa na kuomba kazi (Luka 15:11-32). Lakini badala ya kuwa na hasira au kumkataa mwanawe, baba anamkaribisha kwa mikono kunjufu. Kisa hiki kinaonyesha jinsi Mungu atakavyotusamehe kwa furaha tunaporudi kwake.
Hatimaye, mfano wa tajiri na Lazaro unasimulia kisa cha tajiri ambaye hakutoa chochote kwa maskini mmoja aliyeitwa Lazaro (Luka 16:19-31) baada ya vifo vyao. Lazaro aliletwa kwenye “Kifua cha Ibrahimu,” mahali pa kufikirika panapowakilisha maisha mema baada ya kifo. Na tajiri alienda kuzimu, ikionyesha maisha ya adhabu baada ya kifo. Ingawa kisa hiki hakikukusudiwa kuonyesha kwa usahihi kinachotokea baada ya watu kufa, kisa hiki hutumiwa kuwasilisha wazo kwamba aina ya tabia ambayo watu wanakuza katika maisha yao ya duniani itaathiri hali yao ya milele. Kwa maneno mengine, watu watawajibishwa kwa kushindwa kuonyesha huruma na rehema kwa wenzao kama vile Yesu alivyofanya, ambayo pia inaonyesha kushindwa kumkubali Yesu kama mwokozi na Mwana wa Mungu.
Kwa jumla, mifano hii inasaidia kufikisha upendo mkubwa wa Mungu kwetu na upendo ambao tunapaswa kuwa nao kwa wengine, bila kujali ni akina nani.
Luka pia alizingatia ubinadamu wa Yesu Kristo, akitoa kwa wasomaji picha kamili zaidi ya tukio la kuzaliwa kwake kwa kumtaja malaika Gabrieli alivyomtokea Mariamu (Luka 1:26-38), ziara ya Mariamu kwa binamu yake, Elisabeti (Luka 1:39-45), na kuzaliwa kwa Yohana Mbatizaji (Luka 1:57-66).
Luka pia alisisitiza jukumu la Yesu kama Mwana wa Adamu aliyetabiriwa katika Agano la Kale kwa kuonyesha jinsi alivyo shinda mapambano ya kibinadamu na kuishi maisha bila dhambi.18
Matendo ya Mitume

Photo by Kyle Glenn on Unsplash
Kitabu cha Matendo ya Mitume kinaeleza jinsi kanisa la awali la Kikristo lilivyo kubali utume wa kueneza Injili kote ulimwenguni.
Kama ilivyoandikwa katika Injili ya Luka, kitabu cha Matendo ya Mitume pia kinamlenga Theofilo (Matendo 1:1) na kimeandikwa kwa mtindo na maneno yanayofanana. Vitabu hivi viwili pamoja, kulingana na Komentari ya Biblia ya Kanisa la Waadventista wa Sabato, vinaweza kuitwa kwa ufasaha, “Mwanzo na Maendeleo ya Ukristo.19
Maelezo yake pia yanaendana na ushahidi wa kisayansi.20 Aliitumia majina, lugha, na maelezo yanayolingana na taarifa zinazopatikana kwenye michoro ya kumbukumbu.21
Hivyo, Luka alipataje taarifa nyingi kwa ajili ya vitabu vyake?
Labda kutokana na historia yake ya elimu ya juu, Luka lazima alitumia vyema safari zake za kimishonari na kurekodi maelezo muhimu, kushauriana na mashahidi, na kufanya utafiti zaidi.22 Na baadhi ya sehemu za maandishi yake zilijumuisha uchunguzi wake mwenyewe.
Alishuhudia Paulo akitoa pepo na kumfufua mtu (Matendo 16:16-18; Matendo 20:7-12).
Aliuona uweza wa Roho Mtakatifu ukiwa kazini wakati wa Pentekoste, kutukumbusha jinsi Roho Mtakatifu alivyolikuza Kanisa la Kikristo tangu wakati huo (Matendo 2:1-4).
Luka alishuhudia kanisa la awali likiendelea kukua kutoka kwa kikundi kidogo cha wafuasi Wayahudi hadi kuwa vuguvugu lililosambaa katika Bahari ya Kati.
Mada muhimu katika maandishi ya Luka
Baada ya kuzungumza kuhusu nafasi ya Luka katika kuandika Injili ya Luka na Matendo ya Mitume, hebu tuangalie mada na mafundisho ambayo vitabu hivi vinatupatia.
Baadhi ya mafundisho hayo ni pamoja na:
- Huruma kwa wote:
- Luka anazingatia visa vya watu waliotengwa zaidi kuliko kitabu kingine chochote cha Injili. Aliandika kuhusu wajane na maskini, na alihakikisha anawataja wanawake pia, jambo ambalo halikuwa la kawaida wakati huo.23 Lakini aliwanafsisha watu hawa, kuonyesha kwamba wanamhitaji Mwokozi kwa namna ile ile kama wengine wote. Pia aliandika kuhusu kuonyesha upendo na msamaha kwa wahalifu.24
- Wokovu kwa wote:
- Luka pia alilijikita katika mada ya wokovu kwa watu wote—hasa watu wa Mataifa. Hii ilikuwa ya kipekee kwa wakati huo kwani Wayahudi walikuwa wanachukuliwa kama watu walioteuliwa na Mungu kwa muda mrefu. Wayahudi waliamini Masihi angekuja kuwaokoa Israeli na Yuda. Hawakuwahi kufikiria kwamba alikuwa amekuja kuwaokoa pia watu wa Mataifa.
