Ikiwa umeona jinsi vyombo vya habari vinavyo onyesha mwisho wa dunia, kauli hii inaweza kukufanya uwe na wasiwasi—au hata uogope kabisa.
Hata bila picha za akilini kutoka kwenye filamu au televisheni, wazo la dunia kuisha bado linaonekana la kutisha. Kila hadithi ya kusikitisha tunayosikia kuhusu vita, uonevu, ufisadi, au maafa inaongeza tu wasiwasi wetu wa pamoja.
Na hilo linaeleweka. Hii ndiyo kila kitu tunachojua—ni vigumu hata kufikiria kwamba maisha haya, pamoja na machafuko yake yote, yanaweza kufikia mwisho wake wakati fulani.
Kwa bahati nzuri, mtazamo wa Kanisa la Waadventista wa Sabato kuhusu mada hii unaleta tumaini katikati ya dunia inayohisi kama inazidi kupoteza mwelekeo. Tunategemea uhakikisho wa Biblia kwamba uovu huu wote hautaendelea milele. Yesu Kristo atarudi, na Ataumba upya dunia hii ili iweze kuakisi ukamilifu wake wa asili, kama ilivyokuwa katika Bustani ya Edeni (Mwanzo 1-2).
Lakini tunapaswa kufanya nini sasa?
Waadventista kihistoria wameweka kipaumbele katika kujifunza unabii wa Biblia, na unabii huo unatueleza mambo gani yatatokea kabla ya kurudi kwa Yesu. Hii inatuwezesha kuandaa mioyo yetu na kumtumainia Mungu atuongoze. Hivyo basi, hebu tuangalie kwa karibu kile ambacho Maandiko yanasema, na jinsi tunavyoweza kupata amani ya kina katika maneno hayo.
Haya ni baadhi ya maswali muhimu tutakayojibu:
Waadventista wanaamini nini kuhusu mwisho wa dunia?

Image by sudhanshuamazingboy from Pixabay
Waadventista wanautazama mwisho wa wakati kupitia lenzi ya kibiblia, wakitazamia tumaini letu kuu—Kurudi kwa Pili kwa Kristo. Hili limeelezwa katika Misingi yetu ya Imani 25.
Tumaini hili limejikita sana, kwani lilikuwa sehemu ya mizizi yetu kama kanisa. Harakati ya Waadventista ilianza na watu waliotafuta Maandiko na kutambua umuhimu wa kumtafuta Mungu na kujiandaa kwa ukweli kwamba dunia hii, ilivyo sasa, iko karibu na mwisho wake. Wasisi wetu wa kwanza walimngojea Yesu kwa hamu arudi katika miaka ya 1800, ingawa hawakuelewa vizuri wakati ambao hili lingetokea.
Baadaye, baada ya kujifunza zaidi Maandiko, waligundua kwamba matukio mengine katika unabii wa Biblia bado yanapaswa kutokea kabla ya Yesu kurudi—na kwamba hakuna yeyote isipokuwa Mungu Mwenyewe anayejua hasa siku hiyo itakuwa lini.
Na, ndiyo, kutakuwa na nyakati za changamoto tunapokaribia mwisho wa dunia. Yesu Mwenyewe alizungumza kuhusu vita, migogoro, majanga ya asili, na ukosefu wa upendo na huruma kwa ujumla, pamoja na dalili nyingine, ambazo zitafikia kilele katika kuja Kwake (Mathayo 24, Luka 21). Siku za mwisho na mwisho wa dunia ni kilele cha dhambi ambayo imekuwa ikifuata mkondo wake wa asili katika ubinadamu.
Lakini mwishoni mwa dunia, Shetani (ibilisi) atafanya kazi kwa bidii zaidi kuliko wakati mwingine wowote ili kuleta uharibifu kwa sababu anajua muda wake ni mfupi (1 Petro 5:8; Ufunuo 12:12).
Unabii wa Ufunuo 12 na 13 unatudokeza kuhusu mgogoro wa ibada ambao utatokea wakati huo. Ibilisi atajaribu kuwapinga na kuwadanganya watu wa Mungu (Ufunuo 12:17), jambo ambalo hatimaye litasababisha kila mtu duniani kufanya uamuzi wa mara moja na wa mwisho wa kubaki mwaminifu kwa Mungu au kukubali udanganyifu wa ibilisi (Ufunuo 13).
