Mfano wa Lulu, au Lulu ya Thamani Kubwa, ni somo kutoka kwa Yesu kuhusu ufalme wa Mungu. Unapatikana mara moja tu katika Agano Jipya, katika Mathayo 13:45-46. Na una tafsiri kuu mbili.
Moja, inamweka Yesu Kristo kama mfanyabiashara, anayejitoa kwa kila kitu ili kuwaokoa watu Wake. Na ya pili inaweka watu binafsi kama mfanyabiashara anayetafuta Mwokozi.
Basi, ni tafsiri ipi iliyo sahihi—au inawezekana zote mbili zikawa sahihi?
Kuna mengi zaidi katika mfano huu mfupi uliojaa nguvu kuliko inavyoonekana kwa macho.
Ili kuelewa mambo muhimu ya kujifunza, hebu tuuangalie kwa karibu zaidi:
Tunapoendelea, maana ya mfano huu itafanya iwe wazi jinsi tulivyo wa thamani mbele za Mungu, na thamani ya ufalme Wake kwetu.
Hebu tuanze kwa kukumbuka kisa chenyewe.
Mfano wa Lulu ya Thamani katika muktadha

Photo by Marin Tulard on Unsplash
Mfano wa Lulu ya Thamani umeandikwa tu katika Injili ya Mathayo. Na umezungukwa na mifano mingine kadhaa ambayo yote ina mada ile ile: “ufalme wa mbinguni,” au “ufalme wa Mungu.”
Mfano mzima ni sentensi moja tu, iliyogawanywa katika aya mbili:
“Tena ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri; naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akainunua” (Mathayo 13:45-46, SUV).
Yesu alisimulia mfano huu akiwa ndani ya mashua (inawezekana ilikuwa kwenye Bahari ya Galilaya) kwa umati mkubwa uliokuwa umesimama ufukweni (Mathayo 13:1-3). Ilikuwa ni mwaka wa pili wa huduma Yake ya hadhara, na alikuwa anabadilisha mwelekeo wa mafundisho Yake.
Yesu alikuwa amewaeleza wanafunzi Wake kwa nini sasa alikuwa anazungumza kwa mifano (Mathayo 13:10-17):
1. Kufunua ukweli wa kiroho kwa wale wanaoutafuta kwa mioyo ya bidii.
2. Kuficha ukweli kutoka kwa watu wenye mioyo migumu.
Paulo alisisitiza sababu hii katika 1 Wakorintho 2:14:
“Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni” (SUV).
Sasa hapa kuna maelezo mafupi kuhusu “ufalme wa mbinguni” ambao Yesu aliuzungumzia mara nyingi.
Ni ufalme wa sehemu mbili. Ufalme wa Mungu usioonekana tayari umeanzishwa kwa sababu ya Yesu Kristo, ambaye alitupatia Roho Mtakatifu ili tuweze kukaa katika ushirika wa maombi naye (Luka 17:20–21; Mathayo 12:28). Lakini pia ni ahadi ya tumaini la baadaye wakati Yesu atakaporudi kuanzisha ufalme wake wa unaoonekana milele (Ufunuo 11:15).
Yesu alisimulia mifano nane katika Mathayo 13. Na sita kati ya hiyo zinaanza na kauli, “Ufalme wa mbinguni umefanana na…” Na mifano yote minane inaonyesha vipengele tofauti vya ufalme wa Mungu, pamoja na jinsi wanadamu wanaweza kuhusiana nao:
1. Mfano wa Mpanzi (13:1-9; 18-23): Mtazamo wetu unaamua jinsi tunavyopokea na kuitikia kweli kuhusu Mungu.
2. Ngano na Magugu (13:24-30; 36-43): Sote tunaishi maisha yetu katika dunia hii hii, na mwishowe sote tunakabiliwa na uamuzi mmoja: kumfuata Mungu au la. Na mwishowe, maamuzi ya kila mtu yatawekwa wazi.
3. Mbegu ya Haradali (13:31-32): Ufalme wa Mungu huanza kwa udogo, lakini hukua kupita kiasi.
4. Chachu (13:33): Nguvu ya Mungu hufanya kazi ndani yetu na kupitia sisi ili kukuza ufalme wake.
5. Hazina Iliyojificha (13:44): Tunapogundua thamani halisi ya maisha ndani ya Yesu, hakuna kitu kingine kinachoweza kulinganishwa.