- Na bado, Luka anasimulia matukio ambapo Bwana Yesu anaitikia mahitaji ya watu wa Mataifa, hata wale waliotazamwa kama maadui wa Wayahudi—kama Wasamaria au watu kutoka taifa la Kirumi.25 Walitangaza imani yao Kwake na Yeye aliwasaidia. Wanafunzi waliendeleza kazi hii katika Matendo ya Mitume walipotafuta kueneza habari njema ya Kristo kwa sehemu zote za dunia. Tunaweza kuona hili katika mfano wa safari za kimishonari za Paulo kwenda nchi za mbali na jinsi Petro alivyoaminiwa kuwafikia watu wa Mataifa kama Kornelio (Matendo 10:1-36).
- Kumiminwa kwa Roho Mtakatifu:
- Mada nyingine muhimu katika maandishi ya Luka ni Roho Mtakatifu. Maandishi ya Luka yanatuonyesha jinsi Roho Mtakatifu alivyotolewa kwa mitume siku ya Pentekoste (Matendo 2:1-4). Lakini Luka hakuishia hapo. Aliendelea kuandika jinsi Roho Mtakatifu alivyoongoza Kanisa la Kikristo la awali kupitia maono, miujiza, na karama nyingine za Roho.26
- Ukweli kwamba Roho Mtakatifu hakuwa akifanya kazi tu kupitia Wayahudi ulionyesha kwamba Roho habagui kwa jinsia au kabila. Badala yake, alitolewa kwa yeyote aliyekuwa tayari kuipokea (Matendo 21:9; Matendo 10:44-48).
Kama daktari, Luka huenda alijisikia kuvutiwa katika kupunguza mateso ya wengine kwa kuwaonyesha upendo na huruma. Inaeleweka kwamba angekuwa na nia ya kusaidia wale wanaohitaji msaada.
Mada hizi pia zinaunga mkono jinsi Luka alivyokuwa na shauku ya kuhudumia watu wa Mataifa pamoja na Wayahudi. Hii ingekuwa na maana kwa yeye mwenyewe kuwa ni Mtu wa Mataifa. Hii inamfanya Luka kuwa kati ya viongozi wa kanisa la awali ambao walikuwa wakilenga zaidi kuhudumia Wayahudi, au wengine ndani ya mduara wao, badala ya kuwapa kipaumbele watu wa Mataifa au wanajamii walioachwa kama vile maskini, wagonjwa, au wajane.
Lakini Luka aliwahimiza Wakristo wa awali kuvunja vizuizi hivyo, kushiriki habari za Yesu na yeyote ambaye angekuwa tayari kusikiliza.
Na hivyo ndivyo Luka alivyoishi maisha yake yote. Biblia haijasema jinsi Luka alivyokufa. Kitu cha mwisho Biblia inachosema kuhusu maisha yake ni kwamba alisafiri na Paulo katika safari yake ya kimishonari kwenda Rumi (2 Timotheo 4:11).27 Wengine wanapendekeza kwamba aliuawa kwa imani yake kwa kusulubiwa kwenye mti wa mzeituni hai nchini Ugiriki.28 Wengine wanadhani alifia Bethania.29 Ingawa hatuwezi kujua kwa uhakika jinsi Luka alivyokufa, ni salama kufikiria kwamba aliishi maisha yake yote akifundisha wengine kuhusu Yesu. Na maneno ya vitabu vyake bado yanatuhimiza leo. Alitupatia moja ya visa vya kina kabisa kuhusu maisha ya Yesu, hadi kufikia mwanzo wa Kanisa la Kikristo la awali. Alitambulisha watu muhimu katika Ukristo wa awali kama Paulo na kutuonyesha jinsi Roho Mtakatifu alivyowaongoza wafuasi wa Yesu. Maelezo mazuri aliyotoa na mtazamo wake wa kipekee kuhusu huduma ya Kristo yanaimarisha ufahamu wetu wa historia ya kanisa la awali huku akisisitiza kwamba habari njema ya Yesu Kristo ni kwa kila mtu—wakiwemo watu wa Mataifa: “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu.” (Luka 24:46-47, SUV, msisitizo umeongezwa). Luka huenda alikumbana na kutengwa kama watu wengine wa Mataifa walivyokumbana na hali hiyo. Lakini hakuruhusu hilo kumzuia asiwe tayari kumtumikia Mungu. Na alitumia nafasi yake ya kipekee kuwapa watu wa Mataifa matumaini kwamba nao wanaweza kumfuata Yesu. Je unatamani kujifunza kuhusu waandishi wengine wa kisa cha Injili? Soma kuhusu Mathayo, Marko, au Yohana.
