Ukitembelea ibada ya Kanisa la Waadventista wa Sabato, unaweza kugundua kwamba watu wengi hawavai hereni, bangili, mikufu, au wakati mwingine hata pete za ndoa. Ni jambo la kawaida katika jamii za Waadventista kutochagua mapambo ya nje, mara nyingi wakirejelea kanuni iliyo katika 1 Petro 3:3-4, ambayo inatuonya tusiruhusu mapambo ya nje kuwa chanzo cha uzuri au mvuto wetu.
Hata hivyo, hii sio sheria au kiwango cha dhehebu, na Waadventista kadhaa huchagua kuvaa vito au vitu vingine vinavyoweza kuchukuliwa kama mapambo. Hakika sio swala la wokovu au jinsi mtu alivyo “mtakatifu,” na sio sharti la ushirika wa kanisa.
Lakini msisitizo huu wa pamoja juu ya kiasi ulitoka wapi? Kwa nini lilikuwa swala muhimu katika siku za mwanzo za dhehebu, na je, msisitizo huo ni sawa na uliopo leo?
Hebu tupate majibu ya maswali haya na pia tuone Maandiko yanasema nini. Tutaangalia:
- Kwa nini kuna msisitizo upi juu ya kupunguza mapambo, hasa vito?
- Biblia inasema nini kuhusu kuvaa vito
- Je, Wasabato wanaamini kuvaa vito ni dhambi?
Tutaanza na historia na maelezo ya msingi.
Nini kilicho nyuma ya msisitizo wa pamoja wa Waadventista juu ya kupunguza mapambo ya nje?

Photo by Tamara Bellis on Unsplash
Wakati Kanisa la Waadventista lilipoanzishwa katika miaka ya 1800, viongozi wengi wa kanisa walikuwa na wasiwasi kuhusu athari za baadhi ya mitindo ya jamii ya wakati huo. Moja ya mitindo hiyo ilikuwa ni kupenda sana vito vya thamani na mavazi ya gharama kubwa.
Katika enzi ya Victoria, tofauti kati ya tabaka la juu la matajiri na “watu wa kawaida” ilionekana sio tu kwa kazi, eneo, au nasaba, bali pia kwa jinsi watu walivyopamba muonekano wao wa nje. Mtazamo huu wa anasa wa jamii ya wakati huo ulileta wasiwasi kuhusu athari zake kiroho, hasa ikizingatiwa jinsi Maandiko yanavyoonya dhidi ya kiburi, uroho, kupenda mali, na mambo mengine yanayoweza kuhusishwa na mapambo ya kupita kiasi.1
Basi hebu tuzungumze kuhusu mapambo ya nje.
Nini hufanya kitu kiitwe “mapambo”? Kwa mujibu wa Kamusi ya Collins, mapambo ni “kitu kinachotumiwa kumfanya mtu au kitu kuwa mzuri zaidi.”2
Vito mara nyingi vinahusishwa na mapambo kwa sababu ni wazi kuwa ni kitu cha ziada, badala ya kitu chenye kazi maalum. Shati lina kazi ya kufunika kifua, wakati mkufu kazi yake ni kuongeza urembo wa ziada.
Mapambo yenyewe sio mabaya. Na kuna sehemu nyingi katika Maandiko ambapo yanatajwa kwa namna ya kawaida, au hata kwa mtazamo mzuri.3
Lakini kama mambo mengine mengi, tukijishughulisha sana nayo, inaweza kupelekea kiburi.
Au tunaanza kupata thamani yetu kutokana na mambo yanayotuhusu sisi ambayo yanapaswa kuwa “ya ziada.”
Kuzingatia mali zetu zote kunaweza kutufanya tuhisi kwamba vitu hivyo vinatusaidia kuendana na wengine au kujitofautisha, au kuonyesha kiasi cha pesa tulicho nacho, au kutupatia umakini au thamani binafsi tunayoona kuwa tunaikosa. Vitu hivi hutupotosha kutoka kwenye mambo muhimu zaidi maishani: utambulisho wetu kila mmoja kama mtoto wa kipekee wa Mungu, na uhusiano wetu Naye kama Muumba wetu mwenye upendo.
Ndiyo maana mara nyingi tunasikia kuhusu kiburi kinachotokana na mali kuwa mtego rahisi kuingia ikiwa tutazingatia sana mapambo ya nje.