6. Lulu ya Thamani Kubwa (13:45-46): Mwokozi huwatafuta watu wake kuliko yote, na mara tunapokutana na Mwokozi wetu, hakuna kingine kinacho jalisha.
7. Jarife (13:47-50): Siku moja, ufalme wa Mungu hatimaye utahitaji hesabu. Yesu atawatambua wale wanaotaka kweli kuwa sehemu ya ufalme, na wale wasiotaka.
8. Mwenye Nyumba (13:52): Wengine huchukulia huu kama muhtasari badala ya mfano wa pekee. Lakini inahusu kushiriki thamani ya ufalme na wengine.1
Yesu alizungumzia mambo mengi kuhusu ufalme wa mbinguni.
Kwa nini?
Kwa sababu dhamira Yake yote ilikuwa kuleta tumaini la mbinguni na uzima wa milele kwa wanadamu walioanguka. Anataka tuelewe thamani ya kile anachotupatia na jinsi kitakavyobadilisha maisha yetu.
Huenda pia umeona kwamba Mfano wa Lulu ya Thamani una pacha: Mfano wa Hazina Iliyofichwa. Katika Biblia, kurudia mara nyingi kunasisitiza umuhimu.
Ni wazi, Yesu alitaka kuhakikisha tunaelewa jambo hili muhimu kuhusu ufalme Wake.
Mafundisho ya Mfano wa Lulu ya Thamani Kuu
Ingawa Yesu alisema moja kwa moja kwamba Mfano wa Lulu ya Thamani Kuu unatufundisha jambo kuhusu ufalme wa mbinguni (aya ya 45), mitazamo hutofautiana linapokuja swala la maelezo ya kina.
Wengine wanasema ni kuhusu Yesu kutafuta kurejesha uhusiano Wake na wanadamu, kwa sababu anatupenda zaidi ya vile tunavyoweza kuelewa.
Na wengine wanasema hadithi hii fupi inatusaidia kuelewa kile wanadamu watakachopitia wanapogundua wokovu katika Yesu.
Wengine bado wanaamini inaweza kuwakilisha mitazamo yote miwili.
Ili kuelewa mitazamo hii, hebu tuone kile maelezo haya yanachoweza kuwakilisha:
Mfanyabiashara:
A. Yesu
B. Wanadamu wanaomtafuta Yesu
Lulu nzuri:
A. Watoto wa Mungu (wanadamu waliopotoka)
B. Kila kitu ambacho wanadamu wanakimbilia ili kutimiza maisha yao
Lulu ya Thamani Kubwa:
A. Yesu na zawadi Yake ya uzima
B. Wanadamu ambao Yesu alikufa msalabani kuwaokoa
Aliuza vyote alivyokuwa navyo:
A. Dhabihu ya Yesu kwa ajili yetu
B. Sisi kumchagua Yesu kuliko kitu chochote duniani
Mitazamo hii miwili tofauti kwa kweli inakamilishana.
(Hivyo, tunaweza kusema kwamba, badala ya kuchagua kati ya mtazamo A na mtazamo B, tunaweza kuchagua mtazamo C: vyote vilivyotajwa hapo juu.)
Ili kufafanua zaidi hili, hebu tulivunje kwa njia zote mbili.
Hivi ndivyo inavyoonekana Yesu akiwa mfanyabiashara:
Yesu (mfanyabiashara) anawatafuta wanadamu waliopotea na walioanguka (lulu). Kwa matumaini ya kuokoa hata mmoja wa watoto wa Mungu (lulu moja ya thamani isiyo na kifani), Alijitoa uhai Wake (vyote alivyokuwa navyo)
Sasa, hebu tuangalie kwa mtazamo wa mwanadamu aliyeanguka kama mfanyabiashara:
Mtu (mfanyabiashara) anatafuta kitu (lulu) cha kutimiza shauku ya ndani. Mtu huyu anamgundua Yesu (lulu moja ya thamani isiyo na kifani). Na kwa kuitikia, anaacha uhusiano wowote na dunia hii (vyote alivyo navyo) na kumchukua Yesu kama Mwokozi wake.
Sasa, hebu tuone ni nini kingine tunaweza kugundua katika maelezo ya mfano huu.