Tunatambua jinsi haya yote yanavyoweza kuogopesha na kutia wasiwasi. Lakini Mungu hatupi maonyo haya katika Maandiko ili kututisha. Badala yake, anataka tuwe na ufahamu wa kile kinachokuja ili tusilazimike kuogopa. Na anatualika tumkaribie na kupata faraja katika yale yaliyo zaidi ya mambo haya magumu.
Ingawa watu mara nyingi huzingatia matukio mabaya yatakayotokea mwisho wa dunia, Biblia inasisitiza kinyume chake: inajikita zaidi kwenye ushindi wa Yesu na watu Wake na furaha tutakayokuwa nayo wakati wanadamu watakapounganishwa tena na utimilifu wa Mungu, na sote tutaishi katika dunia mpya nzuri—milele (2 Petro 3:13).
Mwisho wa dunia hii ni sehemu ndogo tu ya muda ukilinganisha na umilele.
Basi, ni matukio gani yanayounda kipindi hicho cha muda?
Ni matukio gani yatakayotokea kabla ya mwisho wa dunia?

Photo by sudhanshuamazingboy
Kwa madhumuni ya ukurasa huu, tutazingatia matukio makuu yatakayotokea kabla tu ya Kurudi kwa Pili kwa Kristo, kisha hadi uumbaji upya wa dunia. Tutajumuisha:
- Mgogoro wa chapa ya mnyama
- Kufungwa kwa mlango wa rehema
- Wakati wa taabu na mapigo saba ya mwisho
- Ujio wa Pili wa Kristo
- Miaka elfu moja (Millenia)
- Uangamizi wa waovu
- Uumbaji upya wa dunia
Ili kujua zaidi kuhusu matukio yanayotangulia haya ya mwisho, angalia ukurasa wetu wa kina kuhusu dalili na matukio yanayo ashiria jinsi tulivyo karibu na mwisho wa historia ya dunia.
Mgogoro wa chapa ya mnyama
Kitabu cha Ufunuo kinaonya dhidi ya kumwabudu mnyama na kupokea chapa ya mnyama katika siku za mwisho. Kwa kweli, sura za 13 na 14 zinatusaidia kuelewa kwamba kutakuwa na mgogoro wa ibada wakati huo. Wanadamu wote watakabiliwa na uchaguzi wa kuabudu Mungu au kuabudu kile ambacho wanadamu wameweka.
Je, mnyama na chapa yake vina uhusiano gani?
Tumezungumzia yote haya katika makala tofauti kuhusu chapa ya mnyama, lakini kwa muhtasari, “mnyama” katika Biblia anawakilisha mamlaka ya kidini-kisiasa. Mnyama huyu katika Ufunuo atatafuta uaminifu wa wanadamu, jambo ambalo litawafanya watu waache uaminifu kwa Mungu kama Mtawala. “Chapa,” basi, inawakilisha uchaguzi wa kuabudu mamlaka hii ya mnyama badala ya kupokea muhuri wa Mungu, ishara ya ndani ya utii kwake.
Mgogoro huu utafikia kilele, na kila mtu ataonyesha anayemwabudu. Wakati huu, kila mtu atajua kama amemkubali au amemkataa Mungu—na hili linatupeleka kwenye tukio linalofuata.
Kufungwa kwa mlango wa rehema
Kufungwa kwa mlango wa rehema kunarejelea wakati ambapo kila mtu duniani atakuwa ameamua kwa ajili au dhidi ya Mungu. Wakati huu, Hukumu ya Upelelezi, ambayo hufanyika katika patakatifu pa mbinguni kabla ya Ujio wa Pili wa Kristo (Danieli 7:9-10, 13-14), itakuwa imekamilika.
Hivyo basi, wakati huu hauhusiani na tendo la Mungu bali unasababishwa na wanadamu.
Biblia inaita uamuzi wa kumkataa Mungu kuwa ni “kufuru dhidi ya Roho Mtakatifu” (Marko 3:29, SUV). Hii hutokea mtu anapolikataa ombi la Mungu kwa muda mrefu kiasi kwamba moyo wake unakuwa mgumu dhidi ya Roho Mtakatifu (jambo ambalo Waebrania 4:7 linawaonya watu wa Mungu kuhusu hilo).