Biblia inatuonya kuhusu tatizo la kupenda mali katika sehemu kadhaa. Yesu aliwashauri Wayahudi “Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo” (Luka 12:15, SUV).4 “Vitu” ni vizuri, lakini sio kila kitu. Watu na mahusiano ni muhimu zaidi.
Na Mfalme Sulemani alijua jinsi kupenda mali kulivyo hatari alipoyaandika maneno haya katika Mithali:
“Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; Na neema kuliko fedha na dhahabu” (Mithali 22:1, SUV).
Maneno yake yana nguvu kwa sababu tunajua alizungumza kutokana na uzoefu. Alikuwa amejishughulisha sana na utajiri wake na kila kitu kilichokuja nao, kiasi kwamba kwa muda, alitengana na Mungu na akajiachilia kushawishiwa na kila kitu kilichomjaribu. Ni baada tu ya kunyenyekezwa ndipo macho yake yalifunguliwa na akaona jinsi ilivyokuwa bure kukimbilia mali.
Na 1 Timotheo 6:7-8 inatukumbusha,
“Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo” (SUV).
Lakini jambo baya zaidi kuhusu ulimwengu wa mali ni uhusiano wake na kiburi. Badala ya kutambua mambo mema kama zawadi kutoka kwa Mungu, ni rahisi kuona utajiri na mali tulizokusanya kama ishara ya thamani au nguvu zetu wenyewe. Tunajikuta tukizingatia uwezo wetu wenyewe, badala ya wa Mungu.
Badala yake, Biblia inasisitiza unyenyekevu na kujishusha (Zaburi 25:9; 1 Petro 5:5; Yakobo 4:6-7).
(Na kwa kawaida, mtu mnyenyekevu anavutia zaidi kuishi naye kuliko mtu mwenye kiburi!)
Lakini pamoja na tabia hizi za msingi za asili ya mwanadamu aliyeanguka, kulikuwa na sababu zaidi nyuma ya msisitizo wa Waadventista wa kwanza kuhusu mapambo kupitia vito na mitindo ya mavazi.
Historia ya kitamaduni
Katika miaka ya 1800, wakati Kanisa la Waadventista Wasabato lilipoanzishwa, ikiwa watu walivaa vito, mara nyingi ilikuwa kuonyesha utajiri wao.5 Ilikuwa ni ishara ya makusudi ya hadhi.
Na kadiri vito vilivyokuwa vya kung’aa au vya gharama kubwa zaidi, ndivyo “heshima” na kutambuliwa zaidi ilivyotarajiwa kutoka kwa wengine.
Makanisa mengi ya Kikristo tayari yalikuwa yanakataza uvaaji wa vito—pamoja na mapambo mengine yasiyo ya lazima kama renda, utepe, mikufu, na makoti na kofia za bei ghali—kabla hata Kanisa la Waadventista kuanzishwa.6 Hivyo viongozi na watu wenye ushawishi katika Waadventista wa awali, ambao walitoka katika makanisa haya, tayari walikuwa na mtazamo huu. Walitambua hili kama lango la kawaida la kiburi, kwa kuwa ilikuwa njia inayoonekana wazi na ya hadharani kutangaza utajiri wa mtu.
Hata hivyo, Maandiko yanatahadharisha vikali kwamba kuzingatia utajiri kunaweza kuwa kikwazo kikubwa kwa imani na afya ya kiroho.
“Ni rahisi ngamia kupenya katika tundu ya sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu” (Marko 10:25, SUV).

Photo by Sandy Millar on Unsplash
Ili kukabiliana na hili, Waadventista wa kwanza walihimiza washiriki wa kanisa kuvaa kwa unyenyekevu na kwa kiasi. Na hili halikuletwa kama sheria, bali kama ushauri wa kiroho.
Hii ilijumuisha vito, isipokuwa kama vilikuwa na kusudi au matumizi ya vitendo. Ellen G. White, mmoja wa waanzilishi wa kanisa letu, aliwahi kupewa kipande cha vito, na alikivaa kwa sababu kilikuwa kizuri lakini kisicho onyesha fahari, na pia kilitumika kama kifungo kwenye gauni lake.7
Kwa mfano, Waadventista wengi wakati huo na hata leo huchagua kuvaa pete za ndoa, ingawa wapo wengi wanaochagua kutovaa. Lakini ingawa ni “vito,” zinatumika kama ishara ya upendo na ndoa. Pia zinaonyesha kwa watu wengine kwamba mtu yuko kwenye uhusiano wa kujitolea, jambo ambalo husaidia kuzuia usumbufu usiotakiwa.