Mfanyabiashara
Haitaji mawazo makubwa kumfikiria Yesu kama yule mfanyabiashara. Yesu kuwatafuta watoto waliopotea wa Mungu ni mada inayojirudia mara nyingi katika Biblia. Hata katika Agano la Kale.
Katika Mathayo 18:12-14, Yesu anajilinganisha na mchungaji na sisi na kondoo aliyepotea anaowatafuta. Katika Malaki 3:17, Mungu anatuita “vito vyake” (SUV). 1 Wakorintho 6:20 inasema tulinunuliwa “kwa thamani” (SUV). Na Yohana 3:16 inasimulia juu ya dhabihu ya Yesu kutuokoa.
Pia si jambo la ajabu kuwafikiria wanadamu katika nafasi ya mfanyabiashara, wakitafuta “lulu nzuri” (kama tafsiri ya King James inavyosema). Tunaona vikumbusho vingi katika Biblia vya kumtafuta Kristo kwa mioyo yetu yote, na kwamba kile anachotupa ni zaidi sana kuliko kile ambacho dunia hii iliyovunjika inaweza kutoa.
Tunaona pia hisia hii katika aya za awali:
“Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote” (Yeremia 29:13, SUV).
“Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa” (Mathayo 7:7, SUV).
Na hadithi kama Mfano wa Mwana Mpotevu zinaonyesha tabia yetu ya kibinadamu ya kutafuta mambo mengine mengi kabla ya kutambua kwamba ni Yesu pekee anayeweza kutupa utimilifu kamili (Luka 15:11-32).
Inaonekana kwamba mitazamo yote miwili kuhusu mfanyabiashara ni ya kibiblia.
Sasa hebu tuangalie kuhusu “lulu nzuri.”
Lulu Nzuri

Photo by Paige Johnson on Unsplash
Tuanze na umuhimu wa lulu katika nyakati za Yesu, na kwa nini inatumika kama mfano mzuri katika mfano huu:
“Lulu…zilizingatiwa na watu wa kale kuwa kati ya vito vya thamani sana, na ziliheshimiwa sana kama mapambo. Ufalme wa mbinguni umefananishwa na ‘lulu ya thamani kuu.’ Katika Mathayo 7:6 lulu zinatumika kwa mfano kuwakilisha kitu chochote cha thamani, au hasa zaidi kwa ajili ya “maneno ya hekima.”2
Kwa upande mmoja, lulu nzuri zinaweza kuwakilisha watoto wa thamani wa Mungu—waliyojaa uwezo, na kila mmoja ana thamani isiyopimika. Yesu, kama mfanyabiashara, anatafuta kitu cha pekee chenye thamani ya kweli duniani: sisi. Kila mmoja wetu ni kazi ya mikono iliyoumbwa kwa uangalifu na makusudi na Muumbaji Anayetupenda (Zaburi 139:13-14).
Yesu haachi kamwe kututafuta, anamkumbatia yeyote anayetamani upendo Wake. Hivyo, kila mmoja wetu anapompokea kama Mwokozi wetu, ni kama mfanyabiashara aliyepata lulu ya thamani isiyopimika.
Hii pia inaunganisha na mtazamo wa wanadamu kama mfanyabiashara katika mfano huo.
Pia tunaishi pamoja na wafanyabiashara wengine wanaotafuta vitu vya thamani, na ni rahisi kupofushwa na lulu zote zinazong’aa lakini zisizo na thamani kubwa katika maisha haya. Mara nyingi tunashindwa kuona kile kilicho na thamani ya kweli. Wakati mwingine tunashikilia sana pesa, nyumba, kazi, hadhi, na kadhalika. Lakini vyote hivyo ni vya muda mfupi. Hakuna hata kimoja chenye thamani ya milele.
Tunapoifungua mioyo yetu kwa Yesu na kutambua kwamba amekuwa akitutafuta sisi muda wote, tunaacha kutafuta lulu nzuri. Tunakubali kwa urahisi kuacha lulu zote za muda mfupi zisizo na thamani kubwa tunapokumbatia lulu moja ya milele ambayo inafanya mwanga wa lulu nyingine zote kufifia.
Lulu moja ya thamani kuu
Mungu anaona lulu ya thamani ndani ya kila mmoja wetu. Lakini lulu pia inaweza kumwakilisha Yesu kama Mwokozi wetu na ahadi ya mbingu.
Basi inaonekanaje kugundua Lulu ya Thamani Kuu?