Lakini kutakuja wakati katika historia ambapo kila mtu atafanya uamuzi wake wa mwisho—iwe ataendelea kuufungua moyo wake kwa Roho Mtakatifu au kuwa mgumu kabisa.
Kwa ajili ya mfano, tunaweza kulinganisha na kumwalika rafiki yako nyumbani kwako kwa ajili ya karamu ya chakula cha jioni.
Unamwalika, na hupati jibu. Unaweza kumkumbusha mara moja au mbili, ili kuhakikisha anajua amealikwa.
Na kama akikataa mwaliko wako, unaweza kumsisitiza kidogo. Lakini mwishowe, unaheshimu uamuzi wake. Kwa kawaida hatuoni umuhimu wa kuwasumbua watu ambao tayari wameonyesha nia yao.
Kwa bahati nzuri, Mungu ni mvumilivu zaidi kwetu! Anatuhimiza na kutualika mara nyingi sana. Lakini mwishowe, lazima aheshimu chaguzi zetu, hata kama zinamuumiza.
Wakati wa taabu na mapigo saba ya mwisho

Photo by Алесь Усцінаў
Biblia inazungumzia wakati wa mateso na shida ambao utatokea kabla tu ya Kurudi kwa Pili kwa Kristo. Ufunuo 7:14 unaashiria hili kwa kutaja kwamba watu wa Mungu watatoka katika “dhiki kuu” (SUV). Kitabu cha Danieli kinarejelea wakati huu wa taabu kwa uwazi zaidi (12:1-2).
Wakati huu wa taabu utahitimisha vita vyote, migogoro, majanga ya asili, na uovu ambao umekuwa ukiongezeka kwa nguvu.
Wakati huo huo, Mungu atatuma hukumu—zijulikanazo kama mapigo saba ya mwisho—dhidi ya wale wanaochagua kupokea chapa ya mnyama (Ufunuo 15:1; 16).
Katikati ya nyakati hizi za ugumu, Mungu atawalinda wale waliobaki waaminifu Kwake, ambao wanangoja kwa hamu kurudi kwa Yesu.
Ujio wa Pili wa Kristo
Ujio wa Pili wa Kristo, wakati mwingine unaitwa Ujio wa Pili, ndicho kitu ambacho wafuasi wa Mungu wamekuwa wakingojea na kutamani. Hatimaye, tutamwona Yesu, kiini cha tumaini letu lote!
Biblia inafundisha kwamba watu wa Mungu hawatoweki duniani kwa unyakuo wa siri kabla ya wakati wa taabu. Badala yake, tumeambiwa kwamba tutamwona “Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi” (Mathayo 24:30, SUV).
Na Yesu atakapofunuka na tukio la utukufu la tarumbeta na malaika, wale waliokufa wakimwamini Kristo watafufuka. Wakati huo huo, wafuasi wa Kristo ambao bado wako hai duniani watanyakuliwa kwenda angani ili kuwa pamoja nao (1 Wakorintho 15:51-54; 1 Wathesalonike 4:16-17).
Wale waliomkataa Mungu watakufa kwa mwangaza wa uwepo wa Yesu wa kiungu, na watabaki makaburini mwao hadi baada ya milenia (Ufunuo 20:5). Hata hivyo, wafuasi wa Mungu watakuwa na jukumu maalum mbinguni wakati huu (Ufunuo 20:4).
Milenia
Milenia, neno la kifahari kwa miaka 1,000, linarejelea kipindi cha miaka 1,000 kati ya Kurudi kwa Pili kwa Yesu na maangamizi ya mwisho ya dhambi (Ufunuo 20:1-6).
Wakati huu, dunia itakuwa ukiwa (Yeremia 4:24-26), na wasio waadilifu watakuwa wamekufa. Shetani atakuwa “amefungwa”—asiyekuwa na uwezo wa kufanya kazi yake ya udanganyifu.
Wakati huo huo, wafuasi wa Mungu watakuwa mbinguni kama “makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu” (Ufunuo 20:6, SUV). Ufunuo 20:4 unatueleza kwamba “mamlaka ya kuhukumu” imekabidhiwa kwao, ikimaanisha kwamba nao watashiriki katika hukumu ya Mungu.