Kwa Waadventista, vito pia vina uhusiano na uwakili. Uwakili unahusu jukumu ambalo Mungu anatupatia la kutunza kanisa Lake, dunia, watu, n.k. Hii inajumuisha kusimamia fedha zako vizuri. Kununua vito ili kuonyesha utajiri wako badala ya kuweka akiba au kutumia fedha hizo kwa kitu muhimu zaidi mara nyingi siyo uwakili mzuri.
Lakini ili kufikia kiini cha kanuni hizi na maamuzi ambayo Waadventista wamefanya kuhusu vito na mapambo ya nje, hebu tuangalie kile Maandiko yanachosema.
Kile Biblia inachosema kuhusu kuvaa vito
Biblia inataja mapambo, unyenyekevu, na mambo mengine yanayohusiana katika sehemu kadhaa, katika Agano la Kale na Agano Jipya. Hapa kuna aya chache zinazohusishwa zaidi na jambo hili.
1 Timotheo 2:9
Andiko hili linasema:
“Vivyo hivyo wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi; si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za thamani” (1 Timotheo 2:9, SUV).
Hapa, Mtume Paulo anashauri watu wavae kwa kiasi, wakiepuka mitindo ya ajabu na mavazi au vito vya thamani isiyo ya lazima. Angalia msisitizo juu ya “heshima na busara” kama sifa za kuigwa linapokuja swala la muonekano wa nje.
Leo, kanuni hii ina maana ile ile. Inatuhimiza kuvaa kwa kiasi na kuepuka maonyesho ya kiburi ya utajiri. Hii inaenda sambamba na 1 Petro 3:3-4.
Waadventista, katika jitihada za kufuata kanuni za andiko hili, kwa kawaida huepuka kuvaa vito kwa sababu ni rahisi kuzidisha kwa vitu vinavyong’aa au vya gharama kubwa.
Isaya 3:18-20
Aya hii inasema,
“Siku hiyo BWANA atawaondolea uzuri wa njuga zao, na kaya zao; na pete za masikio, na vikuku, na taji zao; na dusumali, na mafurungu, na vitambi, na vibweta vya marashi, na matalasimu” (Isaya 3:18-20, SUV).
Ingawa aya hizi zinaonekana kama zinazungumzia vitu maalum ambavyo watu hawapaswi kuvaa, muktadha ni muhimu ili kutoa maana kamili ya aya hizi.
Vifaa vingi vya vito vilivyotajwa katika aya hii vilivaliwa na Waisraeli wa tabaka la juu, wenye kiburi ambao walikuwa wakiwatendea maskini vibaya.
Kwa kutaja vito hivyo, Isaya alielezea tabaka la juu na kutabiri jinsi Mungu angewashusha kwa ajili ya udhalimu wao.8
Isaya hakuwa anasema kwamba vito vyenyewe vilikuwa vibaya, alikuwa anaelezea watu waliokuwa wakitenda visivyo, na jinsi vito hivyo vilivyoonyesha vipaumbele vyao.
Mwanzo 35:2-4

Photo by Yuliya Yevseyeva on Unsplash
Sio muda mrefu kabla ya Yakobo kuitwa Israeli, aliwaambia watu wa nyumbani mwake waondoe sanamu zao, wabadili mavazi yao, na wajitakase.
“Nao wakampa Yakobo miungu migeni yote iliyokuwa mikononi mwao, na pete zilizokuwa masikioni mwao, naye Yakobo akazificha chini ya mwaloni ulioko Shekemu” (Mwanzo 35:4, SUV).
Hebu tuangalie muktadha ili tuone kwa nini pete za masikio zilitajwa maalum, na si bangili au mikufu.
Ni muhimu kuelewa utamaduni. Kama vile maelezo mengi ya Biblia yanavyopendekeza, pete za masikio wakati huo zilitumika kama hirizi na mara nyingi zilikuwa zimechorwa picha za miungu ya kipagani na maneno ya ajabu.9
Pete za masikio pia zilionyesha cheo au hadhi katika jamii—jambo ambalo lingeweza kusababisha kiburi.10
Tabia hizi za kipagani na za kiburi ndizo sababu Mungu alimwambia Yakobo aziondoe. Sio kwamba pete za masikio zilikuwa zisizo na haya au mbaya zenyewe, bali kwa sababu ya kile zilichowakilisha kitamaduni.