Hapa kuna maelezo mazuri, kulingana na maelezo ya Biblia:
“Yeye anayempata Kristo kama jibu la matamanio yote ya moyo wake, anayepata ndani Yake njia ya uzima kwa ukamilifu zaidi, anayepata ndani Yake lengo la maisha, amepata hazina kuu ya maisha.”3
Tunapomjua Yesu na tabia Yake ya kweli sisi wenyewe, hatutaki kamwe kumwacha. Yeye hujaza ule utupu—kile ambacho hatuwezi kukitaja lakini daima kinakosekana. Yeye hufungua macho yetu kuona kilicho cha maana, akiweka mambo yote katika mtazamo sahihi.
Aliuza vyote alivyokuwa navyo

Image by lifeforstock on Freepik
Tukubali—hii ndiyo sehemu ngumu zaidi kuelewa tunapojiona sisi kama yule mfanyabiashara. Tunaweza kuelewa Yesu kujitoa maisha Yake mbinguni na kufa ili kutukomboa. Tayari imeshafanyika. Lakini inamaanisha nini kwako na kwangu “kuuza vyote tulivyo navyo” tunapompata Yesu?
Je, inahusu kupata wokovu kwa matendo? Kamwe. Tunajua Yesu alifundisha wokovu kwa imani (Yohana 5:24; 6:28-29; Luka 7:50).
Na pia haihusu kutoa kila kitu na kuishi katika umaskini.
Ndiyo, inaweza kukukumbusha yule kijana tajiri, ambaye aliamua kwamba utajiri wa sasa ulikuwa bora kuliko maisha ya baadaye mbinguni (Mathayo 19:16-26). Lakini ni mojawapo ya matukio machache katika Biblia ambapo Yesu alimwambia mtu atoe kila kitu alichonacho.
Yesu anajua mioyo yetu, hivyo anajua nini kinachotuzuia kila mmoja wetu. Na utajiri ndio uliomzuia mtu huyu kumtegemea Mungu.
Paulo alitambua kwamba kumfuata Kristo haikuwa kuhusu kutoa kafara utajiri, bali inahusu kujisalimisha kabisa:
“Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo. Naam, zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo” (Wafilipi 3:7-8, SUV).
Alikuwa amepata kile alichokuwa akikikosa. Yesu alitimiza mahitaji yake ya ndani kabisa. Na hakuna kitu kingine kilichomjalisha tena. Ndiyo maana yule mfanyabiashara katika mfano aliona afadhali kuachana na lulu zote alizowahi kupata kwa ajili ya lulu moja ya thamani kuu.
Pia tunakuta maoni haya kuhusu mwitikio wa Paulo alipoipata Lulu ya Thamani Kuu:
“Ingawa wokovu hauwezi kununuliwa, hata hivyo unagharimu yote aliyo nayo mtu. Kama Paulo, yule anayemwona Kristo kweli atahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri wa kumjua Kristo Yesu, na kuwa tayari kuvumilia kupoteza vitu vyote ili ampate Kristo (Wafilipi 3:8). Kumjua Kristo ni kujaza pengo maishani ambalo hakuna kitu kingine kinachoweza kujaza. Kumjua Yeye ni uzima wa milele (Yohana 17:3).”4
Mapema katika huduma Yake, Yesu aliwaonya wasikilizaji wasijiwekee na “hazina” za duniani. Alisema waelekeze mawazo yao kwenye hazina ya baadaye ya uzima wa milele mbinguni (Mathayo 6:19-20).
Alitukumbusha pia kwamba, “kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako” (Mathayo 6:21, SUV).
Tunapofahamu thamani isiyo na kipimo ya uzima wa milele pamoja na Yesu, Yeye anakuwa ndiye kitovu chetu na hazina yetu.
Lolote tunalohisi tunatoa dhabihu ili kumfuata Yesu, Mungu anaahidi zaidi sana (Wafilipi 4:19). Anaweza kufanya “kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo” (Waefeso 3:20, SUV).
Lakini hilo linaweza kuonekana vipi katika maisha yetu ya kila siku?
Je, Mfano wa Lulu unatumikaje leo?