Kuangamizwa kwa waovu

Photo by Vladimir Shipitsin
Ufunuo 20 inasema kwamba mwishoni mwa milenia, waovu watafufuliwa na Shetani atajaribu kuwadanganya tena ili waishambulie Yerusalemu Mpya, ambao utakuwa umeshuka kutoka mbinguni (aya ya 7-8). Moto utashuka kutoka mbinguni na kuwateteketeza, na hivyo kuleta mwisho wa dhambi, ibilisi, malaika zake, na wote waliokumbatia dhambi na kumkataa Muumba wao Mungu.
Hatimaye, dunia itakuwa huru kutoka kwenye dhambi.
Kuumbwa tena kwa dunia
Mara tu dunia itakapokuwa imesafishwa kwa moto, haitabaki tupu. Wafuasi wa Mungu watapata nafasi ya kipekee kushuhudia Yeye akiiumba upya dunia na kuirudisha katika ukamilifu wa Edeni tena.
Itakuwa mahali pazuri—pasipo na mauti, maombolezo, kilio, maumivu, na mambo yote ya dhambi yaliyofanya maisha kuwa magumu hapa duniani hapo awali (Ufunuo 21:4).
Na kilicho bora zaidi, Mungu atakaa uso kwa uso na watu wake, na hatatengana nao tena milele (Ufunuo 21:3).
Je, dhana hizi zinaendana vipi na imani nyingine za Kiadventista?
Kwa Waadventista, mwisho wa dunia ni habari njema: Biblia inatuhakikishia kwamba mwishoni mwa dunia, tutaungana tena na Yesu, na vita kati ya mema na mabaya (inayoitwa Pambano Kuu), ambayo imekuwa ikiendelea tangu dhambi ilipoingia ulimwenguni mwetu, hatimaye itakoma. Yesu ni Mwokozi wetu sio tu kutoka katika nguvu za dhambi bali pia kutoka katika dunia ambayo dhambi ipo kila mahali.
Hatimaye, uovu na mateso yote yanayotuumiza sisi na kumuumiza Mungu yatakoma. Na tutapata furaha ya kuishi katika uwepo wa Mungu—kama vile Adamu na Hawa walivyofanya katika Bustani ya Edeni kabla ya kudanganywa.
Ingawa mwisho wa dunia unaweza kuonekana wa kutisha na mbaya, magumu na changamoto siyo lengo letu kuu. Hatupaswi kuogopa yatakayokuja kwa sababu, ikiwa tumemchagua Yesu, ameahidi kutulinda, kutufariji, na kututia nguvu. Magumu hayo yataonekana madogo sana ukilinganisha na mema yote yatakayokuja.
Kujua yatakayojiri mwisho wa dunia pia kunatutia moyo kuishi tukiwa tayari.
Hatujui hasa ni lini matukio haya yatatokea. Biblia inatuambia kwamba hatujui siku wala saa ya kuja kwa Yesu (Mathayo 24:36). Hii inamaanisha tunapaswa kuishi tukitarajia kwamba mambo haya yanaweza kuanza wakati wowote.
Na inatupa hamu ya kumtafuta Yesu na kutimiza wito wa kushiriki Injili ya milele ya Yesu, kama ilivyoelezwa katika Ufunuo 14.
Waadventista hujiandaaje kwa nyakati za mwisho?

Photo by Tima Miroshnichenko
Kujiandaa kwa ajili ya mwisho wa dunia hakuhusu “kujiandaa kimwili”—kuhamia maeneo ya mbali, kuhifadhi vyakula vya makopo na karatasi za chooni, na kujiandaa kuishi nyakati za machafuko. Sio hivyo kabisa! Neno la Mungu badala yake linahimiza maandalizi ya ndani na mtazamo wa utayari wa kukutana na Yesu.
Inahusisha kujitoa kila siku kumfuata Yesu ili tutamani kukutana Naye atakaporudi.
Aina hii ya utayari itatusaidia kutuliza hofu zetu, hasa tunapokumbuka kwamba Yesu anatufariji na kutuambia tusihofu (Isaya 41:10, Mathayo 24:6).