Mwanzo 24:47-48
Maelezo haya kuhusu vito hutokea wakati mtumishi wa Ibrahimu anasafiri kwenda mji wa Nahori kutafuta mke kwa ajili ya Isaka. Kupitia uongozi wa Mungu, anampata Rebeka.
“Kisha nikamwuliza nikasema, U binti wa nani wewe? Naye akasema, Mimi ni binti Bethueli, mwana wa Nahori, Milka aliyemzalia. Nami nikamtia hazama puani mwake na vikuku mikononi mwake” (Mwanzo 24:47, SUV).
Aya hii haina maana yoyote mbaya kuhusu vito.
Katika utamaduni huo wakati huo—na hata leo—pete za puani na vikuku vilikuwa mapambo ya kawaida ya kila siku.11 Havikuchukuliwa kama alama za kiburi kama vile aya nyingine zinavyopendekeza katika tamaduni za Waisraeli na Warumi-Wakristo.
Zawadi hizi zilitolewa kwa Rebeka kwa ajili ya wema au labda kama zawadi ya uchumba, na kwa idhini ya Mungu (Mwanzo 24:12, 26-27).
Zawadi hii ya pete ya puani inapatikana sehemu nyingine katika Biblia, kama vile Ezekieli 16:12. Katika aya hii, Mungu kwa mfano anaweka pete ya puani Yerusalemu, ambayo inawakilisha mke wake. Ilikuwa na maana ya kuonyesha uhusiano wake nao.
Hata hivyo, aya chache baadaye, Ezekieli anaonyesha kile kinachoweza kutokea mapambo yanapokuwa kitovu cha uzuri au hadhi. Anasema kwamba Yerusalemu “uliutumainia uzuri wako” na akawa kahaba wa kiroho (Ezekieli 16:15).
Aya zote katika Mwanzo na Ezekieli zinazozungumzia zawadi ya pete ya puani lazima zichukuliwe katika muktadha wa utamaduni na wakati ule. Inaweza kuwakilisha mambo tofauti katika tamaduni za leo. Ni vyema kutumia busara yetu na kujitahidi kuwa wanyenyekevu na wapole, tukitamani kuwa wasimamizi wema wa kile ambacho Mungu ametupa katika maisha yetu.
Kwa ujumla, aya hizi zote zinatuonyesha nini kuhusu vito? Zinatuhimiza kufikiria kwa makini kuhusu nia zetu. Kama ilivyotajwa awali, ni vizuri kujiuliza, kwa nini tunavaa vito?
Hatimaye, hatutaki mwonekano wa nje wa vito vyetu utupotoshe sisi au wengine kutoka kwa Mungu na kanuni Zake. Haiwezi kupingwa kwamba kile tunachovaa kinaweza kutuma ujumbe kwa wengine. Vito na mavazi mengine ya anasa vinaweza kutuma ujumbe usio sahihi, hata bila kukusudia.
Na hili linahusu mambo mengine zaidi ya vito pia, bila shaka. Kujipamba kupita kiasi kunaweza kutokea kwenye nyumba zetu, magari yetu, au vitu vingine vingi ambavyo havihitajiki au ni vya ziada. Tunaweza hata kujionyesha kwa mafanikio yetu au vyeo kama njia ya kupamba jinsi tunavyoonekana, tukijaribu kuongoza jinsi wengine wanavyotufikiria.
Jambo la msingi ni kwamba, kile tunachopamba na jinsi tunavyopamba vitu vinaweza kuonyesha vipaumbele vyetu. Na kama tunainua mambo ya kidunia na kuyapa umuhimu zaidi kuliko Mungu na uhusiano wetu Naye, ni wakati wa kujichunguza. Vinginevyo, tunahatarisha kuwa kama “kijana tajiri” aliyeandikwa katika Mathayo 19:16-22.
Lakini tukirudi kwenye vito—kwa kuwa Waadventista wengi hawavivai, je, wanaviona kama dhambi?
Je, Waadventista wanaamini kuvaa vito ni dhambi?

Photo by Maddi Bazzocco on Unsplash
Hapana kabisa. Ingawa Waadventista wanashauri kutovaa vito, hatuoni kama ni dhambi, na hakuna Mwadventista au kanisa la Waadventista linapaswa kukusumbua kuhusu hilo.