Photo by LEONARDO DOURADO
Jitihada za mfanyabiashara wa lulu kupata lulu yake ya thamani zinatukumbusha tuweke mkazo kwenye kilicho muhimu. Sio kuhusu mafanikio au kushindwa kwetu katika dunia hii. Hakuna kati ya hayo litakalokuwa na maana Yesu atakaporudi. Kilicho muhimu ni hiki:
1. Yesu anawathamini watoto Wake kuliko uhai Wake mwenyewe.
2. Tunapotambua Yesu ni nani na kile anachotoa, mambo mengine yote yanapoteza mvuto ukilinganisha na hayo.
Yesu alitutafuta na kutupata—lulu Zake. Sasa ni juu yetu kukubali kile anachotupatia: maisha mapya ndani Yake. Ndiyo maana maana hizi mbili zinakamilishana.
Yesu ana thamani kuu kuliko kitu chochote kingine ambacho tumekuwa tukikikimbilia. Anatupatia:
- Amani kamilifu, hata katikati ya machafuko (Isaya 26:3; Wafilipi 4:6-7)
- Roho Mtakatifu kutuongoza na kututia nguvu (Yohana 14:26, Yohana 16:13, Matendo 1:8)
- Kufanywa wana wa Mfalme wa wafalme (Waefeso 1:5)
- Urithi unaotusubiri mbinguni (1 Petro 1:3-4)
- Maisha mapya na yenye kuridhisha sasa (Yohana 10:10)
- Mwenye nguvu kuliko vyote kupigana upande wako (Kumbukumbu la Torati 20:4)
- Uzima wa milele Yesu atakaporudi (1 Wathesalonike 4:16-17)
Ndiyo, mara nyingi kafara na kujisalimisha inahusika.
Wokovu ni zawadi ya bure. Lakini tukishaikubali kweli, tutaanza kumweka Kristo kuwa kitovu cha maisha yetu na kumruhusu atubadilishe.
Hatuwezi kushikilia dunia ya dhambi na Mwokozi wetu kwa wakati mmoja (Mathayo 6:24; Yakobo 4:4; Wagalatia 2:20). Hii haimaanishi kwamba tunapaswa kuwa watawa juu ya mlima. Inamaanisha kwamba tunapomkabidhi Kristo maisha yetu, tutaanza kuachilia chochote kinachoweza kudhuru ahadi hiyo.
Ufalme wa Mungu na dunia yetu iliyoanguka ni kama ncha mbili za sumaku ambazo zinakataa kukaribiana. Mfano unaweza kuwa kwamba tunaporuhusu Roho Mtakatifu atubadilishe, unyenyekevu wetu utakua tunapoachilia kiburi chetu.
Mfano unaoonekana zaidi ni muumini mpya anayeanza kujifunza tabia mpya na kuacha zile za zamani. Na wakati mwingine marafiki au familia wanaweza kumletea changamoto—hasa kama walihusika kwa namna fulani katika zile tabia za zamani. Mambo ya aina hii yanaweza kuonekana kama kafara mwanzoni. Lakini tunaweza kujua kwamba ufalme wa milele wa Mungu unastahili kwa asilimia 100 kuacha chochote kinachoweza kututenganisha na Yeye.
Tukizaliwa upya katika Kristo Yesu, mabadiliko yenye afya na ukuaji wa kiroho vitafuata. Na Mungu atafanya kazi pamoja nasi tunapojisalimisha kwa chochote kinachoturudisha nyuma.
Inaweza kuonekana tofauti mwanzoni, lakini inaweza kuwa huru sana!
Ni kama pale mume na mke wanapoamua kuwa wazazi. Hiyo ni kafara hakika. Mtazamo wao utabadilika milele. Haitakuwa rahisi kila wakati, lakini watapata aina ya furaha ya kina ambayo inaweza kupatikana tu kwa kuwa wazazi.
Na ukifikiria, kila wakati tunapojitolea kwa kitu tunachokithamini, tunakuwa na muda na umakini mdogo kwa mambo mengine. Huu ni mbadilishano wa kawaida, na unasimamiwa na kile tunachokiona kuwa muhimu katika maisha yetu. Na wakati mwingine, hata haionekani kama kafara kubwa kwa sababu ukilinganisha na kile tunachokithamini, hakuna kitu kingine kinachotuletea furaha au utimilifu wa aina hiyo.
Tunapoanza kuishi maisha na Yesu, tunagundua kwamba chochote anachotuomba tukiachie kitafanya maisha kuwa bora—si mabaya zaidi. Hata kama mwanzoni haionekani hivyo.