Mwisho wa Mathayo 24, sura inayozungumzia dalili za “mwisho wa dunia,” Yesu anafananisha utayari wa mwisho wa dunia na kuwa “mtumishi mwaminifu na mwenye hekima,” akifanya kwa uaminifu kile ambacho Mungu ametuita tufanye.
Sura inayofuata, Mathayo 25, inatoa mifano mitatu inayoonyesha maana yake.
Mfano wa kwanza—mfano wa wanawali kumi—unazungumzia wanawali watano wenye hekima waliokuwa na mafuta ya kutosha katika taa zao walipokuwa wakimsubiri bwana arusi.
Mafuta hayo yanawakilisha kuwa na Roho Mtakatifu (Zekaria 4:1-7), yakituhimiza kutafuta uhusiano binafsi na Yesu ili Atujaze Roho Mtakatifu, ambaye hutuongoza na kutufariji.
Mfano wa pili—mfano wa talanta—unasimulia hadithi ya watumwa watatu waliopokea “talanta,” fedha, kutoka kwa bwana wao. Wawili kati yao walitumia fedha hizo na kuzizidisha, ilhali mmoja alificha fedha zake ardhini kwa sababu ya hofu.
Fundisho la kisa hiki ni nini?
Mungu anataka tutumie vipawa na uwezo Alivyotupa. Badala ya kuogopa mwisho wa dunia, tunaweza kuwa na bidii katika kumtumikia na kushiriki Injili tunapomsubiri arudi.
Na hatimaye, mfano wa tatu—mfano wa kondoo na mbuzi—unaonyesha umuhimu wa kuishi upendo wa Mungu na kuwajali wasiojiweza. Katika mfano huo, Mungu anawasifu wale waliomtunza Yesu kwa kuwatunza “walio wadogo”—wenye njaa, walio uchi, wagonjwa, na walio gerezani (Mathayo 25:35-40, SUV).
Ujumbe unaopatikana katika mifano hii ni huu: kuwa na uhusiano wa moyoni na Yesu unaotuongoza kutumia vipaji na uwezo wetu kuwahudumia wengine. Hivi ndivyo tunavyojiandaa kwa ajili ya mwisho wa dunia na Kurudi kwa Yesu Mara ya Pili.
Mwisho wa dunia—njia kuelekea ulimwengu bora
Waadventista hupata faraja na amani katika kile ambacho Biblia inasema kuhusu mwisho wa dunia. Kama Wakristo, hatupaswi kuogopa yale yanayokuja!
Badala yake, ukweli wa Biblia unatuchochea kumtafuta Yesu kwa kina zaidi na kuishi jinsi Alivyokusudia tuishi. Ingawa hatuwezi kudhibiti machafuko ya dunia yetu tunapokaribia mwisho wake, tunaweza kupumzika kwa uhakika katika Yeye aliyeahidi kuwa pamoja nasi.
Mwisho wa dunia kama tunavyoijua unaweza kuwa unakuja. Lakini yote haya ni kutuandaa kwa ajili ya ulimwengu bora zaidi—ulio huru kutokana na dhambi na uharibifu wote uliosababishwa nayo.
Kurasa Zinazohusiana
Majibu Zaidi
Tazama Vyuo na Vyuo Vikuu vya Kiadventista
Kwa nje, vyuo vikuu vya Waadventista wa Sabato vinaweza visionekane tofauti sana na vyuo vingine. Lakini tofauti halisi ziko nyuma ya pazia.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria” Kuhusu Kampuni za Nguo?
Dini nyingi zina mwongozo kuhusu mavazi, lakini je, Kanisa la Waadventista wa Sabato lina maoni gani? Gundua jinsi Waadventista wanavyochagua mavazi kulingana na kanuni za Kibiblia.
Mkutano wa Kambi wa Waadventista wa Sabato ni Nini?
Ingawa mikutano ya kambi haikuanza na Kanisa la Waadventista wa Sabato, ni jambo la msingi sana katika utamaduni wa Waadventista.
Ukweli wa Sasa—Ni Nini na Kwa Nini ni Muhimu
Ukweli wa sasa, kulingana na Waadventista wa Sabato, ni imani kwamba ukweli fulani wa Biblia ni muhimu kwa watu wa Mungu katika nyakati maalum katika historia.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria” Za Ndoa?
Dini nyingi au tamaduni ulimwenguni zina mila, taratibu, au matarajio ya kipekee katika ndoa au sherehe ya harusi.