Makanisa mengine yanaweza kuwa na mitazamo tofauti kuhusu vito, lakini haipaswi kuwa swala la ushirika, wokovu, au kukubalika kwa ujumla.
Na baadhi ya watu katika makanisa fulani wanaweza kukushinikiza uvue, lakini hili sio jambo linalofaa, na usihisi kwamba lazima ufanye kama wanavyosema. Waadventista wengi huvaa vito, na kuvaa au kutovaa hakubadilishi uwezo wako wa kuokolewa au kupendwa na kutumiwa na Mungu.
Ni uamuzi binafsi tunaofanya na Mungu. Daima unaweza kuzungumza na mchungaji au mzee wa kanisa ikiwa una maswali.
Wakati pekee ambapo vito vinaweza kuwa tatizo ni, kama ilivyoelezwa awali, pale vinapokuwa kikwazo katika uhusiano wako na Mungu.
Na huo uhusiano ndio jambo la muhimu zaidi.
Yesu alitoa ushauri mzuri aliposema,
“Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako” (Mathayo 6:19-21, SUV).
Mambo ya duniani yanaweza kuwa ya kuvutia na kufurahisha. Na hilo halimaanishi kwamba yote ni mabaya. Lakini ni muhimu tukumbuke kwamba mwishowe, hayana umuhimu. Hayalingani kabisa na yale Mungu aliyotuandalia mbinguni na katika Dunia Mpya (1 Wakorintho 2:9).
Kurasa Zinazohusiana
- Matthew 19:24; Luke 12:15; 1 Timothy 2:9-10; 6:10; Isaiah 3:16-24; 1 Peter 3:3-4 [↵]
- “Adornment,” Collins Dictionary, [↵]
- Exodus 28:20; 2 Chronicles 3:6; Job 40:10; Psalm 93:5; Proverbs 3:22; Isaiah 61:10; Matthew 6:29; Luke 12:27; Titus 2:10 [↵]
- 1 Timothy 6:7-8, Luke 12:15, Proverbs 22:1. [↵]
- Lasiter, Lyndon, “Victorian Era Jewelry: Style and Characteristics,” M. S. Rau, [↵]
- Braun, Dennis H., “A Seminar on Adventists, Adornment, and Jewelry,” Andrews University, p. 25, [↵]
- Braun, Dennis H., “A Seminar on Adventists, Adornment, and Jewelry,” p. 43. [↵]
- Braun, Dennis H., “A Seminar on Adventists, Adornment, and Jewelry,” p16. [↵]
- “Genesis 35:4,” Bible Hub, [↵]
- “The Ancient and Fascinating Origin of Earrings,” Noe’s Jewelry, May 20, 2016, [↵]
- “Genesis 24:22,” Bible Hub, [↵]
Majibu Zaidi
Vilabu vya Wavumbuzi na Watafuta Njia ni Nini?
Vilabu vya Wavumbuzi na Watafuta Njia ni Nini?Kama ilivyo kwa skauti wa kiume au wa kike, Watafuta njia na Wavumbuzi hujifunza kuhusu asili na ujuzi wa maisha. Lakini kinachofanya vilabu hivi kuwa maalum ni lengo lao la kuwavuta vijana karibu zaidi na Yesu. Ikiwa...
Tazama Vyuo na Vyuo Vikuu vya Kiadventista
Kwa nje, vyuo vikuu vya Waadventista wa Sabato vinaweza visionekane tofauti sana na vyuo vingine. Lakini tofauti halisi ziko nyuma ya pazia.
Jinsi Waadventista Wanavyoutazama Mwisho wa Dunia
Mwisho wa dunia sio jambo la kufurahisha kufikiria. Lakini hivi ndivyo tunavyoweza kupata tumaini na faraja katika yanayokuja.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria” Kuhusu Kampuni za Nguo?
Dini nyingi zina mwongozo kuhusu mavazi, lakini je, Kanisa la Waadventista wa Sabato lina maoni gani? Gundua jinsi Waadventista wanavyochagua mavazi kulingana na kanuni za Kibiblia.
Mkutano wa Kambi wa Waadventista wa Sabato ni Nini?
Ingawa mikutano ya kambi haikuanza na Kanisa la Waadventista wa Sabato, ni jambo la msingi sana katika utamaduni wa Waadventista.
Ukweli wa Sasa—Ni Nini na Kwa Nini ni Muhimu
Ukweli wa sasa, kulingana na Waadventista wa Sabato, ni imani kwamba ukweli fulani wa Biblia ni muhimu kwa watu wa Mungu katika nyakati maalum katika historia.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria” Za Ndoa?