Ndiyo maana anasema, “Mzigo wangu ni mwepesi” (Mathayo 11:30, SUV).
Tunapomwamini kwa maisha yetu, anaahidi kutupa “mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo” (Waefeso 3:20, SUV).
Thawabu ya kujisalimisha kwa Kristo huenda isionekane au kupimika hapa duniani. Na haitakuwa na maana kwa wale wasiomjua Kristo (1 Wakorintho 1:18). Lakini daima huleta furaha na amani.
Ni Yesu pekee “Maana hushibisha nafsi yenye shauku” (Zaburi 107:9, SUV). Yeye hujaza nafasi ule utupu ndani yetu sote.
Ndiyo maana Mfalme Daudi alisema:
“Utanijulisha njia ya uzima; Mbele za uso wako ziko furaha tele; Na katika mkono wako wa kuume Mna mema ya milele” (Zaburi 16:11, SUV).
Alikuwa amegundua lulu ya thamani kuu.
Na ipo ili nawe uipate pia.
Imeonekana: Lulu ya Thamani Kubwa Sana
Mwisho wa yote, Mfano wa Lulu ya Thamani Kubwa Sana unahusu thamani ya watu wa Mungu na thamani ya ufalme wa mbinguni. Kwa Mungu, sisi ni vito vya thamani isiyo na kipimo. Na alimtuma Yesu kutukomboa kutoka katika dunia ya dhambi kwa gharama isiyoweza kufikirika kwake Mwenyewe.
Lulu ya Thamani Kubwa Sana pia inahusu kutafuta ukweli, kukubali wokovu, na kujisalimisha kwa Yesu, tukiamini kwamba Atatuongoza na kututunza.
Na jambo bora zaidi ni kwamba, ingawa Lulu hii ina thamani kuu, si vigumu kuipata:
- Fungua moyo wako kwa Mungu katika sala. Wakati wowote, mahali popote.
- Mwambie Yesu unataka kukubali zawadi Yake ya wokovu.
- Mwombe akusaidie kujisalimisha kwa kile chochote kinachoweza kukuzuia.
- Mruhusu Roho Mtakatifu akubadilishe na kukuongoza.
- Tafuta ushirika wa Kikristo, kama vile kujiunga na masomo ya Biblia.
- Soma Neno la Mungu kila siku ili uendelee kukua katika Kristo.
Unataka kusoma hadithi nyingine zinazofafanua kuhusu ufalme wa mbinguni?
Makala Zinazohusiana
- Wahlen, Clinton, PhD, “Lessons from Matthew 13,” Biblical Research Institute. [↵]
- Smith, William LLD, Nelson’s Quick Reference Bible Dictionary (1993), pp. 494-495. [↵]
- Nichol, Francis D., “Matthew” The Seventh-day Adventist Bible Commentary, Vol. 5 (1956), p. 411. [↵]
- Nichol, Francis D., “Matthew,” The Seventh-day Adventist Bible Commentary, Vol.5 p. 411. [↵]
Majibu Zaidi
Mfano wa Yesu wa Mpanzi Unahusu Nini?
Mfano wa mpanzi hatimaye unahusu jinsi watu walivyompokea kwa Yesu Kristo na ujumbe Wake wa ufalme wa Mungu—Injili.
Mfano wa Vazi na Viriba Unahusu Nini Hasa?
Kutumia mbinu ya kufikiria ya zamani kufanya kitu ambacho awali hakijawahi kufanywa mara nyingi haina maana.
Kuelewa Mfano wa Kondoo Aliyepotea
Kuelewa Mfano wa Kondoo AliyepoteaMifano ya Yesu inafundisha kwa vielelezo kuhusu ufalme wa Mungu. Na mifano mitatu maalum, Mfano wa Kondoo Aliyepotea, Mfano wa Sarafu Iliyopotea, na Mfano wa Mwana Mpotevu, hususan hufundisha kuhusu upendo wa Mungu usio na masharti...
Hadithi ya Mwana Mpotevu Kweli Inamaanisha Nini?
Hadithi ya Mwana Mpotevu inaeleza kisa cha mwana aliye mbali na familia, kaka mwenye wivu, na baba mwenye upendo usio na masharti. Tuchunguze tunachoweza kujifunza kutoka kwake leo.