Viongozi wa Kanisa: Ni Nini Majukumu ya Mchungaji wa Kiadventista?
Wachungaji – tumesikia juu yao, lakini wanafanya nini hasa? Hebu tuangalie nafasi ya mchungaji wa Kiadventista katika kanisa.
Biblia Inasema Nini Kuhusu Staha na Adabu?
Biblia inafundisha kwamba adabu, aina ya unyenyekevu na heshima, ni sifa yenye thamani kwa kila mtu—wanaume, wanawake na watoto.
Muhtasari wa Elimu ya Juu ya WaAdventista wa Sabato
Muhtasari wa Vyuo Vikuu Vya Waadventista wa SabatoKanisa la WaAdventista Wasabato lina takribani shule za sekondari 118 ulimwenguni kote.1 Ingawa nyingi zipo ndani ya Amerika Kaskazini, pia utapata vyuo vikuu vya WaAdventista katika nchi mbalimbali duniani—mahali kama...
Waadventista Wasabato Wanatafsiri Vipi Unabii wa Biblia?
Jifunze zaidi kuhusu jinsi Waadventista wanavyotafsiri unabii katika Biblia—hasa katika vitabu kama Danieli na Ufunuo.
Je, Waadventista Wasabato Wana “Sheria”?
Tunashikilia kanuni tunazoamini zitasaidia kuweka uhusiano wa karibu na Yesu na Neno lake. Jifunze jinsi kanuni hizi zinavyo-ongoza mtindo wa maisha wa Waadventista.
Jinsi Waadventista Wanavyoshughulikia Kifo na Mazishi
Mazishi mengi ya Waadventista wa Sabato yanafanana na yale ya madhehebu mengine ya Kiprotestanti, kama vile Wamethodisti, Wabatisti, au Wapresbiteri, lakini unaweza kupata tofauti chache au taratibu za pekee.
Filamu za Kiadventista: Mahali Imani na Filamu Zinapokutana
Tangu mwanzo, lengo la Kanisa la Waadventista wa Sabato limekuwa kueneza kweli ya Mungu katika Biblia.
Ni nini Mtaalam wa Matibabu wa Kiadventista?
Mmishonari wa matibabu katika Kanisa la Waadventista ni mtu anayejali mahitaji ya matibabu ya watu kama njia ya kuonyesha upendo wa Yesu.
Je, Waadventista Wasabato Wanasherehekea Siku Kuu Zinazohusiana na Pasaka?
Kufufuka kwa Yesu, kunakoadhimishwa katika siku kuu nyingi zinazohusiana na Pasaka, ni muhimu katika imani za Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Chakula cha Pamoja Katika Kanisa la Kiadventista: Mahali Ambapo Chakula na Urafiki Vinakutana
Mara nyingi, kawaida kwenye ratiba inayotofautiana kutoka mara moja kwa wiki hadi mara moja kwa mwezi hadi mara moja kwa robo, kanisa la Waadventista litakuwa na “karamu za ushirika,” mara nyingi zikiitwa chakula cha mchana cha pamoja.
Je, Mahubiri ya Waadventista wa Sabato Yako Namna Gani?
Karibu katika kila Kanisa la Waadventista wa Sabato, mahubiri ndiyo kitovu cha ibada kuu—kama ilivyo kwa madhehebu mengi ya Kikristo ya Kiprotestanti.
Wasimamizi wa Waumini Wana Nafasi Gani Ikilinganshwa na Wachungaji?
Neno “Usimamizi wa kidini” linatokana na neno la Kigiriki laikos, ambalo maana yake ni “wa watu.”
Muundo wa Uongozi wa Kanisa la Waadventista wa Sabato.
Kanisa la Waadventista wa Sabato lina mfumo wa uwakilishi unaounganisha makanisa yake zaidi ya 90,000 ulimwenguni na kuwapa washiriki wake nafasi katika kufanya maamuzi.
Kitabu cha Nyimbo cha Waadventista Wa Sabato
Kitabu cha nyimbo cha Waadventista wa Sabato ni kitabu cha nyimbo kinachotumiwa ulimwenguni kote na makanisa mengi ya Waadventista wakati wa ibada zao.





