Dini nyingi au tamaduni ulimwenguni zina mila, taratibu, au matarajio ya kipekee katika ndoa au sherehe ya harusi.
Viongozi wa Kanisa: Ni Nini Majukumu ya Mchungaji wa Kiadventista?
Wachungaji – tumesikia juu yao, lakini wanafanya nini hasa? Hebu tuangalie nafasi ya mchungaji wa Kiadventista katika kanisa.
Biblia Inasema Nini Kuhusu Staha na Adabu?
Biblia inafundisha kwamba adabu, aina ya unyenyekevu na heshima, ni sifa yenye thamani kwa kila mtu—wanaume, wanawake na watoto.
Muhtasari wa Elimu ya Juu ya WaAdventista wa Sabato
Muhtasari wa Vyuo Vikuu Vya Waadventista wa SabatoKanisa la WaAdventista Wasabato lina takribani shule za sekondari 118 ulimwenguni kote.1 Ingawa nyingi zipo ndani ya Amerika Kaskazini, pia utapata vyuo vikuu vya WaAdventista katika nchi mbalimbali duniani—mahali kama...
Waadventista Wasabato Wanatafsiri Vipi Unabii wa Biblia?
Jifunze zaidi kuhusu jinsi Waadventista wanavyotafsiri unabii katika Biblia—hasa katika vitabu kama Danieli na Ufunuo.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria”?
Tunashikilia kanuni tunazoamini zitasaidia kuweka uhusiano wa karibu na Yesu na Neno lake. Jifunze jinsi kanuni hizi zinavyo-ongoza mtindo wa maisha wa Waadventista.
Jinsi Waadventista Wanavyoshughulikia Kifo na Mazishi
Mazishi mengi ya Waadventista wa Sabato yanafanana na yale ya madhehebu mengine ya Kiprotestanti, kama vile Wamethodisti, Wabatisti, au Wapresbiteri, lakini unaweza kupata tofauti chache au taratibu za pekee.
Filamu za Kiadventista: Mahali Imani na Filamu Zinapokutana
Tangu mwanzo, lengo la Kanisa la Waadventista wa Sabato limekuwa kueneza kweli ya Mungu katika Biblia.
Ni nini Mtaalam wa Matibabu wa Kiadventista?
Mmishonari wa matibabu katika Kanisa la Waadventista ni mtu anayejali mahitaji ya matibabu ya watu kama njia ya kuonyesha upendo wa Yesu.
Je, Waadventista Wasabato Wanasherehekea Siku Kuu Zinazohusiana na Pasaka?
Kufufuka kwa Yesu, kunakoadhimishwa katika siku kuu nyingi zinazohusiana na Pasaka, ni muhimu katika imani za Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Chakula cha Pamoja Katika Kanisa la Kiadventista: Mahali Ambapo Chakula na Urafiki Vinakutana
Mara nyingi, kawaida kwenye ratiba inayotofautiana kutoka mara moja kwa wiki hadi mara moja kwa mwezi hadi mara moja kwa robo, kanisa la Waadventista litakuwa na “karamu za ushirika,” mara nyingi zikiitwa chakula cha mchana cha pamoja.
Je, Mahubiri ya Waadventista wa Sabato Yako Namna Gani?
Karibu katika kila Kanisa la Waadventista wa Sabato, mahubiri ndiyo kitovu cha ibada kuu—kama ilivyo kwa madhehebu mengi ya Kikristo ya Kiprotestanti.
Wasimamizi wa Waumini Wana Nafasi Gani Ikilinganshwa na Wachungaji?
Neno “Usimamizi wa kidini” linatokana na neno la Kigiriki laikos, ambalo maana yake ni “wa watu.”
Muundo wa Uongozi wa Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Kanisa la Waadventista wa Sabato lina mfumo wa uwakilishi unaounganisha makanisa yake zaidi ya 90,000 ulimwenguni na kuwapa washiriki wake nafasi katika kufanya maamuzi.
Kitabu cha Nyimbo cha Waadventista Wa Sabato
Kitabu cha nyimbo cha Waadventista wa Sabato ni kitabu cha nyimbo kinachotumiwa ulimwenguni kote na makanisa mengi ya Waadventista wakati wa ibada zao.