Kufuatilia Safari ya Utume ya Luka akiwa na Paulo
- Aliondoka Troa pamoja na Paulo (Matendo 16:11).
- Alisafiri pamoja na Paulo kwenda Filipi (Matendo 16:12).
- Alishuhudia uongofu wa Lidia (Matendo 16:13-15).
- Aliona Paulo akimtoa pepo msichana (Matendo 16:16-18).
- Alikaa Filipi; ikirejelea sehemu za “sisi” wakati Paulo anarudi Filipi (Matendo 20:5-6).
- Alishuhudia Paulo akimfufua mtu (Matendo 20:7-12).
- Alikutana na wanafunzi huko Tiro (Matendo 21:3-4).
- Alikutana na Filipo mwinjilisti na mabinti zake (Matendo 21:8-9).
- Alishuhudia nabii mmoja aitwaye Agabo akimwonya Paulo (Matendo 21:10-11).
- Alimwomba Paulo asikwee Yerusalemu (Matendo 21:12).
- Akajiunga naye katika safari yake kwenda Yerusalemu (Matendo 21:17).
- Akapona baada ya meli kuzama na kutua Malta (Matendo 27:1-44; Matendo 28:1).
- Alishuhudia Paulo akiponywa kimiujiza baada ya kuumwa na nyoka (Matendo 28:3-6).
- Alitazama Paulo akiwaponya watu wa Malta (Matendo 28:7-10).
- Akifuatana na Paulo kwenda Rumi na kukaa naye huko (Matendo 28:14-16).
- Alimsaidia Paulo wakati wa kifungo chake (2 Timotheo 4:11).
Kurasa zinazohusiana
- The Remnant Study Bible, Remnant Publications, 2009. pp. 1205. [↵]
- Ibid. [↵]
- Ellis, Earle E., “Saint Luke,” Britannica, August 5, 2024. [↵]
- Hubbard, Reuben A., “Medical Terminology in Luke,” May 1977, Ministry Magazine. [↵]
- Ibid. [↵]
- Philemon 1:24; 2 Timothy 4:11; Acts 28:16; Acts 16:10-17; Acts 20:6; Acts 27:1. [↵]
- Ellis [↵]
- Acts 27:1-44; Philemon 1:24; 2 Timothy 4:11; Acts 28:16; Acts 16:10-17; Acts 20:6; Acts 27:1. [↵]
- Ibid. [↵]
- Nichol, Francis D. Seventh-day Adventist Bible Commentary And Bible Students’ Source Book, Vol. 5 , 1978, p. 663. [↵]
- Ibid. [↵]
- Hubbard. [↵]
- “Who is Theophilus in the Bible books of Luke and Acts?” Bible Info; “The Gospel According to Luke.” Britannica. [↵]
- Remnant Study Bible, p. 1205. [↵]
- Seventh-day Adventist Bible Commentary, Vol. 5 . p. 665. [↵]
- Remnant Study Bible, p. 1205. [↵]
- Luke 10:25-37; Luke 15:11-32; Luke 16:19-31. [↵]
- Remnant Study Bible, p. 1206. [↵]
- Seventh-day Adventist Bible Commentary, Vol. 5, p. 665. [↵]
- Remnant Study Bible, p. 1288. [↵]
- Edwards, James R., “Archaeology Gives New Reality to Paul’s Ephesus Riot,” Biblical Archaeology Society, 2016. [↵]
- Ibid. [↵]
- Luke 16:19-31; Luke 1:39-56; Luke 18:1-8. [↵]
- Luke 23:39-43. [↵]
- Luke 7:2-3, 9-10; Luke 17:11-19. [↵]
- Acts 2:4; Acts 3:6-8; Acts 4:30-31; Acts 10:9-23. [↵]
- “Saint Luke,” [↵]
- Seventh-day Adventist Bible Commentary, Vol. 5, p. 663. [↵]
- “Saint Luke,” [↵]
Majibu Zaidi
Yohana ni Nani, Mwanafunzi “aliyependwa na Yesu”?
Biblia inasemaje kuhusu mtume Yohana? Anajulikana kwa jambo gani leo? Jifunze zaidi kuhusu maisha, huduma, na urithi wa Yohana hapa.
Kujifunza Kuhusu Marko – Mwandishi wa Injili na Mfuasi wa Yesu
Kujifunza Kuhusu Marko - Mwandishi wa Injili na Mfuasi wa YesuMarko (ambaye jina lake kamili lilikuwa Yohana Marko) alikuwa na majukumu mengi katika Agano Jipya: alikuwa mfuasi wa awali wa Yesu Kristo, alisafiri katika Bahari ya Kati kama mhubiri wa Kikristo, na...
Mfalme Daudi: Alikuwaje Mtu Ambaye Aliupendeza Moyo wa Mungu?
Vita, umwagaji damu, mauaji, uzinzi—maovu haya yote yalifunika maisha ya mtu wa Agano la Kale aliyeitwa Daudi.
Mariamu Magdalene ni Nani Katika Biblia?
Mariamu Magdalene alikuwa mfuasi na msaidizi wa kipekee wa Yesu Kristo wakati wa huduma yake duniani.







